IMEANDIKWA NA : FAKI A FAKI
*********************************************************************************
Sitausahau mwaka elfu moja mia tisa na sabini na nane. Nina sababu tatu za kutousahau mwaka huo. Sababu ya kwanza ni kuwa kulitokea vita vya Kagera. Majeshi ya Iddi Amin aliyekuwa Rais wa Uganda yalivamia nchi yetu na kusababisha maafa makubwa.
Kaka yangu wa kwanza alikuwa ni miongoni mwa askari waliokuwa mstari wa mbele waliokwenda kuikomboa nchi yetu na aliuawa katika vita hivyo.
Sababu ya pili ya kutousahau mwaka huo ni kuwa ndio mwaka nilioanza kufanya kazi. Niliajiriwa na kampuni ya STC iliyokuwa na maduka ya ushirika nchi nzima. Na mwaka huo pia ndio nilitimiza umri wa miaka ishirini.
Lakini sababu ya tatu na iliyokuwa kubwa zaidi ya kutousahau mwaka huo ni kuwa nilikutana na tukio ambalo lilibadili maisha yangu.
Je lilikuwa tukio gani?
SASA ENDELEA
Ilikuwa februari 18 mwaka 1978. Nilikuwa mmoja wa wafanyakazi wa STC tuliokopeshwa pilipiki. Furaha yangu ikanituma kwenda kuangalia sinema. Wakati huo hakukuwa na video wala televisheni. Kulikuwa na majumba ya sinema. Kwa pale Tanga nilikokuwa naishi kulikuwa na majumba matatu ya sinema.
Kulikuwa na Majestic Sinema, Novelty Sinema na Regal Sinema. Majestic Sinema ndiyo iliyokuwa kubwa na maarufu zaidi na ilikuwa katikati ya jiji.
Mimi nilikuwa mpenzi sana wa filamu za kihindi. Filamu za kihindi zilikuwa zikioneshwa siku ya jumapili tu, yaani mara moja kwa wiki na zinakuwa zinajaza watu kuanzia wahindi wenyewe hadi waswahili.
Tikiti huanza kukatwa tangu asubuhi. Ukienda jioni hupati kitu. Nakumbuka filamu iliyokuwa inaoneshwa siku hiyo iliitwa Dost, ilikuwa filamu ambayo nilishapata sifa zake, hivyo kutokana na furaha ya kupata pikipiki nikaona niende nikaione.
Pikipiki tulikabidhiwa siku ya jumamosi, siku ya jumapili ndio niliamua kwenda kuitazama filamu hiyo ya Dost.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Nilikwenda na pikipiki yangu hadi Majestic Cinema. Nikaiegesha katika eneo la kuegesha na kwenda kupanga foleni. Nilikuta foleni ndefu ya watu waliokuwa wanakata tikiti.
Nilifika hapo saa nne asubuhi. Mpaka nafika kwenye kidirisha cha kukata tikiti ilikuwa saa tano kasorobo. Mbele yangu kulikuwa na watu watatu. Wakimalizika wao kukata tikiti ndio inafika zamu yangu. Akaja msichana mmoja ambaye alikuwa amevaa baibui na hijabu akaniomba nimkatie tikiti.
Ilikuwa ni kawaida mtu kukufata ukiwa kwenye foleni na kukuomba umkatie tikiti. Hivyo sikushngaa msichana huyo ambaye sikumfahamu aliponiomba nimkatie tikiti.
Alikuwa anataka kunipa pesa nikakataa kuchukua pesa yake.
“Nitakukatia kwa pesa yangu kisha utanipa” nikamwambia.
“Asante kaka yangu”
Alikuwa na sauti nzuri ya kusisimua.
Wakati amebaki mtu mmoja mbele yangu, kundi la vijana wakihuni likavamia pale kwenye kidirisha na kuharibu foleni, ikawa vurugu. Mmoja wa vijana hao alinibana na kunikatia vifungo vya shati langu. Nikajaribu kutumia nguvu mpaka nikafanikiwa kukifikia kidirisha, nikakata tikiti mbili za usiku.
