SURA YA SITA
Kwa treni hadi Tabora
Ben R. Mtobwa
afari ya Mwanza hadi Tabora ilikuwa
ya kusisimua sana. Ilikuwa safari yangu ya kwanza maishani kusafiri bila
kutumia nguvu za miguu
au mikono yangu. Toka Kigoma hadi
Kagera hadi Mwanza nilitumia mikono au miguu yangu. Toka Kigoma hadi Kagera
hadi Mwanza nilitumia mikono yangu kupiga makasia hadi tulipowasili majuzi.
Safari hii kazi yangu ilikuwa kukaa kitako, kando ya dirisha, huku macho yangu
yakifaidi kilometa zote 453 za safari kwa kuburudishwa na mazingira aina aina.
Tulisafiri kwa aina mpya ya usafiri
iliyotambulishwa nchini na utawala wa Mjerumani, gari moshi. Ujenzi wa reli,
vyuma imara ambavyo vilitumiwa na gari moshi hiyo kuteleza juu yake, ambao
ulianza huko Darisalama mwaka 1912 uliweza kufika Mwanza 1923, ikiwa moja ya
matawi ya reli hiyo lililoanzia Tabora. Reli hiyo, maarufu kama reli ya kati
inayokata nchi toka mashariki hadi magharibi na toka kaskazini hadi kusini inakadiriwa
kuwa na urefu wa kilomita 2600. Ni moja kati ya kumbukumbu za utawala wa
mjerumani, ambazo kamwe hazitafutika katika historia ya nchi hii.
Reli hii ni kiungo pekee muhimu
kinachoiunganisha nchi toka bahari ya hindi kwa upande mmoja hadi ziwala Tanganyika
kwa upande wa pili, jambo linaloifanya iwe tegemeo kubwa kwa usafirishaji wa
watu na mizigo si kwa nchi yetu pekee bali pamoja na zile za Burundi, Kongo na
Rwanda pia.
Licha ya sababu hizo za kiuchumi
reli ilikuwa pia mshirika mkubwa katika masuala ya kiutamaduni na kijamiii
nchini. Kwanza iliwezesha makabila yapatayo mia na ishirini ya Tanganyika
kufahamiana kwa urahisi. Mzaramo wa pwani angeweza kukutana na Mmanyema wa
Kigoma, au Mchaga wa Kilimanjaro kufahamiana na Mfipa wa Mpanda kwa urahisi zaidi
ya siku zile za akina Livingstone kutumia miaka maporini toka pwani ya Bahari
ya Hindi hadi pwani ya ziwa Tanganyika.
Na hilo halikuwa kwa makabila ya
ndani tu. Ujenzi wa reli hiyo ulimfanya mkoloni wa Kijerumani alete vibarua
wengi wa kazi hiyo toka nchini India. Hawa ni chanzo cha msamiatai wa ‘kuli’
neno lililozaliwa kutokana na lile la kiingereza ‘Coolie’ wakatii huo
likitumiwa kama kashfa kwa vibarua wasio na ujuzi wowote. ‘Kuli’
haikutofautiana sana na ‘manamba’ wa hapa nyumbani ambao walikamwatwa kwa
visingizio mbalimbali kubwa ikiwa kushindwa kulipa kodi ya kichwa, na kupelekwa
kufanya kazi za mikono katika mashamba ya mkonge kaskazini magharibi mwa nchi
yetu.
‘Kuli’ wengi walitoka India, ama
walinogewa, ama hawakuwa na uwezo wa kurudi kwao, ama yote mawili, wakaishia
kuwa wakazi wa hapa. Leo hii jamii mpya ya akina Gulamali, Manji, Adamjee; na
kadhalika inapatikana sehemu yoyote ya Tanganyika; hasa vijijini.
Jing – janga – jing – jang – jing -
jang garimoshi lilihangaika kuvuta mabehewa sita wa abiria na manne ya mizigo
yaliyofanya tuwe kama joka refu linaloteleza kwa kujikongoja.
Injini ya garimoshi hilo, ambayo
sikuhitaji kuambiwa kuwa ilikuwa ikitumia kuni kutengenezea mvuke wa kuiendesha
ilikuwa ikitoa moshi mwingi na mzito sana. Moshi ambao ulilala juu ya treni
kama wingu jeusi lisilopendeza machoni. Nadhani hiyo ni sababu pekee
iliyowafanya waswahili waamue kuita usafiri huo wa ‘garimoshi.’
Nikiwa nimeketi raha mustarehe
dirishani pangu nililitazama kwa masikitiko ziwa nililolipenda la Nyanza
likitokomea machoni mwangu taratibu. Ziwa hilo lilinilea, lilinihifadhi na
kunifadhili kwa muda wa kutosha. Ndilo lililonifundisha kuogelea na kutafuta
pesa. Ziwa lililonitoa Kagera na kunifikisha Mwanza. Hilo ndilo ziwa ambalo leo
naliacha bila kuwa na uhakika wa kuliona tena. “Nitarudi!” nilinong’ona
taratibu.
“Nini?” jirani yangu, mzee wa makamo
ambaye tulichangia kiti, alinihoji akidhani nazungumza naye.
Sikumjibu.
Tukapinda na kupenya katikati ya
majabali marefu mfano wa milima. Tuliacha jabali moja baada ya jingine, mbuyu
mmoja baada ya mwingine huku tukivuka vijito na mito ya hapa na pale.
Mara tukazama katika mapori na
misitu mikubwa, kwa mbali tukawaona wanyama mbalimbali kama ngedere waliokuwa
wakirukaruka kwenye miti au mbuzimawe ambao walirandaranda juu ya majabali ya
hapa na pale. Katika eneo moja lenye mabwawa tuliwaona ndege aina ya flamingo
wenye miguu mirefu na midomo myekundu wakiwinda samaki au wadudu ndani ya maji
hayo. Ndege wengine, aina mbalimbali pia walikuwa wakiruka huku na huko kama
wanaotushangaa au kutushangilia hadi tulipotokomea.
“Mantare!” Yule jirani yangu
aliropoka.
Ikawa zamu yangu kumshangaa, “Nini?”
nilimuuliza.
“Tumefika stesheni ya Mantare,”
alifafanua.
Kweli. Nililiona garimoshi
likipunguza mwendo na hatimaye kusimama kando ya nyumba mbalimbali ambazo
zilionekana kuwa za wafanyakazi wa reli hiyo.
Palikuwa na purukushani fulani, watu
wakipanda wengine wakishuka. Miongoni mwa watu hao walikuwepo pia
wafanyabiashara wenye bidhaa mbalimbali kama vyakula, mapambo na mifugo.
Walionunua walinunua, wasionunua tulijifanya hatuoni.
Tulisimama hapo kwa dakika kumi tu.
Mara garimoshi hilo lilianza tena safari yake kwa mwendo wake wenye maringo, taratibu
kama halitaki na baada ya kuchochea huku likikohoa kwa uzito wa mabehewa.
“Kwimba!” mzee aliropoka tena.
Nilikuwa nimeanza kusinzia. Nikafunga macho na kuona tukiingia katika stesheni
nyingine. Nikatoa kichwa dirishani na kuwatazama wanaoshuka na kupanda.
Tukaondoka.
Jirani yangu huyo alikuwa amejipa
kibarua. Kila tulipokaribiakituofulani nilimsikiaakitamkakwanguvu,“Malya,”
kisha “Seke.” Sikufumbua macho yangu hadi pale aliponitikisa kwa nguvu huku
akiniambia, “Amka tumefika Shinyanga!” nilifumbua macho. Jina la Shinyanga
lilikuwa na uzito wake katika kumbukumbu zangu. Hata hivyo, nilimwambia
taratibu “Siendi Shinyanga. Nakwenda zangu Tabora.”
“Tabora! Kuna nini Tabora?”
Sikumwelewa, “Kuna nini Tabora?”
nikamjibu kwa swali jingine. “Kwani Shinyanga kuna nini?”
Kumbe mzee alikuwa na hamu ya
maongezi. Alianza kwa kutabasamu. Baadaye aliporomosha sifa za Shinyanga. Kuna
kila kitu ambacho binadamu anahitaji. Ardhi bora yenye rutuba tele. Misitu
imejaa wanyama kila aina. Ng’ombe wa hapa wamenenepa na wanatoa maziwa mengi
kuliko popote pale. Hata Wazungu wengi siku hizi wanatembelea milima yetu mara
kwa mara. Kuna fununu kuwa huko ardhini kuna mali nyingi ambazo huko kwao ni
utajiri mkubwa.”
Nilitabasamu lakini sikumjibu.
Sikuwa na jibu la haraka.
“Enhe na Tabora?” alihoji. “Tabora
nini?” nilimuuliza. “Kuna nini Tabora?”
Niliamua kumnyamazisha kwa kumpa
kile ambacho nilikipata vitabuni, ambacho nina hakika kuwa alikuwa hakijui.
“Tukianza na reli hii tunayoitumia sasa. Roho yake iko Tabora.”
“Kwa vipi?” alihoji akicheka.
“Tabora ni kituo pekee muhimu sana.
Pale Tabora ndipo ambapo reli hii inajigawa, moja ikienda Kigoma, ambako
inafika hadi ziwa Tanganyika linalotuunganisha na nchi za Kongo, Burundi na
Zambia. Pia, kuna reli inayokwenda hadi Mpanda, kusini mwa nchi yetu.”
Wakati akitafakari hilo nilimpa la
pili. “Unaijua eropleni?” nilimuuliza.
“Ndege Ulaya!” alisema akicheka.
“Sio naijua, nimeipanda mara nyingi.”
“Kutoka wapi kwenda wapi?”
nilimuuliza kwa mshangao. “Burma,” alinijibu. “Kwenye vita kuu ya kwanza nilikuwa
mmoja wa wapiganaji tuliorushwa kwa ndege kwenda kusaidia
wenzetu waliozingirwa na maadui,”
alisita kidogo kabla ya kuniuliza, “Ndege ina uhusiano gani na Tabora?”
“Tarehe 22 Julai mwaka 1920 ndege ya
kwanza kutua nchini Tanganyika ilitua katika uwanja wa ndege Tabora. Ndege hiyo
ndogo ya Mwingereza iliruka toka Nairobi Kenya hadi hapa na kuweka historia ya
pekee kwa nchi ya Tabora.
Mzee alicheka. “Hilo tu?”
aliniuliza.
“Yako mengi, “ nilimjibu. “Yule
kiboko wa Waarabu, Mtemi Milambo, aliishi katika ngome yake Iselemagazi
iliyokuwa Tabora. Yule Mwingereza Davidi Livingstone aliyekataa kurudishwa kwao
na akafia Zambia alipata kuishi Tabora kwa muda, kabla hajahamisha makazi yake
Ujiji, Kigoma. Tabora ulikuwa mmoja kati ya miji michache nchini iliyokuwa na
watu wengi, toka miaka ya 1700, mji mdogo huo?”
Mzee aliyatafakari maneno yangu.
“kichwa chako kinafanya kazi vizuri sana, mjukuu wangu. Naweza kutabiri
unakwenda Tabora kufanya nini.”
“Naenda kufanya nini?” nilimjaribu.
“Kusoma,” alinijibu. “Kweli au uongo?” “Kweli tupu.”
Mzee akacheka kabla hajaongeza,
“Naweza hata kukuambia jina la shule unayokwenda.”
“Shule gani?”
“Unakwenda Tabora School. Shule ya
misheni inayopokea watoto wa machifu. Kweli au uongo?”
“Ni kweli,” nilimjibu kwa mashangao.
“Umejuaje mzee?” “Uzee dawa. Uzee ni kuona mengi ni kuona mbali. Jinsi
ulivyovaa, jinsi ulivyotulia, jinsi unavyoongea, ni wazi kuwa wewe ni mtoto wa
Chifu. Na nina imani kuwa utafika mbali
katika safari yako ya maisha.”
Nilitamani kucheka, nilitamani
kulia. Sikujua nifanye lipi katika hayo. Kwa mara ya kwanza, baada ya muda
mrefu nikamkumbuka babu yangu, mzee Kionambali.
Mtoto wa Chifu!
* * *
Tulifika Tabora siku mbili baadaye.
Stesheni ya Tabora ni sehemu moja
yenye kila aina ya pilikapilika. Ilikuwa na watu wengi wenye purukushani hii na
ile, huyu akihangaika kupanda behewa, huyu akishuka, yule akibadili behewa
kuhamia lile, huyu akipiga kelele kuuza asali na bidhaa nyingine na kadhalika
na kadhalika. Lakini purukushani kubwa zaidi ilikuwa ya magarimoshi yenyewe.
Vichwa vilikuwa vingi mno, vikienda hapa au pale, kuhamia reli hii au ile huku
vikicheua moshi na honi za mara kwa mara, hali iliyofanya pawe mahala ambapo
mtu asingependa kukaa kwa muda mrefu.
Nilishuka, nikachukua mzigo wangu na
kutoka nje ya stesheni. Huko nje kitu cha kwanza kilichovuta macho yangu ni
wingi wa maembe. Barabara nzima toka stesheni hadi mjini zilizingirwa na miembe
mikubwa, kila upande kwa namna iliyofanya iwe na kivuli murua cha kusisimua.
Nilipiga hatua moja kwenda nyingine kuifuata barabara hiyo ya aina yake. Kila
hatua ilinifanya nione kuwa wingi huo wa miembe haukuwa wa kando ya barabara
pekee. Mapori yote ya mji yalitawaliwa na miembe mingi, mikuwa, ambayo baadhi
ilikuwa na maembe yaliyoiva, ambayo yalionyesha kuwa watoto wa mji huo
walishachoka kuyala.
Mji wa Tabora ulikuwa mdogomdogo,
wenye nyumba za kawaida, ambazo hazikutofautiana sana na zile za Mwanza.
Tofauti pekee kubwa niliyoiona ni mavazi na lafudhi. Kimavazi
nilishangaa kuona watu wengi wakiwa
wamevaa mavazi yenye asili ya Kiarabu, kanzu nyeupe na kiko mdomoni kwa wanaume
na baibui jeusi lililofunika moja ya kumi ya mwili isipokuwa sehemu ndogo ya
uso kwa wanawake. Katika mazungumzo yao nilibaini pia kuwa lafudhi ya wengi wao
ilikuwa ya Pwani zaidi. Japo walizungumza kwa namna iliyofanya nihisi ama
wanaibembeleza lugha ama inateleza kwenye ndimi zao.
‘Karibu Tabora mwanangu!’
nilijikaribisha.
Nikauliza njia ya kwenda shule ya
Tabora School. Nikaelekezwa. Nikaifuata njia hiyo taratibu, mzigo mkononi,
mluzi mdomoni, ndoto za mafanikio zikiwa tele moyoni.
Nilipokelewa na mlinzi nje ya geti
la kuingilia shuleni. Nikajitambulisha kwake. Alinifungulia geti na kunielekeza
iliko ofisi ya mkuu wa shule. Nilikwenda kwa mwendo wa kujiamini, huku nikiwa
tayari nimetoa barua yangu ya utambulisho toka kwa ‘baba yangu,’
Chifu Masanja mwana Kasanga.
Wanafunzi wenzangu tayari walikuwa madarasani. Niliweza kuwasikia baadhi ya
walimu wakifoka kwa sauti kubwa katika jitihada za kujaribu kuingiza kitu
fulani katika vichwa vigumu vya wanafunzi.
Karani wa mkuu wa shule alinipokea,
akaipokea barua yangu na kuiingiza chumbani kwa bosi wake. Muda mfupi baadaye
niliitwa katika ofisi hiyo.
Mkuu wa shule alikuwa Mzungu. Mtu
mnene miraba minne, ambaye angefaa zaidi kuwa mwalimu wa ngumi badala ya
taaluma. Nilimkuta kasimama nyuma ya meza yake, barua yangu ikiwa mkononi
mwake. Alinikazia macho makali kwa dakika moja au mbili kabla hajatamka neno
moja tu “Keti.” Nikaketi kwenye kimoja wapo cha viti viwili vilivyomuelekea
mwalimu mkuu, miguu yangu ikianza kupoteza nguvu, mikono
ikianza kutetemeka kwa sababu ambayo
sikuifahamu. “Barua yako hii?” alinihoji baadaye.
“Ndiyo.” “Umeipata wapi?”
“Kwa nini? Nimepewa na Chifu… baba…
nikuletee.” “Chifu nani?”
“Masanja mwana Kasanga.”
Mkuu huyo wa shule alinitazama kabla
hajaongeza swali jingine, “Unaitwa nani?”
Nusura nitaje jina langu halisi.
“Cheyo,” nikatamka.
Nilimwona mkuu wa shule akizidi
kushangaa. Mara akawa kama kakumbuka jambo. Akatoka na kumnong’oneza jambo
karani wake. Kisha akarudi na kuketi. Muda mfupi baadaye mlango uligongwa,
mwanafunzi mmoja akaingia na kuelekezwa kuketi kiti cha pili kilichokuwa wazi.
Mkuu wa shule akimkazia macho kama
alivyofanya kwangu kabla ya kumuuliza, “Ulisema wewe ni nani, unatoka wapi na
baba yako ni nani?”
“Naitwa Cheyo. Kwetu Mwanza. Mimi ni
mtoto wa Chifu Masanja mwana Kasanga.”
Miguu yangu iliishiwa nguvu.
Nilitamani ardhi ipasuke, inimeze yaishe. Ardhi haikufanya hivyo. Nikahisi
nimeanza kutetemeka mwili mzima, jasho jembaba likinitoka.
Mkuu wa shule alikuwa akinitazama
kwa makini. “Nani anasema uongo, nani anasema ukweli kati
yenu?” aliniuliza. “Juzi tu,”
aliongeza. “Alikuja huyu kijana, akatuambia kwamba anaitwa Cheyo na ni mtoto wa
chifu Masanja. Kwa maelezo yake baba yake hataki aje shule, anataka akae
nyumbani kusubiri kurithi Uchifu wake atakapokufa. Kwamba amekuja hapa shuleni
kwa kutoroka baada ya
jitihada za kumsihi baba yake
kumruhusu kushindikana. Na kwa jina na nafasi yake ilikuwa wazi bado tumempokea
na kumruhusu kuendelea na masomo. Leo umekuja wewe. Unadai wewe ni Cheyo mtoto
wa Chifu Masanja na una barua yake ya kuomba upokelewe hapa. Nataka kujua nani
mkweli nani mwongo kati yenu,” aliniuliza akitutazama kwa zamu. Cheyo naye
alishangaa. Akageuka kunitazama. Nilijitahidi kuinua uso wangu nimtazame pia,
ilikuwa kazi ngumu kuliko zote nilizopata kufanya. Hicho kidogo nilichobahatika
kuona katika uso wake kilionyesha wazi kuwa si kwamba hatufahamiani tu, bali
pia tulikuwa hatufanani kwa namna yoyote ile. Pale ambapo mimi nilikuwa mng’avu
yeye alikuwa mweusi tii, pale nilipokuwa mrefu yeye alikuwa mfupi na mwenye
kiribatumbo. “Mnafahamina?” mkuu wa shule aliuliza baada ya
kutupa dakika za kutumbuliana macho.
Wote tulitikisa vichwa kukataa.
Mkuu wa shule akacheka, “Iweje
watoto wa mtu mmoja, tena waotumia jina moja wawe hawafahamiani?”
Hatukumjibu.
Haikumchukua mkuu wa shule muda
mrefu kubaini ukweli wa mambo hayo. Kutokana na udadisi wa Chifu Masanja juu ya
kumpeleka mwanae shule, bila shaka kwa muda mrefu sasa, ndipo akabuni hila ya
kuteua mtu mwingine ili aache kusumbuliwa, jambo ambalo limetibuka baada ya
mwanawe kutoroka nyumbani na kuja shuleni bila ridhaa wala khiari yake.
Mkuu huyo alinikazia macho kama
anayesubiri uthibitisho wa kile kinachopita katika fikra zake bila kutamka.
Nilitamani asome jibu la ‘ndiyo’ katika nafsi yangu ili yaishe, niondokane na
aibu hiyo. Nadhani alisoma hilo katika macho
yangu, kwani nilimsikia akisema
taratibu, “Sipendi kuchezewa. Sipendi kudanganywa. Natoa dakika kumi tu, yule
ambaye anafahamu kati yenu kuwa si mtoto halali wa Chifu masanja aondoke mbele
yangu na ndani ya eneo la shule yangu. Vinginevyo, nitamchukulia hatua kali za
kisheria.”
Sikungojea dakika hizo kumi. Moja tu
ilinitosha. Niliinuka, nikachukua begi langu na kutoka taratibu. Nyuma yangu
nilisikia kicheko, kicheko ambacho kiliashiria mwisho wa ndoto yangu ya kupata
elimu zaidi ya ile ndogo niliyokuwa nayo.
* * *
Niliduwaa kwa muda nje ya eneo la
shule. Nilihisi akili yangu ikiwa imedumaa kiasi kwa kuwa mvivu wa kufikiri,
hali ambayo ilitokana na uchovu wa ubongo wangu kwa ajili ya tukio hilo zito.
Nikatafuta kivuli na kukaa.
Kelele za wanafunzi ambao walikuwa
wakitoka, ndizo zilizonizindua hapo chini ya mwembe nilipoketi. Nikainuka
nikachukua begi langu na kuitumia miguu yangu kuniondoa hapo. Sikujua naelekea
wapi. Lakini sikushangaa pale miguu yangu iliponifikisha stesheni ya treni,
mbele ya dirisha la mkata tiketi.
“Nipe tiketi,” nilimwamuru. “Ngapi?”
“Moja.”
“Ya kwenda wapi?”
Niende wapi? Nilijiuliza. Sikuhitaji
kujiuliza sana, “Tiketi yoyote ile. Kigoma, Dar es Salaam au Mpanda,”
nilimjibu.
Mkata tiketi huyo alinitazama kwa
macho ya mshangao wa muda, akinichungulia toka katika kijidirisha chake.
“Unaumwa?” baadaye alinihoji.
Sikutarajia swali hilo, “Kuumwa!
Kuumwa nini?” “Chochote kile. Kama akili hivi?”
Ikawa zamu yangu kumshangaa, “Kwa
nini uniambie hivyo?” nikafoka.
“Mtu yeyote asiyejua anakokwenda ama
ni mngonjwa wa akili, ama ameiba anataka kukimbia. Wewe uko katika kundi gani
katika hilo?”
Lilikuwa swali la kifedhuli kuliko
yote. Lakini nadhani alikuwa akinitendea haki. Mwenyewe pia nilianza kujishuku.
Ninakwenda wapi? Ninakimbia nini? Nimechanganyikiwa kwa kupoteza nafasi yangu
nyingine ya kupata elimu? Lakini mara ngapi nimesikia kuwa kukosa elimu ya
darasa siyo mwisho wa elimu duniani? Wangapi duniani wamefanya maajabu na
kuingia katika vitabu vya kihistoria kwa kiwango cha elimu kama yangu au ndogo
zaidi.
Wazo hilo lilinifanya niangue
kicheko. Nilicheka kwa muda wa dakika mbili nzima mpaka nikapaliwa. Nikaanza
kukohoa.
Kicheko changu kilifanya mkata
tiketi huyo aamini hisia zake, kuwa naumwa. Na siumwi kitu kingine zaidi ya
akili. Nilimwona akichukua simu na kuzungusha namba kadhaa. Alizungumza kwa
sauti ya kunong’ona huku akiwa amenikazia macho ya tahadhari. Baada ya hapo
alifunga dirisha lake.
Huku nikicheka niliinua begi langu
na kuanza kuondoka eneo hilo. Lakini sikuweza kupiga zaidi ya hatua kumi kabla
sijajikuta nikivamiwa na watu wawili waliovaa sare za polisi, shati na kaptula
za kaki, kofia zilizovaliwa upande, soksi na viatu vyeusi. Mkononi kila mmoja
alikuwa na rungu.
“Polisi! Tulia kama unanywolewa!”
mmoja aliniamuru.
Nikiwa nimeshikwa na mkanda wa
suruali kwa nyuma, hali iliyofanya nining’inie juu juu na kutembelea ncha za
vidole vyangu sikuwa na nguvu zozote za kujitetea. Niliburuzwa hadi katika
chumba chao kidogo ambako nilisukumwa na kufungiwa kwa nje bila kuulizwa swali
lolote.
“Nimefanya nini jamani?” niliwapigia
kelele. Hakuna aliyenijibu.
SURA YA SABA
Lyampa Mfipa
ilipohoojiwa na polisi kwa dakika
kumi tu kabla hawajathibitisha kuwa nilikuwa na akili zangu timamu. Lakini
ilikuwa baada ya kufungiwa
chumbani humo kwa siku nzima.
Alikuja mmoja kati ya wale
walionikamata, akiwa amefuatana na mtu mwingine mfupi, mnene, ambaye alinukia
dawa za hospitali. Sikuhitaji kuambiwa kuwa mtu huyo alikuwa daktari, pengine
wa maradhi ya akili, toka hospitali ya Kitete. Walipoingia ndani yule daktari
aliketi mbele yangu na kunikazia macho. Mie pia nikamkazia macho. Hata hivyo, nusu
dakika baadaye niliyakwepa macho yake kwa kuinamisha uso wangu.
Akiwa bado amenikazia macho daktari
yule alitabasamu, mimi sikutabasamu. Aliangua kicheko. Mimi sikufanya hivyo.
Kisha alitikisa kichwa chake kwa kujiyumbisha huku na kule kama aliyekusudia
nifuate mfano wake. Sikufanya hivyo. Nikamwona kama mtu aliyepatwa na mshangao.
“jina lako?”
Nikamjibu kwa kutaja lile nililopewa
na chifu Masanja, “Cheyo.”
“Kabila lako?”
“Msukuma. Ingawa sikijui vizuri.”
“Kwa nini?”
“Nilizaliwa na kukulia Buha.
Nafahamu Kiha kuliko kisukuma.”
“Mwakeye!” Akanijibu.
“Saa hizi sio mwakeye, ni mwidiwe,”
nikamsahihisha.
Akatabasamu. Nadhani akiba yake ya
Kiha ilikuwa inaishia pale, kwani alirudi kwenye Kiswahili. “Enhe, una tatizo
gani?” alihoji.
“Nadhani hawa walionifungia hapa
ndio wenye matatizo. Wamenikamata bila sababu na kunifungia humu bila maelezo,”
nilisema kwa sauti yenye hasira.
Daktari huyo alinitazama kwa makini,
toka kichwani hadi miguuni. Mavazi yangu yalikuwa safi, viatu vyangu viking’ara
kwa kiwi. Hata mwili wangu pia ulikuwa safi, ukimeremeta kwa afya na mafuta
niliyopaka kabla ya kwenda mbele ya mkuu wa shule ile iliyonikataa. Begi langu
pia lilikuwa safi, jipya, lililofura mali ambazo mgonjwa wa akili hawezi kuwa
nazo. Daktari huyo aliacha kunitazama mie akawa akimtazama yule askari.
Nilihisi kuwa alikuwa katika wakati mgumu wa kuamua nani mgonjwa wa akili kati
yangu na hao walionikamata. “Wamekuhangaisha bure,” alisema baadaye. “Ilikuwa
tukukamate, upelekwe Dodoma kwenye hospitali ya wenye maradhi ya akili.
Unaonekana huna tatizo loolote.”
Askari huyo hakuweza kunitazama
usoni kwa aibu.
Mara niliporuhusiwa, nilichukua begi
langu na kurudi katika dirisha lilelile la mkata tiketi. Nilimkuta karani
yuleyule bado akiwa kazini. “Nataka tiketi,” nilimwamuru.
Aliponitazama alishtuka kama
aliyeguswa na waya wa umeme. “Ya kwenda wapi?” alinihoji kwa sauti ambayo
haikuwa imara kama awali.
“Popote,” nilimjibu kama awali.
Alitazama huko na huko kama
anayetaka kuomba msaada. Kisha akasema, “Leo kuna treni mbili. Moja inakwenda
Kigoma, itapita usiku. Nyingine inakwenda Mpanda, itaondoka hapa baada ya nusu
saa.”
Nipe ya Mpanda.” Nilisema bila ya
kufikiri sana.
“Shilingi tano, njia moja.”
“Nipe,” nilimjibu nikimlipa.
Nikapokea tiketi na chenji zangu na kuzitia mfukoni. Nikaenda mgahawa mmoja
uliokuwa karibu ambapo nilinunua wali kwa maharage, nikayashushia kwa chai ya
rangi. King’ora cha abiria wa treni ya Mpanda kilipolia nilikuwa mmoja wa
abiria wa kwanza kuiparamia.
* * *
Sikuhitaji kufikiri sana kabla ya
kukata tiketi hiyo kwa sababu nyingi. Kwanza, nilikuwa na hisia kuwa Tabora
haukuwa mji wangu wa bahati. Kuumbuliwa na mkuu wa shule kwa kiwango kile
kulinitia doa na dosari kubwa iliyofanya nijisikie aibu isiyo na kifani. Mimi
sio yatima. Nina baba na mama. Nina babu mwerevu kuliko mamia ya mababu
ninaowajua. Kiu ya elimu haikuwa sababu nzuri ya kunifanya nikubali wazo la
kipuuzi la kufanywa mtoto wa kambo wa Chifu Masanja.
Ni wazo hilo lililofanya nitupilie
mbali wazo la kurejea Usukumani. Ningemwambia nini Chifu?
‘Nimebainika. Mtoto wako halisi yuko
shuleni, kwa hiyo nitafutie hifadhi mpya!’ Aibu iliyoje. Ningemwambia nini
mkewe na watumishi wa himaya yake ambao bila shaka wengi waliijua
kinachoendelea?
Ndipo nilipowaza juu ya kurudi
nyumbani. Nipande garimoshi hadi Kigoma, huko nitafute njia ya kufika Kasulu.
Huenda tayari kulikuwa na malori ambayo yalibeba watu na mizigo kama sehemu
nyingine za nchi.
Hata hivyo, hilo pia sikulitekeleza
kwa sababu tele. Moja ilikuwa aibu. Mwanamume akitoka ametoka. Akirudi ana kitu
cha kuonyesha kijijini. Ama vyeti vya kuhitimu masomo yako ama fedha au mtaji
au kujenga nyumba bora zaidi. Mimi ningerudi na aibu tupu. Sikuwa tayari
kufanya hivyo.
Sababu nyingine iliyonizuia kwenda
nyumbani ni babu yangu. Ni kweli alinipenda sana na angefurahi sana kuniona.
Lakini sikupenda kujitokeza mbele yake kichwa kitupu, mikono mitupu. Alitegemea
nirudi na elimu. Alitegemea nirudi na mali. Kamwe asingefurahi kuona nikirudi
mnyonge, kama kinda la ndege, linalotegemea mama akutafutie, akutafunie, umeze.
Lakini kuna sababu nyingine, kubwa
zaidi, iliyonifanya nisijisikie kumtazama babu machoni. Hirizi yake. Hirizi
hiyo ya familia, ambayo kwa mujibu wa maelekezo yake ilivaliwa na babu yake,
baba yake na kisha yeye mwenyewe. Hirizi ambayo ilimpeleka Ughaibuni na
kumrejeshha salama. Naam, hirizi ambayo aliivua na kunivisha mimi, badala ya
baba, ili nipate kile ambacho aliamini kingeinua ukoo na familia yetu.
Hirizi ambayo niliipoteza kwa
uzembe!
Haikuwa kweli kuwa chanzo cha
migogoro yangu hii mipya, ikiwa pamoja na kukataliwa nafasi ya kusoma, kwa
namna moja au nyingine ilihusiana na kupotea kwa hirizi ile? Mara kwa mara
niliwaza.
* * *
Gari moshi liendalo mpanda
hulazimika kueleka magharibi kwa kilometa kadhaa kabla ya kuchepuka kuelekea
kusini. Kwangu mimi ilikuwa sawa na kuelekea nyumbani, Kigoma. Tuliiacha
stesheni ya Tabora, tukatafuna reli hadi Usoke. Toka hapo tuliingia Urambo.
Tuliacha Urambo na kufika Kaliua ambako tulianza safari ya kusini.
Kama ilivyokuwa safari ya kutoka
Mwanza safari hii pia ilikuwa sawa na kusafiri katikati ya bustani ya Eden.