Nikazitia mfukoni tikiti hizo kisha nikaanza kumtafuta yule kijana aliyeniumiza. Nikamuona akiuza tikiti yake kwa bei ya juu kwa mhindi mmoja. Nikamkwida ukosi na kumtikisa.
“Wewe mshenzi umenifanya nini pale?” nikamuuliza.
“Hebu niache fala wewe…” akaniambia huku akiukutua mkono wangu.
Nikamtandika ngumi moja tu iliyomtupa chini. Damu ikawa inamtoka mdomoni.
Yule msichana aliyeniomba nimkatie tikiti akanifuata haraka.
“Usipigane” akaniambia huku akinishika bega.
“Angalia jinsi alivyokata vifungo vyangu”
Nikamuonesha yule msichana papi za shati langu ambalo lilichomoka vifungo vitatu.
“Basi muache”
Yule kijana alinyanyuka na kukimbia.
Nilitoa zile tikiti mbili, nikampa tikiti moja yule msichana.
“Asante kaka yangu, ngoja nikupe pesa zako” akaniambia.
Nikaona nimuachie tu.
“Basi usinipe pesa, nimekukatia kwa pesa zangu”
“Kwnini unakataa pesa?” akaniuliza.
“Nimekukatia mimi kama zawadi yako”
“Asante kaka yangu”
“Haya, kwaheri” nikamuaga.
“Basi tutaonana jioni” akakiambia kichogo changu. Nilikuwa nimeelekea kwenye mlango nikitoka.
Nikiwa nje ya jumba hilo nilichukua pikipiki yangu nikaondoka kurudi nyumbani.
Nilikuwa ninaishi eneo la Mabawa kwenye nyumba ya kupanga. Nyumba yenyewe ilikuwa na sehmu mbili. Sehemu moja nilipangisha mimi na sehemu nyingine alipangisha kujana mmoja wa kichaga aliyekuwa akifanya biashara ya duka la nguo barabara ya kumi na tatu.
Nilipofika nyumbani niliingiza ndani pikipiki yangu nikakaa sebuleni kwangu na kutafakari.
Nilikuwa sijaoa, sikuwa na mke wala mtoto. Ndiyo nilikuwa naanza maisha. Wakati huo mzazi wangu aliyebaki alikuwa mmoja, ni mama yangu. Baba yangu alikuwa ameshafariki dunia miaka miwili iliyopita.
Mama yangu alikuwa akiishi barabara ya tisa kwenye nyumba yetu tuliyozaliwa. Kaka yangu wa pili alikuwa akiishi eneo la Chuda na kaka yangu mwingine aliyefuata alikuwa akiishi eneo la Kwaminchi.
Usiku ulipowadia nilitoa pikipiki yangu nikaenda kwenye mkahawa mmoja kula chakula kisha nikaongoza njia kuelekea Majestic.
Nilifika Majestic saa mbili na nusu. Sinema ilikuwa inaanza saa tatu hadi saa sita usiku. Baada ya kuegesha pikipiki yangu niliingia kwenye ukumbi huo nikatafuta siti yenye namba yangu nikakaa. Mpaka imebaki dakika moja kuanza trela, siti ya upande wangu wa kulia ilikuwa tupu. Nilishuku ilikuwa siti ya yule msichana niliyemkatia tikiti kwani siti hizo zilikuwa zikifuatana na namba zilizomo kwenye tikiti.
Ghafla taa zikazimwa na trela ikaanza. Hapo ndipo nilipomuona msichana akiingia na kuja kukaa kwenye kile kiti kilichokuwa kitupu. Alikuwa ni yule msichana niliyemkatia tikiti. Sikujua alijuaje kuwa kiti chake kilikuwa pale. Nikawaza kwamba pengine aliwahi kuingia mapema akakiona kiti chake kisha akatoka.
“Tumekutana tena” akaniambia huku akitabasamu.
“Nilikuwa najiuliza huyu msichana yuko wapi”
“Nilichelewa kidogo, unajua ninaishi mbali”
Sikumuuliza anaishi wapi, akili yangu ilikuwa kwenye ile trela iliyokuwa ikioneshwa.
Sote tukawa kimya. Tuliangalia trela hadi ikaisha. Msichana alitoka, mimi sikutoka. Baada ya muda kidogo alirudi akaketi kwenye kiti chake. Mkononi alikuwa ameshika chupa mbili za soda na pakiti mbili za karanga.
“Chukua soda” akaniambia huku akinipa ile chupa moja.
Nikaipokea.
“Chukua na karanga”
Akanipa na pakiti moja ya karanga.
“Asante’
Hapo hapo taa zikazimwa na filamu ya Dosti ikaanza. Ile filamu ilikuwa ikizungumzia marafiki wawili, mmoja kipofu na mwingine mlemavu wa miguu. Ilikuwa filamu nzuri na ya kusikitisha sana. Ilikuwa na nyimbo nne. Nyimbo tatu ziliimbwa na muimbaji maarufu wa India Mohamed Rafiy ambaye kwa sasa ni marehemu na moja iliimbwa na Usha Mangesh ambaye ni dada wa Lata Mangesh.
Sinema ilipomalizika tuliinuka kwenye viti na kutoka. Kwa vile kulikuwa na watu wengi, nilipotoka sikumuona tena yule msichana, nikaenda kuchukua pikipiki yangu nikaiwasha na kuondoka.
Kutoka Majestic Cinema nilishika barabara ya Eckenford hadi bustani ya Uhuru ambapo nilikata kushoto na kushika barabara ya Pangani. Wakati nalivuka eneo la Tangamano niliona mtu akinipungia mkono mbele yangu. Alikuwa mwanamke na nilihisi likuwa anataka kuniomba lifti.
Kusema kweli muda ule wa usiku nilikuwa sipakii mtu nisiyemfahamu hata kama ni mwanamke. Kwa hiyo nilitaka kumpita lakini pikipiki ikazimika moto ghalfa. Mwanamke huyo akaona nilisimama kwa ajili yake, akanifuata.
Alipofika karibu yangu nikaona alikuwa ni yule msichana niliyekuwa naye sinema. Nikajiuliza alifikaje pale wakati nilimuacha kule Majestic?
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Nilipomuona nikatabasamu.
“Ni wewe kumbe?” nikamuuliza.
“Ni mimi, naomba unisaidie lifti”
“Unaishi wapi?” nikamuuliza.
Kabla hajanijibu alikuwa ameshakaa nyuma yangu.
“Unaishi wapi?” nikamuuliza tena.
“Mikanjuni” akanijibu.
Nikaguna lakini bila kutoa sauti. Eneo alilolitaja, wakati huo lilikuwa kama pori la miti ya mikanju. Viwanja vilikuwa vikipimwa sasa na kama kulikuwa na nyumba zilikuwa chache na za kienyeji. Kwenda huko usiku ule ilikuwa ni hatari.
Lakini msichana alikuwa ameshakaa nyuma yangu akijisogeza upande wangu ili akae vizuri.
Nikajikuta nikipiga kiki ya pikipiki ili kuiwasha kwani pikipiki ilikuwa imezima moto. Pikipiki ikawaka, nikatia gea ya kwanza ya kuondokea na kuondoka.
Msichana aliupitisha mkono wake kwenye tumbo langu ili kujizua. Mkono huo uliniletea changamoto na hisia toauti kwenye akili yangu.
“Kama unakaa Mikanjuni kwanini unakwenda sinema za usiku?” nikamuuliza.
“Nimeshazoea” akanijibu. Kidogo aliliminya tumbo langu, pengine ni kwa bahati mbaya, nikashituka.
“Mbona unashituka?” akaniuliza.
“Nilikuwa najiweka sawa”
“Mh!” Msichana akaguna. Sikujua ni kwanini aliguna.