Kila upande tulizungukwa na ama misitu minene iliyoashiria kila aina ya hazina,
ama mapori ya kutisha yaliyoonya juu ya wingi wa mbolea katika ardhi yake.
Mara kwa mara tulipishana na wanyama
ainaaina waliokuwa kando wakitushangaa, pamoja na ndege ainaaina walioruka hapa
na pale juu ya miti, wakifaidi asali ya maua na wadudu wadogowadogo. Baadhi ya
maeneo kulikuwa na mabwawa makubwa yaliyoshawishi kilimo cha mpunga au mito
ambayo ilinikumbusha samaki wa ziwa Nyanza.
Toka Kaliua tuliingia Mfulu, baadaye
Ugalla na hatimaye tukawasili Mpanda. Huo ulikuwa mwisho wa reli hii, lakini
haikuwa mwisho wa safari yangu.
Pamoja na shahuku yangu kubwa ya
kuondoka Tabora, ndoto yangu ya kuja Mpanda ilikuwa na malengo yake. Zilikuwepo
fununu za hapa na pale kuwa maeneo mbalimbali ya huku yalikuwa dhahabu.
Uchimbaji wa dhahabu hiyo sikuona kama kwa namna yoyote ile ungenishinda.
Kuchimba udongo hadi ufikie mchanga maalumu kuchekecha mchanga huo hadi uone
chembechembe za dhabahu na kuiokoteza, vipi kungenishinda?
Hilo lilikuwa wazo la kwanza. Wazo
la pili, ambalo nilikuwa na hakika nalo zaidi ni uvuvi. Toka Mpanda hadi
Ikola au Kerema ambayo ni miji ya
kandokando mwa ziwa Tanganyika haikuwa safari ndefu. Ningeweza kufika huko hata
kwa miguu. Nilipanga, kama kazi ya kuchimba dhahabu ingeshindikana ningeelekea
huko na kujiunga na uvuvi. Ndiyo, nasikia ziwa Tanganyika lina kina kirefu
kuliko maziwa yote duniani. Kama kuna ukweli kwa hilo bila shaka samaki wake
pia ni wengi zaidi na watamu zaidi. Ningekuwa mmoja kati ya walaji wake. Wala
nisingeishia kula tu; samaki hao wangenipatia fedha za mtaji ili nirudipo kwetu
nirudi kishujaa. Hivyo ndiyo ilikuwa ndoto yangu. Kwa bahati, nzuri au mbaya,
haikwenda kama nilivyotarajia. Hali hiyo ilitokana na kukutana kwangu ana kwa
ana na mtu ambaye sikutarajia kamwe kumwona tena katika maisha yangu, mtu
ambaye sikupata hata kulifahamu jina lake. Alikuwa mmoja kati ya wale Wamanyema
wawili waliofuatana na Mwarabu katika safari yetu ya miguu toka Buha hadi kwa
Wahaya, miaka zaidi
ya mitano iliyopita.
Ni yeye aliyeniona kwanza, “We mtoto
wewe! Kama nakufahamu vile?”
Nikageuka kumtazama. Mara moja
nilimkumbuka, “Mmanyema! Unafanya nini huku?” niliuliza kwa mshangao.
“Wewe je? Umefikaje huku?” Sikujua
nimweleze nini. “Babu yako hajambo?”
Sikuwa na jibu. Nikainamisha uso kwa
aibu.
Nadhani Mmanyema alisoma kitu fulani
katika uso wangu, kwani alinitazama kwa muda kabla hajanikaribisha chai kwa
mihogo ambayo alikuwa akiila. Nikapokea kikombe cha chai ya maziwa na kipande
cha muhogo. Njaa iliyoanza kuninyemelea ikakimbia mara moja.
Wakati tukinywa chai hiyo yapata saa
kumi na moja za alfajiri. Gari moshi lilikuwa limechelewa sana njiani kutokana
na mafuriko katika maeneo mbalimbali. Ilibidi gari hilo liendeshwe taratibu
sana. Tulikuwa tumeketi nje ya stesheni, kwenye benchi la chuma ambalo bila
shaka lilijengwa kwa ajili ya wasafiri.
Nilishangaa pale Mmanyema
aliponiambia kuwa tulisafiri katika behewa moja toka Tabora hadi hapo. Kuwa
aliniona lakini hakuwa na hakika na macho yake hadi aliposikia sauti yangu na
kuniona nikimkumbuka.
Alikuwa mzungumzaji sana mzee huyu.
Alinieleza jinsi alivyoacha kazi ya kumtumikia yule Mwarabu baada ya
kufilisika. “Yaelekea Mwarabu yule hakuwa na ujuzi wowote zaidi ya biashara ya
watumwa. Kila alichojaribu kushika kiliteleza. Hata mishahara yetu alishindwa
kulipa. Tukaachana naye na kuanza shughuli zetu binafsi,” Alinieleza kwamba
yeye sasa alikuwa akifanya biashara ya kununua dagaa toka kwa wavuvi
wadogowadogo wa kandokando ya ziwa Tanganyika na kuwauza kwa walanguzi wakubwa
ambao waliwapeleka Tabora, Dodoma na Dar es Salaam kwa matumizi ya binadamu na
mifugo. Kwamba sasa hivi alikuwa na mtaji wa kutosha ambao utamwezesha kupeleka
mwenyewe dagaa hao hadi Dar es Salaam ili apate faida kubwa zaidi. “Toka huku
nitanunua nyavu na vifaa vingine vya uvuvi na kuwauzia watu Kigoma na Kongo.
Nikijaliwa miaka miwili baadaye nitakuwa mmoja wa matajiri wakubwa wa nchi
hii,” alisema kwa kujipamba.
“Sasa unakwenda wapi? Mbona huku
hakuna dagaa?” nilimuuliza.
“Nakwenda Sumbawanga.” “Kufanya
nini?”
Alinitazama na kucheka kidogo kabla
hajasema, “Unaonekana wewe ni mtoto mdogo sana kuliko umbile lako. Hujui watu
huenda Sumbawanga kufanya nini?”
Mie: Sijui
Yeye: Pole sana. Kwa hiyo, hata
maana ya jina Sumba
- Wanga hujui?
Mie : Sijui
Alitikisa kichwa kwa namna ya
kunisikitikia. Kisha alisema, “Sumba-Wanga maana yake ‘Tupa Uchawi.’ Kwa maana
ya kuwa mji huo ni wa watu wazito, watu waliokomaa. Hivyo, ukiingia huko na
vijiuchawiuchawi vyako utaumbuka. Ni huko ambako watu wazima huenda kugangwa, ili
wasichezewechezewe ovyo kishirikina. Huwezi kufanya biashara kama hujafundwa
ukafundika.”
Ilikuwa habari mpya kwangu.
Niliipokea kwa mshangao na kutoamini. “Lakini Biblia inasema…” nilijaribu
kumwambia. “Achana na Biblia. Mimi ni Mwislam. Tunatumia Msahafu wa Mwenyzi
Mungu. Ulioshushwa toka peponi kwa
mkono wa mtume Mohamed S.A.W.”
“Lakini hata Uislam unakataza
ushirikina.”
“Kujikinga sio ushirikina. Hayo ni
mambo ya wakoloni tu, walipoamua kututawala miili na mioyo yetu. Walitarajia
kuwa mila na tamaduni zetu kupotea huku wao wakihifadhi za kwao. Kila binadamu
ana nyota na anahitaji kuisafisha mara kwa mara. Kila binadamu ana wahenga
ambao anahitaji kuwaenzi kwa sadaka na tambiko. Asiyefanya hivyo kamwe hawezi
kufanikiwa.”
Lilikuwa somo jipya kwangu, somo
ambalo sikuwa na ujuzi nalo. Nikaamua kunyamaza. Mmanyema alichukulia ukimya
wangu kama dalili ya kumwelewa.
“Haya na wewe nieleze ukweli wa kile
kilichokufanya ufike huku. Kama nakumbuka vizuri babu yako alikupeleka Uhayani
ukasome. Nadhani ulipata shule kwani nilipoonana naye mwaka mmoja baadaye
alinidokeza kuwa ulishaingia shuleni,” alisema.
Nusura niruke kwa shauku, “Ulionana
na babu?” “Ndiyo!”
“Wapi?”
“Nyumbani kwenu. Kasulu. Tulilala
pale siku mbili na alituchinjia beberu mkubwa sana. Babu yako ni mkarimu sana.”
Bila kutegemea nilijikuta nikitokwa
na machozi. Babu yuko hai! Babu alirudi salama! Sikupata kupokea habari njema
kama hiyo kwa miaka nenda rudi.
Sikuiona haja yoyote ya kumficha
chochote Mmanyema huyu. Nilimwona kama baba yangu. Kama malaika, kwa kuweza
kunipa walao fununu tu ya habari za nyumbani. Nikamweleza kila kilichonisibu,
toka mwanzo wa mikasa yangu hadi nilipofikia.
Alinisikiliza kwa makini sana, mara
kwa mara akitikisa kichwa kwa masikitiko. Mwisho wa maelezo yangu alinishika
mkono na kuninong’oneza, “Pole sana mtani. Usijali. Hujafika mwisho wa safari
yako kimaisha. Nitakusaidia.”
Nilimwamini. Sikujua kwa nini
nilimwamini haraka kiasi hicho.
* * *
Safari ya Ikola au Karema ilikufa.
Ndoto ya kuchimba dhahabu nayo ilikufa. Safari ya Sumbawanga ikazaliwa.
Tulikaa kwa siku mbili kabla ya
kupata gari lililotufikisha
Sitalike. Hapo tulipumzika tena kwa
siku tatu tukifaidi kula nyama pori ambazo zilikuwa tele toka katika mbuga za
Katavi. Tukaondoka hadi Kisi, Chala, Nkundi na hatimaye Sumbawanga.
Wakati huo sumbawanga kilikuwa kimji
kidogo tu, chenye wakazi wachache lakini kikiwa na mambo makubwa. Mandhari ya
mji, ambayo yalipambwa na mlima Malonje wenye urefu wa mita 2418 toka usawa wa
bahari, mito na misitu tele yalifanya nitamani kuishi hapo kwa muda mrefu
zaidi.
Lakini Mmanyema ambaye baadaye
alinitajia jina lake kuwa ni Baraka Khalfan alikuwa na ratiba tofauti na yangu.
Alikuwa na majina ya vijiji mbalimbali na waganga mbalimbali ambao alipanga
kuwaona. “Huku ni Ufipa, mdogo wangu. Lyampa Iya Mfipa, umepata kulisikia?”
Sikupata.
“Lyampa Iya Mfipa kwa tafsiri ya
kawaida ni mlima mdogo tu, ambao unatambaa hadi kando ya ziwa Tanganyika na
kupita chini hadi Kongo, katika eneo la Moba, nchi ya Watabwa. Lakini kwa
wajuzi wa mambo Lyampa Iya Mfipa linabeba uzito wa pekee. Ni jiwe la tambiko
ambalo ukikaangwa juu yake hakuna mtu yeyote atakayekuchoma. Na hayo hafanyiki
mjini, isipokuwa vijijini kwa wazee, waliofundwa na babu zao,” alinieleza.
“Watu wengi wenye nafasi zao
wamepitia huku. Watu toka sehemu mbalimbali za dunia huja huku kufanyiwa mambo.
Watabwa wa Kongo nao huja huku, ingawa ni kweli pia kuwa wazee wa huku katika
kuimarisha uwezo wao huvuka ziwa kwenda Kongo,” aliongeza.
Hivyo, zilianza safari za hapa na
pale. Mara Chapota, mara Kasanga, mara Wampembe na kwingineko. Safari hizo
zilitufikisha Pwani ya ziwa
Tanganyika na kuniwezesha kuona milima ya Kongo mbele yetu na ile ya Zambia
kushoto kwetu. Ziwa hilo lilinikumbusha hamu ya kurudi nyumbani, kwani kwa
kuambaa nalo tu, nikielekea kulia ningeweza kufika Kigoma. Kwa bahati mbaya,
sikuwa tayari kwa safari hiyo.
Mmanyema alikuwa na pilikapilika
nyingi. Mara kwa mara aliniacha peke yangu na kwenda hapa na pale na aliporudi
alikuwa kachanjwa chale ama za kwenye paji la uso ama katika viwiko vya mikono
na miguu. Wakati mwingine alinituma kumtafutia vifaa mbalimbali kama mayai
viza, mizoga ya paka au njiwa weusi.
Siku moja aliondoka alfajiri na
hakurudi. Nililala peke yangu katika chumba tulichofikia cha mwenyeji wetu
mmoja. Kwa kuwa nilikuwa peke yangu nililala mapema sana, mara baada ya chakula
cha usiku. Nilipofumbua macho tena ilikuwa alfajiri. Baridi kali iliyotokana na
upepo ziwani nadhani ndiyo iliyoniamsha. Nilipotazama huko na huko sikuweza
kuyaamini macho yangu. Nililala ndani, juu ya kitanda, lakini niliamka nikiwa
nje, tena juu ya mbuyu mkubwa ulikuwa mbele ya nyumba hiyo. Isitoshe nilikuwa
mtupu, bila nguo yoyote mwilini! Nilishuka harakaharaka na kuingia ndani. Nguzo
zangu zilikuwa zimetupwa ovyoovyo chumbani humo. Nikaziokota na kuvaa
harakaharaka. Ni wakati nikivaa nilipobaini kuwa nilikuwa nimechanjwa chale
mbili katika paji langu la uso na
kupakwa vitu vyeusi kama masizi ya
mkaa.
Nilikosa raha. Niliduwaa katikati ya
chumba hicho huku nikitetemeka kwa hasira.
Mara mlango uligongwa na kufunguka
kabla sijaitikia. Mwenyeji wetu, mzee Imilio Kahigi aliingia ndani. Alikuwa
akicheka huku anatikisa kichwa. “Mtoto, mbona unasafiri
ukiwa mwepesi hivyo?” aliniuliza.
Sikumwelewa, hivyo sikumjibu.
“Uko mtupu mno. Mwepesi kupita
kiasi. Kwani hukuaga kwenu?” aliuliza tena.
“Niliaga!” nilimjibu.
Alicheka kabla ya kusema, “Hukuaga.
Na kama uliaga wazazi wako ni watoto vilevile. Jana watoto wenzako wameamua
kukupima baada ya kuona huelewekiheleweki. Wakakuta ni mwepesi mno. Ndiyo maana
wakakuacha pale juu ya mti baada ya kukuchezea usiku kucha.”
Sikujua mzee huyo alitarajia jibu
gani kwangu. Hivyo, niliendelea kukaa kimya wima, nikiwa nimemkodolea macho.
“Utafanyaje?” aliniuliza ghafla.
Nilijua nitakachofanya. “Nitaondoka,
leo hii hii,” nilimjibu.
Alicheka tena kabla hajasema,
“Unadhani utafika
unakokwenda?”
“Nitafika. Kwa nini?”
“Wenzako wamekutia alama. Popote
utakapokwenda wajuzi wa mambo watakubaini mara moja na kukugombea kama mpira wa
kona, maana una alama, alama ya shari.”
Nilizidi kuduwaa. Nadhani hata mdomo
wangu niliusahau ukiwa wazi wakati nikiwa nimemtumbulia macho. “Huyu Mmanyema
unamfahamu kwa kiwango gani?”
Aliniuliza ghafla.
“Simfahamu vizuri. Tulikutana naye
safarini miaka mingi iliyopita. Tumekutana naye tena majuzi na kufuatana naye.
Basi.”
Mzee Kahigi alitikisa kichwa kwa
namna ya kunihurumia sana. Kisha aliongeza swali jingine, “Alikuambia anatafuta
nini huku?”
“Waganga.” “Wa?”
“Kujiganga. Anataka kinga.”
Mzee akacheka tena. “Humjui vizuri,”
alisema. “Humjui hata kidogo. Huyu bwana anatafuta kizimba, dawa ya mali.
Ametakiwa kutoa kichwa cha mtu. Alitakiwa atoe mtoto wake wa kwanza, ageuzwe
ndondocha, awekwe chini ya maji kumswagia dagaa. Hana mtoto wake wa kuzaa.
Anachofanya sasa ni kukutoa wewe. Utageuzwa akili, utawekwa chini ya maji
maisha yako yote, hadi kifo cha kweli kitakapokutokea.”