“Ulitegemea ungerudi nyumbani kwa usafiri gani usiku huu?” nikamuuliza.
“Ninaomba lifti tu kwa watu”
“Ukikosa lifti unakwenda kwa miguu?”
“Naweza kukodi teksi lakini sijawahi kukosa lifti hata siku moja”
Baada ya hapo tukabaki kimya.
Nilikwenda hadi Duga kisha nikakata kushoto na kushika barabara ya kuelekea Mikanjuni. Hapo ndipo nilipoanza kupita kwenye eneo la vichaka na miti ya mikanju.
Tulipoingia katika eneo la Mikanjuni nikamuuliza.
“Unaishi sehemu gani?”
“Twende tu, nitakuonesha” akaniambia.
“Una maana hatujafika bado?”
“Bado”
Nikaendelea kwenda mbele. Laiti angekuwa mwanaume mwenzangu, ningemshusha hapo hapo nikarudi kwa hofu ya kutaka kunipora pikipiki.
Sasa tulikuwa tunaingia kwenye pori kamili. Kulikuwa na nyumba moja moja tena zikiwa mbali mbali na hazina taa za umeme . Sehemu nyingi vilikuwa ni viwanja vitupu.
“Simama hapa hapa” Msichana akaniambia tulipokuwa tunaupita mti wa muwembe.
Nikasimamisha pikipki. Msichana akashuka.
“Asante sana kaka” akaniambia.
“Unaishi wapi?” nikamuuliza kwa sababu sikuona nyumba karibu.
“Naishi mtaa wa pili” akaniambia. Mtaa huo pia sikuuona lakini nilimkubalia ili niwahi kurudi.
“Uende salama, mimi nakwenda zangu” nikamwambia huku nikiigeuza pikipiki.
Nikamuona msichana akichapuka kuelekea mtaa huo aliosema. Nikatia gea kwa nguvu na kuingia gea ya pili na kuondoka.
Wakati narudi nilimsikitikia sana msichana yule, alikuwa anaishi pembeni sana na katika mazingira ambayo hayakulingana naye.
Nilipotokea kwenye barabara ya Duga nilikata kulia nikarudi nyumbani kwangu.
Nilifungua mlango nikaingiza pikipiki yangu ukumbini kisha nikaingia chumbani kwangu. Nilivua nguo nikajifunga taulo na kwenda bafuni.
Nilijimwagia maji ya baridi ili kuuosha mwili wangu ulikuwa umetota kwa jasho. Nilipotosheka nilirudi chumbani kwangu na kujiandaa kulala.
Asubuhi kulipokucha nilitoka kwenda kazini kwangu. Baada ya kama wiki moja hivi nilikutana tena na yule msichana. Nilikuwa nimekwenda katika duka moja la vitabu kununua kitabu cha “Mashimo saba ya Mfalme Suleyman”
Mara nyingi niwapo nyumbani hupenda kujisomea vitabu vya hadithi. Katika orodha yangu ya vitabu kitabu hicho hakikuwemo hivyo nikataka nikinunue ili niwe nacho.
Kabla sijaingia kwenye duka hilo nilikiona kitabu hicho kwenye safu ya vitabu vilivyokuwa kwenye kioo. Nilipoingia humo dukani nilimwambia muuzaji kuwa nataka kitabu cha Mashimo Saba ya Malme Suleiman.
“Vimekwisha” akaniambia.
“Kipo kimoja, nimekiona kwenye kioo” nikamwambia.
“Umekiona?” akaniuliza.
“Ndiyo nimekiona”
“Njoja nitazame”
Muuzaji huyo alizunguka nyuma ya kioo akakiona kitabu hicho.
“Ni kweli kipo, kilibaki kimoja tu” akaniambia huku akikifuta vumbi na kunipa.
“Bei gani?”
Akanitajia bei yake nikatoa pesa na kumlipa.
Wakati ninatoka nje ya duka nikakutana na msichana aliyekuwa akiingia dukani humo. Akanishitua aliponiambia.
“Kaka habari ya tangu siku ile?”
Nikaangaza macho yangu kumtazama. Nikamkumbuka. Alikuwa ni yule msichana niliyekutana naye sinema siku ile.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
“Oh nzuri! Hujambo?” nilijibu salamu yake.
“Sijambo. Leo tumekutana tena”
“Imekuwa kama bahati. Nilikuwa natoka kununua kitabu”
“Mimi pia nimekuja kununua kitabu. Nilikuwa nahitaji kitabu cha “Mashimo Saba ya Malme Suleiman”
“Vimeisha. Kilikuwa kimebaki kimoja tu nilichonunua mimi” nikamwambia.
“Kumbe wewe pia ulikuja kununua kitabu hicho hicho?”
“Nilikuja kununua kitabu hicho”
Nikakitoa kile kitabu na kumuonesha.
Akakishika na kukitazama.
“Una umuhimu nacho sana kwa leo na kesho?” akaniuliza.
“Ni kwa ajili ya kujisomea tu”
“Basi naomba uniazime kwa siku mbili tu halafu nitakurudishia”
Sikuwa na sababu yoyote ya kukataa. Nilihisi yule msichana alikuwa akikihitaji zaidi.
“Nitakuazima, sasa sijui nitakipata vipi?”
“Keshokutwa nitakuwa majestic Cinema, utakuja?” akaniuliza.
“Ninaweza kuja kwa ajili yako tu”
“Basi njoo usiku saa mbili na nusu hivi utanikuta nakusubiri pale nje”
“Kutakuwa na picha gani?”
“Picha nzuri ya James Bond”
“Inaitwaje?”
“Dk No”
“Inarudia. Nakumbuka Dk No ndio picha ya kwanza ya James Bond, ilitoka kwa mara ya kwanza mwaka 1961”
“Sijui. Mimi sikuwahi kuiona lakini ni ya Seen Conary mwenyewe?”
“Mimi pia sikuwahi kuiona ila niliisikia tu. Mbabe wake ni Seen Conary mwenyewe”
“Nimekuuliza hivyo kwa sababu kuna mtu mwingine anakuja kwenye picha za James Bond anaitwa Roger Moor”
“Ile ni ya Seen Conary si Roger Moor”
“Huyo ndiye ninayemtaka mimi”
“Basi mimi nitafika hapo Majestic Cinema keshokutwa”
“Asante kaka, ngoja niingie humu dukani nione kama nitapata vitabu vingine vya hadithi”
‘Sawa”
Msichana akaingia mle dukani na mimi nikapanda pikipiki yangu na kuondoka.
SASA ENDELEA
Yule msichana alikuwa ameniambia nikutane naye kesho kutwa saa mbili usiku nje ya Majestic Cinema. Ilipofika siku hiyo niliondoka nyumbani kwangu saa mbili usiku kuelekea Majestic Cinema kufuatia kitabu changu. Nilipofika ilikuwa saa mbili na nusu kama tulivyoahidiana na msichana huyo ambaye sikuwahi hata kumuuliza jina lake.
Nikamkuta amesimama mbele ya mlango wa jumba hilo akiwa na mavazi yake yale yale, baibui jeusi la kiiran na hijabu.
“Niko hapa nakusubiri” akaniambia.
“Nimeshakuona”
“Vipi hali yako?”
“Mimi sijambo, sijui wewe”
“Mimi mzima tu, karibu”
“Asante”
Msichana alikuwa ameshika tikiti mbili mkononi. Akanipa tikiti moja.
“Nimekukatia tikiti uingie”
“Mbona mimi sikupanga kuangalia sinema” nikamwambia huku nikipokea ile tikiti.
“Hukupanga? Si nilikwambia juzi…”
“Wewe ndio ulisema utakuja sinema, mimi nilikuwa nije kuchukua kile kitabu tu”
“Kwa vile nimeshakukatia, ingia tu tuangalie pamoja”
Wakati akiniambia hivyo watu walikuwa wanatoka ndani ya jumba hilo. Onesho la jioni lilikuwa limekwisha.