Sikuyaamini masikio yangu.
“Mmanyema!”
“Naam!”
“Mimi!”
“Naam… tena mipango yake inakwenda
vizuri sana. Kesho au keshokutwa utakufa, tutakuzika. Lakini wajuzi wa mambo
tutaona tunavyozika mgomba huku wewe ukiongozwa kikondoo kupelekwa ziwani.”
Baada ya taarifa yake hiyo ‘njema’
alinikazia macho kabla hajaniuliza tena, “Utafanya nini?”
Bado sikujua alitaka nimjibu nini,
“Nitaondoka,” nilimjibu.
“Nimekwishakwambia umetiwa alama.
Hutafika mbali.” “Nitaondoka nikafie mbali. Siyo hapa.”
Baada ya kuwaza sana alisema,
“Nitakusadia. Utaondoka hapa salama ufike salama kokote uendako. Siwezi
kukubali mtu wa kuja afanye ushenzi katika milki yangu. Kaa kama kawaida, kula
kama kawaida, usiku ufunge vitu vyako vyote tayari kwa safari.”
Sikujua ilinipasa kumshukuru au la.
Kwa ujumla, sikujua kama nilipaswa kumwamini au kutomwamini. Nilichojua ni
kwamba maisha yangu yalikuwa katika mashaka makubwa. Unapopigania roho yako,
bila kumjua nani adui nani rafiki, sio suala la mzaha.
Nilifanya kama nilivyoelekezwa.
Sikumwambia mtu yeyote juu ya masaibu yaliyonipata usiku huo. Nilioga, nilikula
na baadaye kutembeatembea kijijni hapo kana kwamba hakuna lolote la ajabu
lililonipata.
Mmanyema alirudi mida ya saa nne
hivi. Alionekana mtu mwenye furaha na matumaini makubwa. Huku akitabasamu
alinivuta chemba na kuninong’oneza, “Mdogo wangu mambo yamekwisha. Kama
nilivyokuambia baada ya miaka miwili tutakuwa watu katika watu. Pesa halitakuwa
tatizo tena. Wewe, kwa kuwa umesoma kuliko mimi utakuwa mhasibu. Utatunza
hesabu ya fedha na mali zetu zote.” Aliongeza kwa kunidokeza kuwa jioni hiyo
angesafiri tena. Atakaporudi tutakuwa tayari kurudi Kigoma.
“Unakwenda wapi safari hii?”
Nilimuuliza.
“Nakwenda Kipili hadi Mtakuja.
Nitajitahidi kurudi keshokutwa. Nikirudi tu yamekwisha,” alinijibu. Kisha
alinitazama usoni na kuniuliza “Hapo umefanya nini?”
“Nilijikuna,” nikamjibu.
Nilihisi hakuniamini. Alizikagua
chale zile kwa muda mrefu kidogo.
“Sidhani,” alisema. “Nikirudi
tutaangalia suala lako vilevile. Isije kuwa washenzi wanakuchezea, maana umekaa
mweupemweupe kama kinda la ndege.”
Nilitamani sana kumwamini.
Sikubahatika kuipata fursa hiyo.
Mara tu alipoondoka nilifunga vifaa
vyangu katika begi langu. Baada ya mlo wa usiku nilijilaza mapema nikisubiri
usingizi unichukue ili kesho ifike nione mzee Kahigi atanisaida vipi ili niweze
kuondoka nchi hiyo ya Wafipa salama.
Sikujua usingizi ulitokea wapi.
Nilihisi ghafla kama naota, mlango ukifunguka na mzee Imilio Kahigi akiingia
chumbani humo. Alikuwa mtupu, isipokuwa kwa kipande kidogo cha kaniki
alichofunga mbele ya kiuno chake. “Inuka,” aliniamuru. Niliinuka. “Chukua begi
lako unifuate,” nilifanya kila alichoniamuru na kumfuata hadi nje ya nyumba.
Hapo kulikuwa na ungo mkubwa wenye
vikorokoro mbalimbali ambavyo sikuweza kuvifahamu. “Ingia ukae hapo,”
aliniamuru tena. Nikamtii.
Mara alianza kuimba kwa lugha ya
Kifipa, maneno ambayo sikuweza kuyaelewa. Akaninyunyizia kitu fulani chenye
harufu mbaya kwa usinga wake huku akiendelea kuimba. Ghafla nikaona ungo
ukianza kupaa. Ulipaa, ukapaa, ukapaa hadi mawinguni. Naota? Nilijiuliza. Kama
ilikuwa ndoto, basi ilikuwa ndoto ya aina yake ambayo ningependa nirudie kuiota
mara kwa mara.
SEHEMU YA NANE
Kwa Hadi Mbeya
ilizinduka toka usingizini. Nadhani
kilichonizindua ni baridi kali iliyoambatana na upepo wa kipupwe ambao
ulinipiga mwili na
kunifanya nijikute nikitetemeka,
meno yangu yakigongana. Nilikuwa katika kituo cha mabasi, peke yangu. Jogoo
waliokuwa wakiwika huko na huko waliniashiria kuwa ilikuwa alfajiri.
“Niko wapi?” nilijiluliza nikiinuka
na kutazama huko na huko. Begi langu lilikuwa miguuni mwangu, kama
nilivyolifunga jana. Kwa mbali nilianza kuona mtu mmojammoja wakipita hapa na
pale, baadhi yao wakija kituoni kuwahi usafiri. Baadhi ya magari yalianza
kuwashwa.
Niliinama na kuliinua begi langu,
ambalo nililiinua kwa taabu sana. Vidole vyangu vilikuwa vimekufa ganzi. Hata
pale nilipojaribu kutembea miguu yangu ilikuwa kama haipo kwa ajili ya baridi
hiyo kali. Nikajikongoja hadi nilipomfikia taniboi mmoja ambaye alikuwa
akimimina maji katika injini ya gari lake, tayari kwa safari.
“Samahani, hapa ni wapi?”
Nilimuuliza.
“Huwa tunasalimiana kwanza,” alisema
akinitazama kwa mshangao.
Sikumjibu. Si kwa ajili ya ujeuri
bali kwa kuwa sikujua
alitaka salamu za aina na lugha
gani, kwani lafudhi yake ilikuwa tofauti kabisa na ile ya watu wa Sumbawanga.
Alipoona kimya aliniuliza kwa mshangao, “Kwani wewe umetoka wapi hata uulize
hapa ni wapi?”
“Nimetokea Sumbawanga.” “Umekuja na
gari gani?”
Sikuwa na jibu, jambo ambalo
lilimshangaza zaidi. “Ulilewa?”
“Hapana.”
“Ulikuwa unaumwa?” “Hapana.”
“Sasa umewezaje kutoka Sumbawanga
hadi hapa Mbeya bila kujua unapokwenda?”
Sikuendelea kumsikiliza. Mbeya!
Niliwaza kwa mshangao. Niliyakumbuka maongezi yangu na Mzee Imilio Kahigi na
ahadi yake ya kunisaidia. Nikakumbuka tukio la usiku, aliponijia katika mavazi
ya ajabuajabu na kuniamuru kuketi katika ungo, nikiwa nimepakata begi langu.
Nilikumbuka kwa mbali nyimbo zake alizoimba akichezesha usinga wake hata
nikaanza kupaa! Mbeya! Nimekuja Mbeya kwa ungo! Sikuamini.
Lakini sikuwa na sababu ya
kutoamini. Baridi kali ambayo ilianza kunila mifupa ilikuwa ushahidi tosha kuwa
niko katika eneo jingine, lililo juu zaidi ya usawa wa bahari zaidi ya
Sumbawanga. Hata mavazi ya watu wengi waliokuwa wakiongezeka mitaani
yaliashiria hali ya hewa nyingine kabisa. Makoti au majaketi makubwa, kofia au
vitambaa kichwani na viatu vizito miguuni. Majina mengi yaliyokuwa
yakitajwatajwa pia yalikuwa mapya masikioni mwangu; Mwakipesile, Mwangonda,
Mwamasika, Mwanjelwa na kadhalika.
Nilipapasa mifuko yangu. Pesa
nilizopewa na Chifu Masanja bado zilikuwemo. Nikajikongoja hadi nilipopata
mgahawa mdogo na kujinunulia chai ya moto sana. Nilikunywa vikombe viwili chapchap
na cha tatu taratibu kabla ya kubaini kuwa chai hiyo ilinichubua midomo na
ulimi kwa kiwango kikubwa sana.
Toka hotelini hapo nilitafuta nyumba
ya wageni ya bei nafuu ambamo nilionyeshwa mapipa ya maji ya moto na kuchota
ndoo moja niliyoitumia kuoga. Baada ya hapo nilipanda kitandani na kujilaza,
nikiwa nimejifunika mablanketi mazito mawili. Usingizi mzito ulinichukua na kwa
muda ukawa umenisahaulisha masaibu yote yaliyonitukia katika muda mfupi wa
maisha yangu. Hata hivyo ulikuwa usingizi wa mang’amung’amu kwani niliandamwa
na ndoto za kutisha, mara nikiwa juu ya mbuyu, mara nikipaa angani, mara nikiwa
nimezingirwa na wachawi wanaopanga kunila nyama na kadhalika.
Nililala mchana kutwa na usiku
kucha. Nilipoamka kesho yake jambo la kwanza nililofanya ilikuwa kwenda
madukani ambako nilinunua mavazi yanayoendana na hali ya hewa ya Mbeya; koti,
sweta zito, kofia na soksi nzito.
Katika pitapita yangu mjini hapo
niliingia duka la vitabu ambamo nilinunua ramani ya mji na vitongoji vya Mbeya.
Nikaketi mahala na kuisoma. Jambo la kwanza lililovuta macho yangu ni urefu wa
safari ambayo nilisafiri kwa miujiza toka Sumbawanga hadi Mbeya. Kama
ningelazimika kusafiri kwa gari ningetumia zaidi ya siku mbili njiani kwa
kupita katika miji na vijiji mbalimbali kama Mpui, Ndalambo, Tunduma, Ihanda,
Iwanda na hatimaye Mbalizi.
Jambo jingine lililovuta macho yangu
ni kubaini kuwa
mkoa wa Mbeya ulikuwa mpakani mwa
Tanganyika na Zambia kwa upande mmoja, nchi ya Malawi kwa upande wa pili. Mji
mkubwa zaidi wa mpakani kwa upande wa Zambia ukiwa Tunduma na kwa upande wa
Malawi mji mkubwa zaidi ukiwa Kyela na Itundi. Mbeya ilikuwa na sifa nyingine.
Ilibahatika kuwa na ziwa kama yale ya Nyanza na Tanganyika, ingawa kwa asilimia
ndogo. Bahati hiyo iliwezesha si kuvua samaki tu, bali pamoja na kuwawezesha
kuwa na bandari, Itungi, ambayo ilihudumia miji ya Karonga kwa upande wa Zambia
na mikao kama Iringa kupitia wilaya ya Ludewa.
Ramani hiyo ilinionyesha kuwa Mbeya
haukuwa mji mdogo kama ulivyokuwa ukionekana. Ulikuwa na mengi ya kusisimua
kiutamaduni, kiuchumi na kimazingira. Pamoja na ukweli kuwa kabila
lililojulikana zaidi la mkoa huo lilikuwa la Wanyakyusa bado kuna makabila
mengine tele kama Wandali, Wasafa na Wasangu ambao ni wenyeji asilia. Aidha,
kuwepo kwa mkoa huo mpakani kulichangia kufanya uhamiaji wa kutokea nchi za
Malawi na Zambia kuwa sehemu ya wakazi.
Sikuhitaji ramani hiyo kusoma ukweli
kuwa wakazi wengi walikuwa wakulima. Mazao kama mahindi, mpunga, migomba, viazi
na mimea mengine ilikubaliana sana na ardhi na hali hewa ya huko, jambo
lililofanya katika pitapita zangu nipishane na wakulima waliobeba mazao ama
kwenye baiskeli ama katika mikokoteni wakielekea sokoni.
Lakini Mbeya ilikuwa na kitu kingine
cha ziada. Dahabu. Purukushani za kutafuta dhahabu, kwa mujibu wa maelezo toka
kwa baadhi ya watu niliobahatika kuzungumza nao, zilianza tangu mwaka 1905
kufuatia fununu za kuwepo kwa madini hayo. Hata hivyo, miaka kumi na mitano
baadaye ndipo ilipodhihirika rasmi kuwepo kwa madini hayo katika
mji wa Chunya. Hali hiyo
iliyopelekea mji huo mdogo upanuke ghafla na kupokea watu wa aina mbalimbali,
wa makabila na mataifa mbalimbali, kila mmoja akijaribu kuutumia mwujiza wa
dhahabu kujipatia chochote. Walikuwemo wachimbaji, madalali, wanunuzi, wauzaji
wa vifaa vya uchimbaji na vyakula na wengineo.
“Nafikiria kwenda huko kesho,”
nilimwambia mmoja kati ya watu niliobahatika kuzungumza nao juu ya suala hilo.
Alikuwa mtu wa makamo, ambaye muda mwingi nilimwona kakaa mbele ya hoteli
niliyofikia. Sikupata kujua kazi yake ilikuwa ipi.
Mtu huyo alinitazama kwa mshangao,
“Nani, wewe?” aliniuliza.
“Ndiyo,” nilimjibu. “Unakwenda
kufanya nini?” “Kuchimba.”
Akacheka na kunitazama kwa dharau ya
dhahiri. “Inahitaji mtu kichaa sana kwenda kuchimba madini,” alisema.
Ikawa zamu yangu kumshangaa. “Kwa
vipi?” nilihoji. “Kwanza hutarudi salama. Na ukirudi utakuwa masikini
kuliko hapo ulipo.” Alinionya.
Sikumwelewa. “Mbona kuna watu huko
na wanachimba?”
“Mdogo wangu, hao walioko huko huwa
hawarudi. Kazi ile ni kama laana hivi. Unaweza kuchimba maisha yako yote bila
kupata chochote cha maana. Unaweza kubahatika kupata mali ya maelfu lakini siku
mbili tatu ukawa huna hata shilingi moja. Fedha za madini ni kama za mashetani.
Hupotea kimiujiza kama zinavyopatikana.”
“Na hawa wanaotajirika?” nilihoji.
“Hao sio wachimbaji. Ni wanunuzi au
wamiliki wa maeneo utakayochimbia. Wachimbaji wa kawaida wako huko, wanazeekea
huko na kufa huko!” alisisitiza.
Laiti angejua taarifa yake ilinikata
maini. Toka nilipofika mjini hapo kimiujiza nilikwishafanya uamuzi. Uamuzi
wangu ulikuwa kwenda Chunya, kujiunga na wachimbaji madini ili nikibahatika
nirudi kwetu sina elimu lakini nina mali. Taarifa za kwenda kuzeekea huko na
kufia huko ziliniacha hoi, taabani. Mshauri wangu aliweza kusoma msuguano wa
mawazo yangu, nilidhani, kana kwamba anapigilia msumari wa mwisho kichwani
mwangu, aliongeza, “Kama umetoka kwenu kwa nia ya kwenda machimboni isahau
kabisa ndoto hiyo. Utakufa siku si zako. Utaugua kifua kikuu kwa vumbi la
machimboni, utazikwa hai kwa kubomokewa na kuta za shimo, utauawa na wachimbaji
wenzako ukibahatika kupata mali nyingi. Kuna
hatari elfu moja na moja.”
Ushauri wake wa bure ulianza
kunichosha. “Kuna kazi gani duniani ambayo haina hatari kwa namna moja au
nyingine?”
“Nyingi tu,” alijibu harakaharaka.
“Kama?”
“Udaktari kwa mfano,” alijibu
harakaharaka.
Nikacheka. “Daktari lazima asome kwa
miaka nenda rudi. Huwezi kuamua tu kwamba unataka kuwa Daktari.”
“Tunazungumzia kazi, sio kisomo.”
Nikabaini kuwa nazungumza na mtu
mweye asili ya ubishi. Nikaamua kumuuliza yeye binafsi anafanya kazi gani.
“Wengine kazi zetu huwa hazitajwi
hovyo.” Alisema.