Tulisimama kwa pembeni kuwapisha watu hao, walipomalizika na sisi tukaingia. Tulitafuta siti zetu, tulipozipata tukaketi. Saa tatu kamili trela ikaanza. Baada ya trela kwisha msichana alitoka. Baadaye alirudi akiwa na chupa mbili za soda na pakiti mbili za njugu.
“Chukua’
Akanipa chupa moja ya soda na pakiti moja ya njugu.
“Asante”
Onesho la sinema likaanza. Tukaitazama filamu ya Dk No mwanzo hadi mwisho. Mara kwa mara msichana huyo alikuwa akimshangilia James Bond kutokana na ujanja wake wa kipelelezi. Filamu ilipomalizika tukatoka.
“Si utanipeleka nyumbani?” msichana akaniuliza tulipokuwa nje ya jumba hilo.
“Kitabu kiko wapi?” nikamuuliza.
“Nilikisahau nyumbani, nitakwenda kukupa huko huko”
Nikaguna kimoyomoyo kwa vile ahadi yetu haikuwa hivyo. pikipiki yangu na kuiwasha.
“Panda twende” nikamwambia.
Msichana ambaye alionesha alikuwa mzoevu wa kupanda pikipiki alikaa nyuma yangu akauzungusha mkono wake kwenye tumbo langu. Nikatia gea na kuiondoa pikipiki.
“Unaitwa nani?” Msichana huyo akaniuliza.
“Naitwa Amour na wewe unaitwa nani?”
“Naitwa Zena, unaishi wapi?”
“Ninaishi Mabawa”
“Unafanya kazi wapi?”
“Nafanya kazi shirika la STC”
“Nimefurahi sana kukufahamu Amour”
“Na mimi pia nimefurahi kukufahamu”
Tukaendelea kuzungumza hili na lile mpaka tukafika Mikanjuni. Safari hii alinifikisha hadi katika nyumba aliyokuwa anaishi. Lilikuwa jumba zuri la kifahari. Ingawa eneo hilo lilikuwa giza, jumba hilo lilikuwa linawaka taa ya umeme.
“Mimi naishi hapa” Msichana akaniambia huku akishuka kwenye pikipiki.
Nilikuwa nikilitupia macho lile jumba, nikataka kumuuliza alikuwa amepangisha chumba au alikuwa akiishi kwao. lakini nilishindwa kumuuliza ili asione ninayachunguza maisha yake.
“Nimepaona” nikamjibu.
“Karibu ndani” akaniambia.
“Asante”
“Karibu” Msichana akanisisitizia.
“Hapa panatosha” nikamwambia nikiwa nimekaa kwenye pikipiki yangu.
“Unataka uishie nje, si vizuri. Tuingie ndani. Ninaishi peke yangu tu usiogope”
“Unaishi peke yako humu ndani?” nikamuuliza.
“Nimejenga mwenyewe kutokana na biashara zangu na ninaishi mwenyewe. Msichana aliniambia huku akifungua geti.
“Karibu”CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
Kwa jinsi alivyokuwa akinibembeleza ilibidi nishuke kwenye pikipiki. Niliposhuka tu msihana aliishika pikipiki yangu akaikokokota na kuiingiza ndani, nikawa namfuata nyuma.
Tulipoingia ndani msichana aliiegesha pikipiki kando ya mti mkubwa uliokuwa umeota katika ua wa jumba hilo. Aliiacha pikipiki akaenda kufunga geti.
“Karibu” akaniambia huku akitangulia kwenda kwenye mlango wa kuingilia kwenye jumba hilo. Nikamfuata.
Alifungua mlango akanikaribisha tena, tukaingia ndani. Tulitokea kwenye sebule pana iliyokuwa na makochi ya chini chini ambayo hutumiwa zaidi na watu wenye asili ya kiarabu. Ilikuwa sebule iliyonakishiwa na kupendeza.