Nikaanza kuamini hisia zangu kuwa
hana kazi. Hiyo
ilikuwa siku yangu ya tatu toka
nilipofika Mbeya na kila
siku namwona ameketi anazungumza na
watu mbalimbali. Nikaamua kupuuza hata mawaidha yake juu ya hatari za uchimbaji
madini. Watu hujiunga na jeshi, wakijua fika kuwa kazi yao ni kwenda vitani
ambako kifo ni jambo la kutarajiwa. Watu hujifunza urubani, wakiwa wanajua
vizuri sana kwamba ndege ikidondoka kupona ni nadra sana.
Nadhani sihitaji ushauri wako zaidi,
nilitamani kuwambia hivyo. Hata hivyo, sikuthubutu. Nilimwona kama mtu ambaye
asingekuwa mwepesi wa kusahau na kwa kila hali sikuhitaji maadui bila sababu za
msingi.
* * *
Nilikaa Mbeya kwa wiki nzima zaidi.
Bado nilikuwa na hamu kubwa ya kwenda Kiwira kujaribu bahati yangu machimboni.
Tatizo lilikuwa usafiri. Hakukuwa na magari ya abiria ya mara kwa mara
isipokuwa yale ya kuvizia tu. Na hayo ilikuwa lazima kuwe na mtu atakayekudokeza
gari fulani, linakwenda siku fulani. Sikuwa nimebahatika kumpata mtu wa aina
hiyo.
Hivyo, niliutumia muda wangu mwingi
kutembea huku na huko katika mji na vitongoji vya Mbeya. Nilifurahia sana
vijilima vingi vilivyotapakaa huku na huko na kufanya safari zangu ziwe za
kupanda na kushuka toka kitongoji hadi kitongoji. Salamu za Kinyakyusa
‘Ugonile,’ ziliniandama kila nilipokwenda. Nami sikujivunga, nilijibu kwa
kujiamini, ‘Ndaga,’ ingawa ilipofuata midahalo mirefu ya kilugha niliufyata
ulimi wangu na hivyo kufanya nijulikane kuwa mimi ni ‘Wakuja.’
Kama fedha zingeniruhusu ningeweza
kusafiri hadi
maeneo mbalimbali maarufu kama
Tukuyu, Mbarali, Ileje,
Kyela na Rungwe ambako nilisikia
kuna mlima mrefu kwa mita 2961 juu ya usawa wa bahari.
Mto Kiwira pia ni kitu kingine
kilichonivutia sana huko Mbeya. Ukiwa unapokea maji yake toka vijito vya
Matogola, Sinini, Kipoke, Kilosi na Mulagala mto huo ulisafiri hadi Ziwa Nyanza
ambamo ulimwaga maji yake siku hadi siku. Kama ilivyo kawaida ya bahari na
maziwa, kamwe ziwa Nyasa halikupata kushiba wala kutapika kwa wingi wa maji
hayo. Pengine ni kweli kuwa hiyo ndiyo kanuni ya maisha? Samaki mkubwa hummeza
mdogo!
Ziwa hilo la Nyasa halikuwa pekee
kwa Mbeya. Walibahatika kurithi sehemu nyingine ya ziwa jingine ambalo
lilijikita katikati ya Mbeya na Rukwa. Hilo ni ziwa Rukwa. Wakati Rukwa
walilifaidi kwa sehemu kubwa ya kusini, Mbeya walilitumia kikamilifu upande wa
Kaskazini. Wakazi wa miji kama Manda na Ngomba walilitumia kwa masuala mbalimbali,
ikiwa pamoja na uvuvi wa samaki.
Kitu kingine kilichonisumbua hapo
Mbeya ni lile shamba la aina yake la maua na miti asilia. Shamba au pori hilo
lililoko Kitulo lilikuwa kama moja ya mashamba ya wafalme wa kale, hata kabla
ya kalenda ya sasa kuanza, jambo lililofanya liwe hazina ya pekee duniani. Kwa
kweli shamba hilo lilinifanya nimkumbuke babu yangu. Alivyokuwa mpenzi wa miti
na mitishamba kama angebahatika kufika shambani humo angekuwa mtu wa kushinda
maporini akinukuu na kukariri hiki na kile.
Mfuko wangu ulianza kukaa vibaya.
Akiba yangu ya pesa nilizopewa na Chifu ilianza kuyoyoma, hali iliyofanya
nianze kufikiria umuhimu wa kupata ajira mapema zaidi. Nikiwa kijana, mwenye
nguvu na afya tele sikuwa na wasiwasi kwa kazi yoyote ambayo ingenitokea mbele
yangu. Hivyo, alipotokea
mzee Ayubu Mwalongo na kuniuliza
kama ningependa kuwa mmoja wa wafanyakazi wake wa lori la abiria na mizigo kama
kondakta sikusita kukubali.
Nilikutana na mzee huyo kwa namna ya
ajabu kidogo. Kwa mara ya kwanza tulikuwa hotelini. Nilikuwa nikinywa uji wa
ulezi. Nilipata hisia kuwa kuna mtu ananitazama sana. Nikainua uso na kukutana
na mzee mmoja mwembamba na mfupi sana. Kwa kweli, ni mvi na ndevu zake ndizo
zilizonifanya nijue kuwa ni mzee. Vinginevyo umbo lake lilikuwa la mtoto mdogo.
Hata mavazi yake nadhani alitoa vipimo vya mtoto. Tulipokutanisha macho
alinitazama kwa muda kama mtu aliyepata kuniona mahala lakini hakumbuki ni
wapi. Mimi binafsi, nikiwa na hakika kuwa sijapata kumwona mahala popote
nilimpuuza na kuendelea kuufaidi uji wangu.
Kesho yake, nikipitapita zangu
katika kituo cha magari kwa matarajio ya kusikia taarifa za gari liendalo
Kiwira nilimwona tena. Na alikuwa akinitazama kwa jicho lilelile la aina
fulani. Wakati nikiamua kuondoka alinifuata. “Samahani kijana,” aliniambia
aliponifikia. “Hivi tulionana wapi?”
“Nina hakika hatujapata kuonana.
Mimi ni mgeni huku
na nimefika majuzi tu,” nilimweleza.
Hakuoneka kuamini, “Unaitwa Nani?”
aliuliza tena. “Kwa nini unahitaji jina langu?”
“Bado ninahisi nilipata kukuona
mahala,” alijibu na kuongeza. “Ulipata kuishi Iringa?”
“Mimi! Hapana.” “Tanga?”
“Hapana.” “Morogoro?” “Hapana.”
Akazidi kushangaa, “Unaitwa nani?”
aliuliza tena.
“Jina la nini?” nami nikahoji.
“Siulizi kwa nia mbaya. Ninapata
hisia kuwa nakufahamu. Kama sikufahamu wewe nitakuwa namfahamu baba yako. Kwani
unakotoka hasa ni wapi?”
“Kigoma,” nilimjibu.
Akaonekana kuchanganyikiwa zaidi.
Nadhani hakupata
kufika huko.
“Unafanya kazi gani?”
“Sina kazi. Natafuta kazi.”
Nikamwona akitafakari kabla ya kuuliza, “Unajua kusoma na kuandika?”
“Mie! Vizuri sana.” “Unajua
mahesabu?”
“Najua. Kwa kiwango cha kutosha tu,”
Nilimjibu
Ndipo aliponieleza kuwa yeye ni
mfanyabiashara wa magari. Kwa jina alijitambulisha kuwa anaitwa Ayubu Mwalongo.
Alikuwa nayo magari manne ya mizigo
yanayokwenda huku na huko. Moja likiwa jipya ambalo halijaanza safari. “Tayari
nimepata dereva. Bado nilikuwa na shida ya kondakta. Kama wewe umesoma na
unataka kazi umepata. Unasemaje?”
Nikatae? Tuliafikiana na kupangiana
mshahara na
majukumu. Nilitakiwa kuripoti kazini
kesho yake.
Mtu mmoja aliniona wakati
nikizungumza na yule mzee pale stendi. Mara tu tulipoachana aliniita kwa jina.
Sikujua alijuaje jina langu. Ni yule aliyejitokeza kuwa mshauri wangu wa
masuala ya madini wa pale nyumba ya wageni niliyofikia.
“Unamfahamu yule mzee uliyekuwa
unazungumza naye?” alinihoji.
“Nani? Mzee Ayubu? Namfahamu.”
“Unamfahamu vizuri?”
“Kwa nini? Nimemfahamu leo tu. Najua
ni
mfanyabiashara mkubwa wa magari na
anayo mengi. Kesho naanza kazi katika moja ya magari yake,” nilimwambia.
“Nini?” alishtuka. “Unaanza lini?”
“Kesho”
“Kwenye magari…!”
“Yake,” nilimjibu. “Kwani kuna
tatizo gani?”
Alinitazama huku akitikisa kichwa
kwa namna ya kunihurumia. Mdogo wangu hujipendi. Naona mji umeingia kwa pupa.
Acha tabia ya papara. Kaa na watu uliza, kabla hujakurupuka. Oh! Shauri yako!”
Hasira zikanipanda. “Kwani lini
nilipata kukuteua wewe kuwa mshauri wangu? Shika hamsini zako, acha nishike
zangu. Nitakapohitaji ushauri labda nitakuomba, siyo leo.” Nilisema nikiondoka
zangu na kumwacha akiwa kanikodolea macho.
Kwa namna fulani nilihisi kuwa
nimefanya makosa. Pengine isingenigharimu chochote kumsikiliza mshauri huyo wa
bure, kumsikia tu, sio kumsikiliza, kwani nilikwishamchukulia kama mtu mwenye
muda mwingi wa kuzungumza na tabia ya kujifanya anajua kuwa ningeishia kuwa
kama yeye, kuketi toka asubuhi hadi adhuhuri akizungumza kwa hofu ya kufanya
hili na lile.
Vilevile, sikutaka mtu yeyote
anishawishi kuacha fursa ya kazi hiyo ya kusafiri. Tangu nilipoanza safari toka
Buha hadi Uhayani na kisha Usukumani hadi Ufipa na sasa huku kwa Wanyakyusa
nilijikuta nimeanza kupatwa na maradhi ya kupenda safari. Nilifurahia sana
kuona sura mpya za nchi za watu, mazingira mapya na tamaduni mpya. Sikutaka mtu
yeyote anishawishi vinginevyo kwa hilo.
9SURA YA 9
Nchi Ya Mkwawa, Ya Wajerumani.
ati ya wageni walioingia katika nchi
yeti kwa mikiki, jeuri na ukatili mkubwa ni pamoja na Wajerumani. Baada ya
kusikia sifa za uzuri
na utajiri wa Tanganyika, toka kwa
Waarabu na Wareno ambao walifika kwanza katika pwani ya nchi yetu wajerumani
walishikwa na tamaa isiyo kifani.
Tamaa hiyo ilichochewa zaidi na
bwana mmoja aliyeitwa John Rebman tarehe 11, mwezi wa tisa mwaka 1848 alipoondokewa
kuwa mtu mweupe wa kwanza kuutia machoni mlima mrefu kuliko yote afrika,
Kilimanjaro. Mlima huu, huko Kaskazini mwa nchi yetu, unakwenda angani kwa mita
zipatazo 5895, ukiwa umepambwa kwa theluji nyingi inayong’ara kwa kumeremata
kwa namna ya kufanya uwe kama shada la ufalme wa Afrika na dunia pia. Hali
nzuri ya hewa iliyootesha vizuri aina mbalimbali za mimea na utulivu wa wakazi
wake vilimtia Rebman wazimu. Aliporudi kwao nchi yake ikapata wazimu, wazimu wa
mapenzi kwa Tanganyika.
Hivyo, mwaka 1884, Novemba 23,
Mjerumani aliposimika bendera yake kule Bagamoyo na mwaka mmoja baadaye,
February 27 kujitangaza wamiliki wa Tanganyika haikuwa muujiza kwa mtu yeyote.
Uvamizi huo wa Wajerumani
kwa kiasi kikubwa ulifanikiwa kwa
ajili ya hila zilizofanywa na mtu wao mmoja, aliyeitwa Karl Peters, ambaye
alipita huko na huko akiwaingiza Machifu na watu wengine katika mikataba ya
ujanja ujanja kuhalalisha utawala wao. Kwa upande mwingine, vitisho
vilivyoambatana na mauaji, kwa kutumia silaha zao ambazo zilikuwa bora zaidi ya
zetu kulifanikiwa azma yao ya kuimeza nchi yetu.
Mnamo mwaka 1991, Mjerumani mmoja,
kwa jina Julius Von Sodden aliteuliwa kuwa gavana wa kwanza wa Ujerumani kwa
Tanganyika. Ni yeye aliyeamua kuhamisha makao makuu ya serikali yao toka
Bagamoyo hadi Dar es Salaam.
Kam Sodden na magava wenzake
waliomfuatia, akina Von Echele, Von Wissman, Von Libert na wenzao wengine; Von
Gotzen, Von Rechenberg na yule wa mwisho Von Schnee walidhani kuwa walikuwa
wameipita Tanganyika kwa urahisi kiasi kile basi walikuwa wamejidanganya.
Huko Tabora aliibuka shujaa mmoja, Isike
Mkasiwa, ambaye alipigana nao kwa muda mrefu hadi Januari 9, 1893 alipozidiwa
na kuamua kujiua badala ya kuchukuliwa mateka. Huyo hakuwa mhanga pekee. Huko
Kilimanjaro mnamo
Machi 2, 1900 Machifu tisa wa koo
mbalimbali za makabila ya huko walinyongwa hadharani kufuatia upinzani wao
mkali dhidi ya Wajerumani. Miongoni mwa Machifu mashuhuri kati ya walionyongwa
alikuwemo Mollelia wa Kibosho, Ngalami pamoja na Meli wa Moshi. Madai ya
watawala wa Kijerumani ni kuwa walikuwa wakichochea upinzani dhidi ya utawala
wao.
Haikuwasaidia, kwani ndio kwanza
Watanganyika walizidisha mapambano. Vita ya majimaji vilienea sehemu mbalimbali
za kusini ikiwa pamoja na Songea, Mtawara, Lindi na kwingineko. Majimajii
walishambulia misheni ya
Mikukuyumbu Nachingwea, wakateka
makao ya Wajerumani ya Liwale, misheni ya Masasi na kuteketeza ile ya Nyangao,
Lindi. Hali hiyo ilipelekea Septemba 1, 1905 Wajerumani waombe msaada zaidi wa
kijeshi toka kwao, ambao uliwezesha kurejesha utawala wao.
Uamuzi waliouchukua baada ya kuona
hata baada ya kumteka Kinjekitile Ngware mganga aliyekuwa akiwapa kinga
wapiganaji ili wasidhurike na risasi za Mjerumani na kumnyonga hadharani katika
kijiji cha Muhoro, Rufiji bado mapambano yalizidi kuwa makali.
Chifu mwingine, akitokea Iringa, kwa
jina Singoyangili Mkwawa hatasahulika kwa kupambana na Wajerumani kwa nguvu
zake zote. Chifu huyu alitokea katika kabila la Wahehe, makazi yake yakiwa
kijijini Kalenga, aliwachachafya Wajerumani kwa kiwango ambacho hawatakaa
wasahau.
Mara kadhaa majeshi ya Mkwawa
yaliwateketeza Wajerumani na kuvunjilia mbali ngome zao. Hali hiyo
iliwasababishia Wajerumani waamue kujenga ngome imara ambayo ilikuja kuwa
chanzo cha mji na baadaye mkoa wa iringa. Mji huo ulijengwa karibu na ngome ya
Mkwawa ya Kalenga. Ndiyo, Mkwawa pia alishindwa na kuamua kujinyonga badala ya
kukamatwa akiwa hai, lakini mji wa Iringa ukawa kielelezo tosha cha nguvu na
misimamo thabiti wa babu zetu dhidi ya utawala wa kigeni.
Niliyafikiria yote hayo nikiwa ndani
ya gari karibuni kuingia katika mji huo wa kihistoria. Ilikuwa safari yangu ya
kwanza kama kondakta. Nilikuwa na muda mwingi wa kufikiri na kutafakari yale
ambayo nilibahatika kuyasoma shuleni na katika vitabu mbalimbali vilivyopata
kunipitia mbele yangu. Mambo hayo yalikuja kama ndoto kutokana na macho yangu
yaliyokuwa yakitazama nje ya gari
muda mwingi zaidi.
Tulisafiri kwa zaidi ya siku tatu,
toka Mbeya hadi kuufikia mji wa Iringa. Tulishusha hapa na kupakia pale, mara
abiria ama mizigo, mara mizigo na abiria. Mara kadhaa tulilala porini kwa ubovu
wa magari, mara nyingine ilikuwa kusubiri mzigo ya michele au matunda
yaliyokuwa yakivunwa.
Kinyume na nilivyoahidiwa kuwa
ningetumia gari jipya, gari hili lilikuwa chakavu lililochakaa sana. Kama
lingekuwa binadamu lingeweza kusema hivyo na kuacha lipumzike kwa amani, lakini
kwa kuwa halikuwa na uwezo huo liliacha liburuzwe kama ng’ombe mzee huku mlio
wake ukionyesha kuteseka sana kwa mashine yake hata kwa mtu asiye na ujuzi wa
ufundi wa magari. Lilikuwa lori, aina ya Bedford. Kila baada ya kilomita kumi
tulilazimika kusimama na kujaza maji katika rejeta ambayo ilikuwa ikiyakausha
kwa kasi ya pekee.
Alichoniambia tajiri yangu juu ya
kutumia gari hilo badala ya lile jipya nililoahidiwa sikupata kukielewa vizuri.
Alitumia maneno kama ‘Ngoja uzowee’ au ‘Vibali vimechelewa.’ Kauli ambazo
sikuona kama alitaka nizielewe vizuri. Kwa kuwa wahanga wanasema ‘mchagua jembe
si mkulima,’ nikapokea jukumu hilo bila maswali zaidi.
Lakini dereva wangu alinishangaa
zaidi pale nilipomuuliza juu ya gari hilo. Alionekana kuwa mtu mwema,
mchangamfu na mkimya. Nilimkadiria kuwa alinizidi umri kwa zaidi ya mara mbili.
Kwa jina alijitambulisha kuwa ni Kalinga. “Gari jipya?” alinihoji akicheka
sana. “Alikuambia analo
jipya? Basi litakuwa hili,”
aliongeza.
“Kwa vipi? Kwani hana gari jipya?”
nilihoji.
“Huu kwangu mie ni mwaka wa tatu toka
niandikishwe kazi kwake. Na nilijiunga kwa hadithi hiyohiyo ya gari jipya.
Sikupata kuliona hata kwa macho.”
Nilipatwa na mshangao wa mwaka.
“Kwanini basi anasema uongo?” nilimuuliza.
“Hata mimi najiuliza hilo mara kwa
mara,” Kalinga alinijibu. “Mtu mzima kwa nini useme uongo? Unajua madereva
wawili kabla yangu na makondakta watatu wameshaacha kazi kwa jili ya ahadi hizo
za gari jipya?”
Ghafla nikajiwa na wazo. “Kwa hiyo
mimi nimeingia
baada ya kondakta wa mwisho kuacha
kazi?” nilihoji. “Kawambwa! Yeye hakuacha,” alisema.
“Ila?” “Alikufa.”
“Alikufaje? Ajali?” nilizidi
kudadisi.
“Wala haikuwa ajali. Kifo chake kina
utata mwingi. Nadhani tuachane na maongezi hayo. Hayakufai kwa sasa,”
alishauri.
Nikamuuliza Kalinga juu ya magari
mengine saba aliyonayo tajiri yetu. Hilo lilimfanya aangue kicheko.
“Mbona unacheka. Hana?”
Kalinga alikohoa kwa namna ya mtu
aliyepaliwa kabla ya kusema taratibu, “Anayo.”
Nilimwona kama mtu aliyeacha neno
alilotaka kulisema. “Anayo, lakini?” nilimshurutisha.
“Lakini ni mabovu kuliko hili. Yote
yako katika magereji mbalimbali, taabani hata mafundi wameyakatia tamaa.
Wanamwambia akayavute, mwenyewe anasema yatatoka yakitembea.”
Ilibidi nami niangue kicheko.
Kilikuwa kicheko cha uchungu. Sikujua kama nilikuwa nikijicheka mie au kumcheka
mwajiri wangu mpya, tajiri wa magari mabovu. Kwa namna
fulani nilihisi fahari. Niliona kama
mimi na dereva Kalinga ndio tuliokuwa matajiri wenye ufunguo pekee za kumkwamua
tajiri yetu ili anunue gari jipya na kufufua yale mengine yaliyoozea kwa
mafundi. Fikra hizo zilinifanya nitupile mbali wazo ambalo lilianza kunijia la
kuacha kazi hiyo mara moja na kutafuta nyingine.
Nikakumbuka yule mshauri wangu wa
masuala ya madini na kubaini kuwa kweli alikuwa na jambo la kunishauri juu ya
tajiri yangu, mzee Ayubu Mwalongo. Kwa mara ya kwanza nilijilaumu kwa
kutomsikiliza.
* * *
Hali ya hewa ikiwa, kwa kiasi
fulani, kama ile ya Mbeya, mji ukiwa juu ya vilima kwa takribani mita 1550 juu
ya usawa wa bahari nilijikuta nikiridhika sana na maisha yangu ya hapa na pale
katika mji, vitongoji na vijiji vya Iringa.
Tulikuwa watu wa safari kila siku.
Tulikwenda Mafinga, ambako baridi ilizidi ile ya mjini kwa kiwango kikubwa.
Tulikwenda Kilolo ambako niliweza kuupanda mlima Luhembelo na kuvutiwa na
wanyama wa ainaaina katika pori moja lililoitwa Udzungwa. Wanyama ambao walikuwa
tele kama wale tuliowaona pia kule Ruaha. Tulifika Makete, tulifika Njombe,
tulifika pia Ludewa.
Kila nilipopata wasaa nilitembelea
kijiji cha Kalenga ili kuona kumbukumbu za yule mzee shujaa, Mkwawa na ngome
yake. Kaburi lake lilikuwa pale, nasikia alizikwa bila kichwa, kwani Wajerumani
walikipokonya na kukipeleka kwao ili kuchunguza uwezo wa ajabu wa mtu huyu
aliyewatoa jasho vigogo waliokaribia kuitawala dunia.
Nilipata pia kutembelea kijiji cha
kumbukumbu cha
Isimila. Niliweza kuona michoro na
vifaa vilivyochongwa kutokana na mawe ambavyo ni sehemu ya uthibitisho kuwa mtu
wa kale, zaidi ya miaka 70,000 aliishi Tanganyika. uthibitisho huo umefanywa na
wataalamu mbalimbali waliobobea katika taaluma za macho ya kale.
Uzoefu wangu mkoani humo ulinifanya
nibaini kuwa hata jina la Iringa lilitokana na udhaifu wa matamshi ya wageni
hao kwa lugha ya Kihehe, kwamba wenyewe walikuwa wakiuhita mji huo Lilinga, kwa
maana ya ng ngome.
Biashara yetu ilikuwa ikienda
vizuri, kama kila mmoja wetu alivyotegemea. Kwanza gari lilipunguza tabia ya
kuharibikaharibika mara kwa mara. Jambo lililomfanya dereva Kalinga ambaye pia
ni fundi anichekelee na kunisifu kuwa nina ‘nyota’ ya biashara, “Sio siri, gari
hili lilianza kushindikana. Mimi mwenyewe nilishaamua kuifanya safari hii iwe
ya mwisho,” alinitobolea siri yake.
Aliyefurahi zaidi , alikuwa tajiri
yetu mzee Ayubu. Kila tuliporejea Mbeya tulikuwa na fedha nyingi za kumpa na
taarifa chache tu za kuharibika kwa gari lake. Kwa mara ya kwanza nilimwona akitabasamu.
Miezi miwili mitatu baadaye nilipomtazama nilihisi amenenepa na kurefuka
kidogo.
Kwa bahati mbaya, mafanikio hayo
yalianza kuambatana na ajali za mara kwa mara. Ajali hizo zilikuwa ngumu
kuelezeka. Ya kwanza, ilitokea katika maeneo ya Ruaha. Nilikuwa nimeshuka nje
ya gari nikimsaidia abiria mmoja mwenye mguu moja kushuka. Mara alipofika chini
mbele yetu, lilisimama gari dogo, aina ya Landrover, lililokuwa na Wazungu
wawili. Waliniita. Nikawaendea. Mara tu nilipowakaribia gunia la mahindi
lililokuwa juu ya gari liliporomoka kwa kasi na kutua palepale nilipokuwa. Kasi
ya gunia hilo lilimwangusha yule
abiria na kumfanya ateguke mguu wa
pili. Ilibidi tumrudishe kwenye gari na kumpeleka hospitali moja ndogo huko
Iringa.
Ajali ya pili ilikuwa mbaya zaidi!
Ilikuwa katika milima ya Kitonga. Gari letu kongwe lilipanda kwa taabu sana
milima hiyo kiasi kwamba abiria wengi walishuka na kutembea taratibu, wakiwa
wamelitangulia gari. Tulibakiwa kwenye gari mimi na dereva pekee. Mara gari
ikaanza kurudi nyuma kwa kasi. Kwa kila hali lilielekea kuporomokea katika yale
mashimo makubwa ambayo hufanya abira wengine wafumbe macho kila wanapofika
hapo, kwa uoga. “Ruka nje!” dereva aliniamuru.
“Na wewe?” nilimuuliza. “Ruka.”
Alifoka
Nikafungua mlango na kuchupa nje.
Dakika hiyohiyo gari liliangukia upande nilioshukia na kunikosa kwa nusu nchi
tu! Mimi pamoja na abiria wangu ambao walikuwa wakishuhudia purukushani hiyo
tulilikimbilia gari kumwahi dereva. Tulimkuta akifungua mlango na kutoka nje
akiwa safi bila hata vumbi kana kwamba alijilaza tu. Kila mtu alishangazwa na
ajali hiyo.
Lakini ajali ya tatu ilishangaza
zaidi. Ilitokea miezi miwili baada ya ile ya mwisho. Tena ilitokea katika kituo
cha kazi, Mbeya. Tulikuwa tukilikagua gari kwa makini kabla ya kuanza safari
yetu nyingine ndefu ya mijini na mashambani.
Baada ya dereva kuwasha gari na
kubaini kasoro fulani katika mlio wake, alikagua maji, oili, mafuta ya breki na
kila kilichohitajika. Kila kitu kilikuwa safi. Alipoiwasha bado ilitoa mlio
usioeleweka. Akaniamuru niingie chini ya gari kuangalia kama kulikuwa na nati
au sukurubu yoyote iliyolegea. Nilikuwa tayari nimevaa vizuri, shati jeupe,
suruali nyeusi na tai shingoni. Nilijitazama, kisha nikakutazama huko chini
nilikotakiwa kuingia. Kulijaa vumbi
na topetope la manyunyu ya ukungu wa baridi.
“Hakufai,” nilimwambia dereva.
Aliponitazama aliridhia kuwa
sikustahili kuingia huko. Akaniamuru kuingia ndani ya gari, niwashe na kupiga
resi wakati yeye akikagua huko chini. Haikuwa kazi kubwa kwangu kufanya hayo.
Katika safari zetu nyingi nilikwishajua kuendesha gari vizuri, ingawa uzoefu
mdogo ulifanya niwe na wasiwasi kidogo.
“Washa!” dereva aliita toka chini.
“Kanyaga resi!”
“Kanyaga breki!”
Ni wakati nikikanyaga breki hiyo
lilipotokea jambo ambalo hakuna aliyeweza kuelewa. Nilisikia mlio wa ‘ka ka ka
ka’ kana kwamba kuna kitu kinachokatika. Haikuwa uwongo kwani mara hiyohiyo
niliona nyufa zikitokea kwenye bodi ya gari na baadaye sehemu iliyobeba injini
ikaanza kudidimia.
“Kalinga! Toka haraka!” Nilipiga
kelele nikifungua mlango na kuruka nje.
“Kanyaga bre….” Ilikuwa kauli yake
ya mwisho kabla injini haijadondoka chini na kumpondaponda vibaya sana.
Majirani walijitokeza na kumsaidia kumtoa chini ya injini hiyo ambayo ilikuwa
bado ikinguruma. Alikuwa akipumua, lakini hakuwa mtu wa kuishi. Uso mzima
ulikuwa umepondeka, kichwa na kiwiliwili vikiwa kama vimeachana.
Sikupata kuona kitu cha kutisha kama
kile maishani mwangu. Nilitetemeka mwili mzima huku machozi yakinitoka.
Nilitetemeka zaidi pale nilipokumbuka kuwa mimi ndiye niliyetakiwa kuwa chini
ya gari lile. Kwa maneno mengine, mimi ndiye ambaye ningekuwa taabani, nusu
maiti. Nilishukuru
pale nilipohisi mtu mmoja akinishika
mkono na kuniongoza taratibu hadi katika chumba changu cha nyumba ya wageni na
kuniketisha kitandani.
“Pumzika. Ikiwezekana lala. Usitoke
kwenda kula nje hadi masuala yote ya kumshughulikia marehemu yatakapokwisha,”
alisema.
“Ame… amekufa!” niliropoka. “Kwa
vyovyote vile.”
Nikainua macho kumtazama mfadhili
wangu huyu. Hakuwa mwingine zaidi ya yule mshauri wangu wa masuala ya madini,
ambaye mara ya mwisho nilipuuza kumsikiliza. Alikuwa akinitazama kwa huzuni,
lakini nilihisi macho yake yalikuwa yakinicheka na kunidhihaki kama yanayosema,
“Si unaona? Nilikuambia nini!”
Kwa sauti alinieleza kile ambacho
alidai alitaka kunieleza toka awali, lakini, ‘nikampuuza!’kuhusu sifa mbaya za
mzee Ayubu, “Ni mtu hatari sana. Ni mshirikina kupita kiasi. Marehemu Kalinga
ni mtu wa tano aliyepoteza maisha katika mazingira ya ajabuajabu katika ajali.”
“Kwa vipi?” nilimuuliza. “Inakuwaje
mambo hayo?” “Ushirikina.”
“Ushirikina?”
Akaamua kunifafanulia. “Inaaminika
mzee Ayubu alipata utajiri wake kwa njia ya ushirikina. Kabla hajawa na kitu
alifiwa na mkewe katika mazingira ya kutatanisha. Mara akaibuka na kununua
magari kwa mpigo. Kipindi fulani alionekana kulegalega kiuchumi mtoto wake
mkubwa naye akafa kiajabuajabu. Akaibuka tena na kuongeza magari. Lakini kwa
kuwa mali ya haramu haidumu magari yake nayo yaliandamwa na mkasa huu na ule.
Mara yapate ajali, mara yaharibike. Mawili yalipata kuibuka bila sababu
yoyote.”
Nilimsikiliza kwa mshangao.
Nikayakumbuka yaliyonikuta mimi mwenyewe kule Sumbawanga ya Mmanyema kudaiwa
kutaka kunigeuza ndondocha.
“Hivi ni kweli mambo haya yapo?”
nilimuuliza.
Swali hilo ambalo lilimfanya
anitazame kama mdudu kwa dharau. “Unauliza ni kweli? Huna hakika! Hujui kuwa ni
wewe uliyekusudiwa? Kalinga amekufa kwa bahati mbaya tu. Wewe ndiye hasa
uliyehitajika!” alisisitiza.
“Mimi! Kwa nini mimi?”
“Kwani hukumbuki mara ngapi
umenusurika?” alinijibu kwa swali jingine. “Ni wewe uliyekuwa chaguo lake. Damu
za wengine wote waliokutangulia hazijafaa. Wewe toka alipokutia machoni
alishajua u chaguo lake,” alinijibu.
“Alijuaje kuwa damu yangu itamfaa?”
nilisisitiza. Aliendelea na mtindo wake wa kunijibu swali kwa swali,
“Kwani hujui?” alinihoji. “Unataka
kusema kuwa hujui kuwa una alama?”
“Alama! Alama gani?” Nilihoji kwa
mshangao uliochanganyika na hofu.
Akaangua kicheko. baadaye alisema
taratibu., “Usijifanye mtoto kuliko ulivyo. Una alama ya shari. Iko wazi usoni
mwako kwa kila mjuzi wa mambo atakayekutazama usoni mara moja. Hapo ulipo una
elimu ya kutosha lakini haikusaidii! Una nyota lakini haing’ari! Wewe si mtu wa
kuhangaika kama unavyohangaika. Unahitaji kusafishwa, kufutiwa alama hiyo.