“Karibu ukae” akaniambia.
Nikaa kaa kwenye kochi mojawapo.
“Nikuletee kinywaji gani, cha moto au cha baridi” akaniuliza.
“Hapana, sihitaji kinywaji chochote” nikamwambia.
Msichana akanitazama na kukunja uso kisha akaondoka hapo sebuleni. Nikajua kuwa amekwenda kunichukulia kitabu changu ili niondoke.
Baadaye kidogo akarudi. Alikuwa ameshika chano kilichokuwa na kijibiika kidogo na vikombe viwili vya kahawa. Chano hicho pia kilikuwa na kisahani kilichokuwa na tende.
Akakiweka chini mbele yangu.
Yeye mwenyewe alikuwa amevua baibui na kubaki na dera la mikono mirefu lililoziba kabisa miguu yake. Dera hilo lilikuwa limedariziwa nyuzi zilizokuwa zikimemeta kama hariri.
Pia alikuwa ameiondoa hijabu na badala yake alijitanda mtandio mwepesi uliokuwa unaonya. Uso wake uliweza kuonekana vizuri. Nywele zake ndefu za maboga kama za kiarabu zilikuwa zimefikia kwenye mabega yake.
“Karibu” akaniambia na kuongeza.
“Kunywa kahawa kidogo. Kahawa inachangamsha”
Sikupenda kuikataa ile takirima ingawa nilimwambia sikuhitaji kinywaji chochote.
Msichana akaketi chini karibu yangu akachukua kile kibirika na kunimiminia kahawa kisha akajimiminia na yeye.
Alichukua kikombe hicho akaionja kahawa kisha akakirudisha chini na kuokota tende moja na kuitia midomoni.
Na mimi niliokota tende kwanza, nikaitia midomoni kisha nikainua kikombe cha kahawa kusukumizia.
“Wewe una asili ya kiarabu?” nikamuuliza.
“Nimechanganya uarabu na uswahili”
‘Muarabu ni baba yako au mama yako?”
“Baba yangu ni muarabu wa Ajemi, mama yangu ndio amechanganya. Zamani tulikuwa tunaishi Zanzibar”
“Sasa wazazi wako wako wapi?” nikamuuliza baada ya kutoa kokwa ya tende mdomoni.
“Iweke hapo kwenye sinia” aliniambia akinionesha kile chano.
Nikaiweka ile kokwa kwenye chano hicho kisha nikaokota tende nyingine.
“Baba yangu yuko Zanzibar na mama yangu yuko Ajemi” akaniambia.
“Kwa hiyo wewe unaishi hapa peke yako?” nikamuuliza.
“Ninaishi peke yangu” Msichana akanikubalia kwa haraka.
“Uliniambia hii nyumba uliijenga mwenyewe kwa biashara zako, unashughulika na biashara gani?”
“Ninauza madini”
“Madini gani?”
“Madini ya kila aina”
“Unayapata wapi?”
“Baba yangu ananiletea kutoka Zanzibar”
“Yeye anayapata wapi?”
Msichana akabetua mabega yake.
“Sijui anayapata wapi”
“Ninavyojua mimi Zanzibar hakuna madini”
“Hayatoki Zanzibar, anayapata kutoka nje ya Zanzibar lakini sio Afrika ila mahali penyewe sipafahamu na hajawahi kuniambia”
“Ndiyo yamekuwezesha kujenga nyumba hii?”
“Ndiyo”
“Hongera sana. Sasa kwanini unaishi peke yako?”
“Sijapata mwenzangu wa kuishi naye”
Kahawa aliyonitilia kwenye kikombe nikaimaliza. Akataka kuniwekea nyingine, nikamwambia.
“Imetosha, asante sana”
“Ngoja nikakuchukulie kitabu chako” akaniambia huku akiinuka. Macho yangu yalimsindikiza hadi alipotoka mlangoni.