Vinginevyo, maisha yako yataendelea kuwa kama ya mbwa koko asiye na mwenyewe.”
Niliyatafari maneno na hoja zake.
Chembechembe za ukweli zilikuwa nyingi kuliko uongo. Kwa mara ya kwanza
nilijikuta nikipatwa na hofu kubwa juu ya maisha yangu, hofu ya kufa Kama mbwa
koko kama alivyonieleza. Leo niko
hapa kesho niko pale! Kila
ninachoshika hakishikiki! Nadhani machozi yalinilengalenga au kunitoka bila
taarifa, kwani nilihisi mkono wa jamaa yangu huyo ukiwa begani kwa namna ya
kunifariji; kitendo ambacho kilifuatiwa na sauti yake yenye huruma
aliponiambia, “Usijali mdogo wangu, nitakusaidia.”
“Utanisaidiaje?” nilinong’ona.
“Nitakupeleka mahala, utasafishwa
vizuri. Baada ya
hapo utaona milango yote
uliyofungiwa ikifunguka.”
Bado nilikuwa na wasiwasi.
“Utanipeleka wapi?” Nilimuuliza.
“Kilwa.”
“Kilwa?”
“Naam. Kuna wajuzi wa mambo haya na
gharama zake ni nafuu. Utaoshwa utasafishwa na kukaangwa upya. Hakuna
atakayekugusa.”
* * *
Mipango ya safari ya Kilwa ilianza
mara baada ya mazishi ya dereva Kalinga. Yalikuwa mazishi yaliyoudhuriwa na
takribani kila mkazi wa Mbeya, waliomfahamu na wasiomfahamu. Wakati wote wa
msiba hadi matanga lilisemwa hili na lile kufuatia muujiza ule wa kifo chake.
Jina la mzee Ayubu lilikuwa mdomoni mwa kila mtu. Wako waliomwita ‘mchawi’
wengine walimwita ‘mshirikina.’ Lakini walikuwepo wengine waliokuwa wakimtetea
kwa madai kuwa anarogwa na watu wenye kijicho kwa mali na jitihada zake. Mradi
kila mmoja alikuwa na lake la kusema.
Mzee Ayubu mwenyewe alikuwa mtu wa
kuhurumiwa sana. Katika kipindi chote hicho cha msiba alikuwa mkimya muda wote
akiwa kajiinamia. Haikuwa rahisi kujua iwapo minong’ono na macho ya kusengenya
ya waombolezaji wengine
ilihusiana na ukimya wake au la.
Nilimhurumia zaidi pale nilipomwita
chemba na kumuarifu kuwa kazi kwake basi. Alishtuka kama aliyeguswa na waya wa
umeme. Nilihisi machozi yakimlengalenga pale aliposema, “Unajua ni wewe
ninayekutegemea? Nakuhitaji sasa zaidi ya wakati mwingine wowote ule. Kuondoka
kwako itakuwa sawa na kuondoka kwa roho yangu.”
Nilitamani kumsikiliza. Nilitamani
kufutilia mbali uamuzi wangu na kurudi kazini kwa kumhurumia. Lakini
nilijihurumia pia, zaidi ya nilivyomhurumia yeye. Nikapiga moyo konde na
kuung’ang’ania msimamo wangu. Hakuwa na la kufanya zaidi ya kunilipa madai
yangu kisha tukaagana bila kuangaliana machoni.
Mfadhili au mshauri wangu mpya,
ambaye sasa nilimfahamu kwa jina kuwa aliitwa Bushiri Mtanashati, alinipongeza
kwa uamuzi wangu wa kiume. “Ni muhimu sana kwa mtoto wa kiume kujua na kusema
‘ndiyo’ au ‘hapana’. Ukishindwa hilo utaishia kuwa hamnazo.”
Akili yangu ilikwisha hama kabisa
toka Mbeya sasa ilikuwa Kilwa. Nilikuwa nikitafakari kile ninachofahamu juu ya
mji huo ambao una historia kubwa kote duniani.
Kufika kwangu Kilwa kungefanya
nifike Pwani na kuiona bahari kwa mara yangu ya kwanza, bahari maarufu ya Hindi
ambayo jiografia inaonyesha kuwa ndiyo inayolinganisha bara letu la Afrika na
lile la Asia. Bahari hiyo naambiwa ina maji mengi lakini hayanyweki kwani yana
chumvi tofauti kabisa na maji ya maziwa yetu kama Nyanza na Tanganyika ambayo
yanafaa kila aina ya matumizi.
Kihistoria Kilwa ni miongoni mwa
miji michache katika Pwani ya Bahari ya Hindi ambayo ilikuwa na idadi kubwa ya
watu walioishi pamoja. Hali hiyo ilisababisha uwe mji wa
kwanza kibiashara katika nchi yetu.
Historia hiyo ilijengeka zaidi April 15, 1497 pale inapodaiwa kuwa mtu mweupe
wa kwanza alipokanyaga ardhi ya Tanganyika, kupitia Kilwa katika jitihada zao
za kutafuta biashara. Juni 2, mwaka uliofuata Mreno aliyeitwa Vasco da Gama,
akiongoza kundi kubwa la watu walifika Pwani ya Tanganyika. Tamaa na uroho wa
da Gama vinaaminika kuwa chanzo cha ukoloni wao nchini. Hivyo ilipofika mwezi
wa Julai, tarehe 16, mwaka 1500 wakazi wa Kilwa walikuta bendera ya utawala wa
Kireno ikipepea juu ya vichwa vyao. Miaka miwili baadaye wakazi hao wa Kilwa
waliamriwa kuanza kulipa kodi ya kichwa kwa serikali ya Ureno na hivyo kuufanya
mji huo kuwa koloni la kwanza la wageni katika Tanganyika.
Utawala wa Wareno haukuja kwa
urahisi kiasi hicho. Baada ya da Gama lilifuata kundi la pili, lililoongozwa na
Pedro Cabral, kamanda katika jeshi la wanamaji. Waliuvamia mji kwa mizinga,
kusambaratisha wakazi na wengi kuuawa kabla ya kufanikiwa azma yao. Baada ya
hapo walimwekea gavana wao wa kwanza, Antonio Fernandes kama mtawala wa kwanza
wa Wareno nchini Tanganyika.
Miaka iliyofuata Kilwa iliondokea
kuwa lango kuu la biashara. Biashara iliposhamiri sana hapa miaka ya 1901 hadi
1914, ingawa ilipigwa marufuku tangu 1873, ilikuwa ile ya utumwa. Lakini pia
biashara za meno ya tembo, dhahabu, vipusa na simbi zilifanyika kwa kasi mjini
hapo zikivuta wafanyabiashara toka nchi mbalimbali za dunia kama China,
Uarabuni na India.
Mzunguko huo wa biashara pia uliwezesha
mazao mbalimbali kama mahindi, viazi na korosho. Aidha, matunda kama vile
mapera na mapeasi na mananasi ni sehemu ya ujio
huo wa Wareno waliopo nchini. Pamoja
na vyakula athari za Mreno katika utamaduni wa Tanganyika hazitaweza kufutika.
Kwa mfano, katika lugha ya Kiswahili maneno kama gereza, meza, leso, karata,
mvinyo na mbolea yana athari kubwa ya lugha ya Kireno.
Kwa mujibu wa kumbukumbu zangu
maeneo mengi ya Kilwa ni vivutio vikubwa kwa macho ya mwanadamu. Kwa wapenzi wa
mazingira kitu cha kwanza kitakachonasa macho yake ni ile delta kubwa ya mto
Rufiji. Delta hii ya aina yake inapambwa zaidi na miti aina ya mikoko
iliyoizunguka miti, miti ambayo huota majini na hivyo mashina yake yenye mizizi
kuwa maficho na mazalio ya samaki aina mbalimbali hasa kamba.
Kwa mwanahistoria delta hii ni
hadithi ya pekee. Ni humo ambamo nguvu za Mjerumani katika Tanganyika zilipata
pigo lake la kwanza pale manowari yake ya kivita, Konigsberg ilipopatwa na
mkasa wa kuharibika na hivyo kuruhusu kipigo ambacho hawatakisahau. Magofu ya
Kilwa Kivinje, Kilwa Visiwani, visiwa vya songo mnara, Songalungu, Sanje na
Kati na Sanje ya Majoma, mapango ya Chetasui, Mkondaji, Mbaga
, Kiinja na Maloho, Jiwe la Mzungu,
Kilola Mbani ni miongoni mwa maeneo ambayo mwanahistoria angesisismkwa sana
kuyaona kwa macho yake.
Na mwana utamaduni naye atavutiwa na
ule mchanganyiko wa tamaduni za makabila mbalimbali ya eneo hilo kama Wamatumbi
na Wangino na ule wa Waarabu na kuzaa kitu ambacho baadhi ya watu hupenda
kukiita ‘waswahili’. Makabila hayo makuu pamoja na na yale ya Wasongo, Wambana,
Wambamula, Wamasoko na Washirazi ni sehemu ya utamaduni wa Kilwa. Wengine ni
Wamachinga,
Wamakonde, Wayao, Wamera na
wengineo. Wengi kati yao wamerithi dini na mila za kiarabu kwa kiwango kikubwa.
Hata hivyo, ndani kabisa ya mioyo yao wengi wao bado ni watu walewale, wenye
imani na tamaduni zilezile za asili yao.
Kwa mfano, wakati kwa Waarabu watu
wa Kilwa wamerithi utamaduni ule ambao hufanya mtoto wa baba mkubwa na wa baba
mdogo waweze kuoana bila pingamizi lolote, bado taratibu zao za jadi katika
masuala kama jando na unyago ni za asili zaidi. Mtoto wa kiume hupelekwa itani,
yaani jandoni afikapo umri wa kati ya miaka kumi na kumi na nne. Baada ya hapo
hupelekwa utagoni, ambako hukaa muda mrefu wakifundwa mila, tamaduni na wajibu
wao kwa jamii. Hatua ambayo inapokamilika hufuatwa na sherehe maalumu yenye
chakula maalum ngando ambacho huandaliwa kwa majani ya mti maalumu, mfulu,
ambao umefanana sana na vidole vya ndege wanayemwita kituku, kwetu akiwa ni
njiwa.
Masuala hayo ya jando huenda
sambamba na yale ya unyago kwa wasichana. Hata hivyo unyago hauna mambo mengi
sana. Siku ya kwanza binti ambaye amefikia hadhi ya mwali hukamwatwa na
kufungiwa ndani akiitwa ‘kukujike.’ Siku ya pili hutapishwa kwa dawa maalumu,
chini ya uongozi wa kungwi mkuu. Siku ya tatu hurudishwa nyumbani kwao ambako
huogeshwa, kupakwa mafuta na kuvishwa kanga mpya. Toka hapo yuko huru kwa
mchumba yeyote anayestahili kumposa.
Hiyo ndiyo Kilwa, Kilwa ambayo
niliifahamu vilivyo kinadharia, baada ya kusoma na kusikiliza simulizi za watu
mbalimbali juu ya mji huo wa kihistoria, mji ambao siku mbili tatu zijazo
ningeutembelea na kujionea kwa macho yangu mwenyewe siri ya umaarufu huo. Siri
hiyo ingesaidia
kuniondolea ‘alama’ katika uso
wangu.
Maandalizi ya safari yalikuwa
yakiendelea vizuri. Rafiki na mshauri wangu mpya, Bushiri Mtanashati, alikuwa
mtu wa kushughulika kinyume kabisa na siku za awali ambazo nilimwona akiwa
amekaa bure muda mwingi. Alienda huko na huko kufanya utafiti wa njia bora
zaidi, gari lipo na lini linaondoka. Mara mbili alichukua pesa kwangu kwa
maelezo yaleyale ya ‘Maandalizi ya safari.’
Nilikuwa na pesa za kutosha na
nilitaka ‘alama’ iondolewe haraka katika paji langu la uso. Hivyo, sikuwa mtu
wa kusita kila nilipotakiwa kutoa. Lakini pale alipokuja kwa mara ya tatu,
akiwa amelewa, na kuniomba nimpe pesa zaidi nilianza kumtilia mashaka. “Leo
unataka za nini?” nilimuuliza.
“Maandalizi.” “Yapi?”
“Kwani hujui?” aliuliza kwa sauti
yenye hasira kidogo “Hii ni safari ndefu. Safari ngumu lakini muhimu sana
kwako. Kivuli cha kifo kinakufuata popote uendapo. Usipokiondoa huna uhai, pesa
unazotafuta hutazifaidi.”
Sikupenda kubishana naye. Nikampa,
shingo upande. Siku hiyo sikumwona tena hadi kesho yake akiwa mchovu sana, bila
shaka kwa ulevi. “Safari imewiva. Kesho mchana tunaondoka. Usiwe na wasiwasi
mdogo wangu,” aliniambia akijilaza juu ya kitanda changu na kupitiwa na
usingizi.
Wasiwasi nilikuwa nao. Bushiri
alinitia wasiwasi. Tabia yake, maneno yake na sasa vitendo vyake vilianza
kunipa picha tofauti kabisa na ile ya awali, kabla hajautia mkono wake katika
mfuko wangu. Alikuwa ameshinda amekaa, ghafla amekuwa hapatikani. Alikuwa
halewi, mara amekuwa mlevi! Nilimtazama wakati kalala chali, akikoroma kama
nguruwe
aliyejeruhiwa. Karatasi mbili tatu
katika mfuko wake wa shati zilikuwa zikichungulia nje. Nikashawishika
kuzichomoa ili kujua kama zilikuwa tiketi au la. Haikuwa tiketi. Moja ya
karatasi hizo kilikuwa kipande cha kodi ya kichwa cha miaka miwili iliyopita. Ni
jina kwenye cheti hicho ambalo liliniacha hoi zaidi. Abdallah Jongo! Mkazi wa
Kisarawe! Sio Shubiri Mtanashati tena! Wala hatoki tena Newala ambako alisema
ni jirani sana na Kilwa!
Nikakumbuka alivyonieleza kwa taabu
sana jina na historia yake fupi baada ya kumsaili mara wa mara.
Mimi: Unajua hujapata kunitajia jina
lako? Yeye: Hivi sijakutajia? Naitwa … Bushili.
Mimi: Bushili au Bushiri? Yeye:
Bushiri
Mimi: Kabila lako? Yeye: M-makonde
Yeye: Mmakonde wa wapi? Wa Msumbiji?
Yeye: (Akicheka) Hapana. Wa
Tanganyika hapahapa. Ingawa nina wajomba wengi huko Nampula, Msumbiji. Mimi
natoka Newala. Ndiyo maana Kilwa naijua vizuri sana.
Mie: Mimi nilidhani wewe Mnyakyusa,
Mbungu au Muandali wa hapahapa Mbeya.
Yeye: (Akacheka tena) Hapana. Wengi
wanafikiri hivyo. Wengine wananiita Mmalila, wengine Msangu, wengine Mbungu.
Sijui kwa nini. Mimi Mmakonde bwana.
Mie: Mbona huna ndonya? Wamakonde
wengi wana
ndonya.
Yeye: Nilinusurika. Sikukulia kule
sana. Hata kilugha naongea kwa taabu sana.
Maongezi hayo sasa niliyatilia
mashaka kutokana na
kulibaini jina lake jingine kwenye
cheti hicho. Karatasi ya pili ilikuwa bili ya vinywaji ambavyo ama alikunywa
ama anadaiwa. Senti hamsini! Fedha ambazo zilitosha kununua shati jipya,
suruali mpya na viatu! Nikaweka nadhiri kutompa hata senti yangu moja bila
uthibitisho wa kile ninachokwenda kufanya.
Safari ya kesho, ambayo tayari
niliitilia mashaka, ilipatwa na pigo jingine. Tajiri yangu wa zamani, mzee
Ayubu alikufa ghafla. Maiti yake ilikutwa ikining’inia kwenye kamba, juu ya
mwembe uliokuwa nyuma ya nyumba yake. Alikuwa amejinyonga. Nilisikitika sana na
kujikuta nikilia kama mmoja wa jamaa zake wa karibu.
Mara baada ya mazishi jambo jingine,
kubwa zaidi, lilitokea na kubadilisha kabisa ramani ya safari yangu iliyokuwa
kichwani.
SURA YA KUMI
Tanga, kama Manamba
osa langu, ambalo nililifanya bila
kukusudia ni kujisahau. Kwa maneno mengine, ni kuyafumbia macho mabadiliko ya
umri na maumbile yangu
kwa muda mrefu. Ni kosa hilo
lililoniletea matatizo ya kisheria, dhidi ya serikali ya Mwingereza na mfalme
wao George.
Nilikuwa nimebadilika. Nilirefuka
kiasi cha watu wengi wanaoitwa warefu kulazimika kunyanyua nyuso zao ili
kunitazama usoni. Sikupata kuwa mnene, lakini mwili wangu ulijaza vizuri na
kunipa ukakamavu na kila dalili ya afya njema. Nadhani sura yangu ilivutia,
kwani nilipata hisia kuwa wasichana wengi walipenda sana kuzungumza na mie,
wakati mwingine bila sababu za msingi. Na pale nilipowakazia macho wengi wao
waliinama kwa aibu kuyakwepa macho yangu.
Rafiki zangu huko mtaani nao
walinishangaza. Walianza kunipisha kila nilipotokea, huku ‘shikamoo,’
zikiwatoka baadhi yao. Heshima hizi zilinifanya nisite kuzipokea kwa ukunjufu
huku nikijawa na mshangao ulioambatana na maswali tele. Yakoje mambo haya? Au
mavazi mazuri ninayovaa na usafi wa mwili wangu vinachangia kunipa heshima?
Lakini ni jana tu nilipoweza kupata
majibu ya fumbo hilo. Nilikuwa nimetoka kuoga, tayari nimepaka mafuta na sasa
najikagua kwenye kioo chenye ukubwa
wa kiganja changu. Niliridhishwa na nywele zangu nyeusi, zilizosheviwa vizuri.
Nilivutiwa na sura yangu ang’avu, yenye pua lililochongoka kiasi cha baadhi ya
watu kunifananisha na Watutsi. Mara macho yangu yakavutwa na kitu kigeni katika
uso wangu huo. Kwenye kidevu changu, chini ya mdomo, palikuwa na vijinywele
vitatu ambavyo havikupaswa kuwa pale. Nilidhani ni nywele zilizokatika toka
kichwani wakati nachana, lakini pale nilipovikung’uta kwa kidole na kuona
haviondoki ndipo nilibaini kinachotokea. Ndevu! Nimeanza kuota ndevu! Hatua
ambayo ilikuwa na tasfri moja tu; Nimekua!
Sina budi kukiri hapa kuwa kubaini
hilo kulinishtua sana. Sikuona kuwa ilikuwa habari njema kwangu kuingia katika
safari ya utu uzima bila kutarajia. Sikuwa nimejiandaa, si kielimu si kiuchumi.
Bado nilikuwa na ndoto za kurudi shule na kujipatia elimu ili niweze kupata
ajira yenye hadhi na wajibu mkubwa zaidi, ambao kwa kawaida huambatana na
malipo makubwa zaidi. Kwa kuona dalili za kuzeeka zikianza, nilianza kupata
mashaka iwapo nitakaa niyafikie matumaini hayo.
Mawazo hayo yalitembea kichwani
mwangu jana tu, leo nilipata majibu. Tulikuwa nje ya hoteli yangu, tukibishana
na Bushiri Mtanashati, au Abdallah Jongo, juu ya kumpa fedha zingine za kile
alichokiita ‘kukamilisha’ mikakati ya safari. Nilimkatalia katakata na
kumwambia wazi kuwa hata safari yenyewe naifikiria kwa mara ya pili.
Alinitazama kwa macho yake makali,
yaliyowekwa katika hali ya kunitisha na kunihurumia pamoja. Kisha, kwa sauti ya
upendo aliniambia, “Mdogo wangu naona hujipendi. Hizo fedha zitakusaidia nini
kama kila uendako unafuatwa na
kivuli cha mauti? Angalia, utakufa
siku si zako.”
Mie pia uvumilivu ulianza
kunishinda. “Hivi wewe ni nani hasa hata uwe na kauli juu ya kifo au uhai
wangu?” Nilimuuliza. “Wewe ni nani?” niliongeza, “Mungu au Shetani?”
Kauli yangu ilimshangaza kuliko kitu
kingine chochote kile. Macho yake yalibadilika na kuwa makali kama simba
aliyeona kila dalili ya windo lake kupokonywa. Alifungua mdomo wake kutaka
kutamka jambo. Lolote alilotaka kusema lilitoweka pale tulipowaona tarishi
watatu wa bomani, walipotujia na kusimama kwa namna ya kutuzingira.
“Toeni vipande vyenu,” tarishi mmoja
kati yao aliamuru baada ya kutuuliza majina yetu.
Nilimwona Bushiri Mtanashati
akitetemeka. “Vipande gani?” aliuliza.
“Vipande vya kodi,” alifafanua.
“Kodi?” niliropoka. “Ilikuwa mara
yangu ya kwanza maishani kuulizwa kodi. Ni hapo nilipobaini kuwa utoto
ulikwishanitoka na nimeingia ukubwani. “Lakini mimi sijaanza kulipa kodi,”
nilijitetea.
“Kwa nini?” Yule msemaji wao
alihoji.
“Mimi bado. Umri haujafika. Isitoshe
mimi ni
mwanafunzi.”
Askari huyo na wenzake waliangua kicheko.
“Umri bado!” mmoja wao alisema.
“Mwanafunzi!” mwingine alitamka
“Mwanafunzi!” aliongeza yule msemaji wa kwanza. “Tunakuona mwaka mzima hapa
unafanya kazi mbalimbali, leo umekuwa mwanafunzi! Pita huku!” Nilielekezwa
upande ambao kulikuwa na watu wengine kadhaa, bila shaka mateka kama mimi.
Nikaenda na kujiunga nao.
“Na wewe?” walimgeukia Bushiri
Mtanashati.
Huku akitetemeka alijishikashika
mifukoni na kuchomoa pochi yake ambayo ilikuwa na vyeti na nyaraka zake kadhaa.
Alitoa mojawapo kwa wasiwasi na kuitazama. Akataka kuirejesha mfukoni. Tarishi
mmoja akawa mwepesi wa mkono. Aliipokonya pochi hiyo na kutoa nyaraka hizo
ambazo alizisoma taratibu na kisha kumtazama Bushiri kwa mshangao.
“Inaonekana umelipa kodi mara ya
mwisho miaka miwili iliyopita,” alimhoji.
Bushiri alikubali kwa kichwa.
“Halafu,” tarishi huo aliongeza
akiwa kamkazia macho, “Umesema jina lako ni nani vile?”
Bushiri alibadilika. Niliona
akitokwa na jasho huku miguu yake ghafla ikionyesha kukosa nguvu za kukibeba
kiwiliwili chake. Alifunua mdomo kutaka kutamka neno ambalo halikutamkika au
kusikika.
Tarishi alimkazia macho. “Hujui jina
lako?” alimuuliza
tena.
Tarishi wengine walivutiwa na
mjadala huo. Wakakiomba
kitambulisho hicho na kukitazama kwa
zamu. Kila mmoja alitikisa kichwa huku akimtazama Bushiri.
“Za mwizi arobaini,” mmoja wao
alisema. “Arobaini za leo zimetimia. Unajiita Bushiri Mtanashati wakati jina
lako ni Abdallah Jongo! Jongo tunayemfahamu sisi, ambaye anatafutwa kwa miaka
miwili sasa ni mhalifu aliyemwibia mwajiri wake fedha nyingi kule Pangani.
Kumbe muda wote umejificha hapa? Twende,” walisema wakimkamata na kumtia pingu.
“Naomba nizungumze faragha na mdogo
wangu,” Bushiri au Abdallah alisihi akinitazama mimi.
“Nani mdogo wako? Huyu?” Waliuliza.
“Mimi siyo mdogo wako” niling’aka
mara moja. “Nimemfahamu hapahapa, tena kwa jina la Bushiri Mtanashati. Hatuna
uhusiano wowote wa damu wala kabila.”
“Mtanashati sio?” Tarishi mmoja
alisema akicheka. “Basi atafanya utanashati wake akiwa jela. Wewe suala lako ni
dogo. Tutakupeleka bomani ukalipie kodi ya faini. Kama huna utapelekwa manamba,
Tanga, ukajifunze kutafuta fedha kwa kukata mkonge.”
***
Safari ya Kilwa ilikufa. Safari ya
Tanga ikazaliwa. Nilikuwa katika kundi la watu wasiopungua arobaini, wenye umri
tofauti, waliokuwa wakiisubiri safari hiyo. Nadhani mimi nilikuwa mdogo kuliko
wote kiumri. Lakini kwa ajili ya umbile langu niliweza kujumuika katika kundi
hilo bila ya yeyote kunishuku.
Sikuwa na sababu kubwa ya kuwemo
katika kundi hilo. Nilikuwa na fedha ambazo zingetosha kulipia kodi na bado
nikabakiwa na akiba. Aidha, barua ile ya Chifu Masanja na madaftari yangu toka
shule yangu ya awali Uhayani, ambayo niliyatunza kama roho yangu, vingetosha
kumwonyesha mkubwa wa hapo bomani na angeniachia mara moja. Lakini sikufanya
hivyo. Sikuona haja yoyote ya kubakia kusini, ambako sikuwa na kazi wala
mipango yoyote inayoendelea kiuchumi au kielimu. Hivyo, sikuona ubaya wowote
kusafiri bure, ukihudumiwa chakula na matibabu, hadi katika nchi mpya maishani
mwako. Si kuna mhenga mmoja aliyepata kusema kuwa bahati ya mwanaume iko
kichwani, miguuni na mikononi mwake? Huwezi jua, pengine huko ambako miguu
yangu inanielekeza ndiko iliko bahati yangu.
Hilo ni moja. La pili lililofanya
nipokee masaibu hayo ni umbali wa huku nyumbani. Lakini habari za watu wengi wa
kutoka kwetu waliokwenda huko kwa njia na mazingira kama haya zilikuwa nyingi.
Wengi wao wakiwa wamelowea hukohuko na kufanya makazi ya kudumu. Hivyo, uhakika
wa habari na hata uwezekano wa kusafiri toka huko hadi nyumbani ulikuwa mkubwa
sana.
Ni kwa mtazamo huo ndipo niliufyata
ulimi wangu nisiweze kujitetea na baadaye kukusanya vitu vyangu vyote ambavyo
ningesafiri navyo kuelekea Mashariki ya Tanganyika.
Tulisubiri safari kwa takribani wiki
nzima, tukiwa tumefungiwa katika ukumbi mmojawapo wa Bomani. Mtu mmoja ambaye
sikupata kumfahamu alikuwa ameingiza nakala mbili tatu za magazeti ya Ngurumo
na Mamboleo ambayo hayakuwa na msomaji zaidi yangu. Gazeti jingine la lugha ya
kiingereza, Tanganyika Standard, ambalo lilikuwa limeanza mwaka 1930 niliweza
kupata nakala yake ya miezi kadhaa iliyopita. Ingawa nililisoma kwa taabu
kidogo kutokana na kiwango changu cha lugha ya Kiingereza bado nililielewa na
kunivutia kwa habari zake.
Bila mwenyewe kuwa na habari, tabia
hiyo ya kujisomea kwangu ilivuta macho ya mateka wenzangu pamoja na watekaji
wenyewe. Afisa mmoja Mzungu alipotembelea makazi yetu kukagua afya zetu
aliponikuta nimejiinamia nikisoma Tanganyika Standard alishangaa sana.
Alishangaa zaidi pale aliponihoji maswali mawili matatu kwa Kiingereza na
nikamjibu vizuri. Akaniuliza kwa nini niko pale. Nilipomjibu kuwa ni tatizo la
kodi alitikisa kichwa kwa masikitiko na kuondoka zake. Baada ya tukio hilo
nilianza kupewa jukumu la ukarani kwa kuratibu mambo mbalimbali ya manamba
wenzangu,
kuwaelekeza wagonjwa matumizi ya
dawa walizopewa na wakati mwingine ukalimani kwa wageni ambao hawakufahamu
kiswahili.
Sikubahatika kumwona tena bwana
Bushiri Mtanashati au Abdallah Jongo. Tangu pale alipotiwa pingu na kuburuzwa
huku akinitupia jicho la ‘kwa heri’ lililoonyesha chuki na hasira dhidi yangu
kwa kile alichokichukulia kama kumsaliti, alitupwa gerezani kusubiri safari ya
pwani kujibu tuhuma dhidi yake. Kwa jumla, nilishukuru kutengana naye, kwani
nilihisi kuwa angenielekeza shingoni badala ya kileleni. Ndiyo, alinishauri
mengi juu ya masibu katika maisha. Lakini gharama ya ushauri wake ilikuwa kubwa
kuliko mahitaji halisi. Kwa vyovyote vile, kama ningeendelea naye ningejikuta
katika lindi kubwa la umasikini pengine na madeni pia badala ya faraja
aliyoniahidi. Kubainishwa kwake mapema kuwa ni mtu wa aina gani kuliniokoa na
mengi.
Safari ilianza alfajiri ya siku ya
nane toka tulipokamwatwa. Tulisafirishwa kwa lori kuukuu, ambalo mlio wake
ulinikumbusha lori la hayati Ayubu ambalo nililitumikia kama kondakta kwa muda
mrefu. Sasa tulikuwa zaidi ya watu tisini baada ya wengine kuletwa siku mbili
kabla ya safari. Tulijazwa nyuma ya lori hilo, watu na mizigo yetu na
kung’ang’ania kuta za bodi ili kujiepusha na kuanguka kwa kuyumba kwa gari
kulikosababishwa na ubovu wa barabra. Ilikuwa safari yangu nyingine ngumu,
ndefu na ya kukatisha tamaa. Lakini Mungu si Athumani, siku ya nne tangu
tulipoanza safari tulifika Muheza ambako tulishushwa ili kusubiri kugawanywa
katika mashamba ya mkonge.
* * *
Umepata kulisikia kabila la
Wandorobo? Hawa kwa kiasi fulani ni watu wa porini. Wanapenda kuvaa
kiutamaduni, pande la ngozi ya nyama (Lusira) au kaniki, ikiwa imefunikwa
sehemu tu ya mwili wake. Nywele zao huwa ndefu na hupendelea kuzivuta kwa
nyuma. Kwa wanaume mara zote utamwona akiwa ameshika upinde, podo la mishale
ubavuni na kishoka, ambacho wenyewe hukiita ‘kitodyo’ mkononi.
Kwa kawaida Wandorobo ni watu wa
kuhamahama, mara msitu huu mara ule. Chakula chao kikuu ni nyama za porini,
mizizi na asali. Aidha, ni wa matunda ya porini yatokanayo na mimea kama
ngabaito na olugumu. Wakati wa mvua Wandorobo hujisitiri kwa kujenga mabanda ya
ngozi za wanyama, mfano wa mahema.
Watu hawa ni mashujaa wa aina yake.
Si waoga, hivyo hawapendi au kujali sana umoja. Mtu na mkewe wanaweza kukaa
porini kwa miaka bila hofu wala kuhitaji msaada wa watu wengine. Inaaminika pia
kuwa wana uwezo mkubwa wa kutumia miti shamba kuyatawala mazingira yao kiasi
cha wanyama wakubwa kama simba, chui na majoka kuwakimbia.
Kuna hadithi nyingi za miujiza ya
watu hawa. Moja ni ile inayosimulia juu ya wawindaji saba walioingia katika
msitu mmoja mkubwa kwa matarajio ya kupata wanyama. Si kwamba hawakufanikiwa
tu, bali pia walipotea mchana kutwa wasiweze kujua njia ya kurudi kwao. Ulipofika
usiku, wakiwa wamekata tamaa waliona mbuyu mkubwa wenye pango kwenye shina,
ambalo lingetosha kuifadhi watu kumi na wa tano au zaidi. Wawindanji hao
waliingia katika pango hilo kwa matarajio ya kupitisha usiku. Ikatokea kuwa
pango hilo lilikuwa makazi ya joka kubwa aina ya chatu. Lilirejea na kuingia
pangoni humo. Wawindaji wale, kwa hofu kubwa walitimka mbio kila mmoja
akikimbilia anakokujua, kuokoa roho yake.
ITAENDELEA

0 Comments