Kusema kweli baada ya msichana huyo kuondoka sikujua tena kilichotokea kwani usingizi ulinipitia hapo hapo bila kutarajia. Nikalala fofofo.
Nilipokuja kuzinduka nilijikuta nimekaa peke yangu mahali pale pale nilipokuwa. Kile chano cha kahawa na tende kilikuwa kimeondolewa. Kwa kutaka kujua ilikuwa ni saa ngapi nilitazama saa yangu ya mkononi, nikaona ilikuwa saa tisa kasorobo ya usiku.
Nikashituka sana kuona nilikuwa nimelala nyumbani kwa msichana huyo hadi muda huo. Nikataka kuinuka ili nimuite mwenyeji wangu ambaye sikujua alikuwa wapi.
Kabla ya kuinuka nikaisikia sauti yake ikitoke nje ya dirisha la kile chumba. Kisha nilisikia sauti nyingine ya kiume ikijibishana naye. Sauti ile ya kiume ikanishitua kwa sababu yule mwanamke aliniambia alikuwa akiishi peke yake mle ndani.
Nikapenua pazia nakuchungulia uani. Nikaiona pikipiki yangu niliyokuwa nimeiegesha kando ya mti. Mbele ya pikipiki niliona kitu kama kisima cha maji. Wakati tunaingia mle ndani kisima hicho sikukiona.
Maji yaliyokuwa kwenye kisima hicho yalikuwa mekundu kama damu na yalikuwa yakitoa harufu ya damu ya binaadamu mpaka nikahisi yalikuwa ni damu kweli.
Ndani ya kile kisima kulikuwa na watu wawili waliokuwa wakioga na ndio waliokuwa wakizungumza. Mmoja akatoka na kusimama kando ya kisima hicho. Mara moja nikatambua kuwa ni yule mwenyeji wangu lakini safari hii alikuwa na umbile la kutisha sana.
Kwanza nywele zake zilikuwa nyingi na ndefu zilizoteremka na kumfikia kiunoni. Zilikuwa nywele nyeupe kama mvi za bi kikongwe. Yeye mwenyewe ngozi yake ilibadilika na kuwa nyeupe kama ya mzungu. Macho yake yalikuwa ya kijivu na mboni zake zilikuwa nyembamba na zilizosimama kama mboni za paka.
Bado alikuwa ameota manyoya marefu mwili mzima. Nikagundua kwenye miguu yake hakuwa na vitanga vya miguu kama walivyo binaadamu wote bali alikuwa na kwato nyeusi kama za farasi au punda. Hakuwa amevaa chochote. Alikuwa uchi wa mnyama!
Mwenzake naye akatoka kwenye kisima. Yeye alikuwa mwanaume lakini alikuwa na umbile kama la yule msichana. Miguu yake pia ilikuwa na kwato.
Walikuwa wakizungumza kwa lugha ambayo sikuielewa. Kwa kweli nilishituka sana. Nikapata hofu na uoga mpaka mwili wangu ukawa unatetemeka.
Nikahisii kwamba yule msichana aliyenikarisha mle ndani hakuwa binaadamu bali alikuwa jini na pale alikuwa akizungumza na jini mwenzake.
Nikatengeza mawazo kwamba huenda msichana yule aliniingiza katika nyumba ile kwa hila ili wanidhuru kwani ile damu iliyokuwa kwenye kile kisima ilikuwa ni ya binaadamu kama mimi. Na bila shaka waliingizwa mle ndani na kuuawa kikatili.
Hapo ndipo nilipochanganyikiwa nikajua kwamba dakika zangu za kuishi zilikuwa zimekaribia kwisha.
CHANZO: https://deusdeditmahunda.blogspot.com/
“Nitatokaje humu ndani?” nikajiuliza.
Nililirudisha lile pazia. Nikaenda kwenye mlango na kutoka ukumbini. Ukumbi ulikuwa kiza. Sikuweza kuona kitu. Sikuelekea upande wa uani tulikoingilia, nikalekea mlango wa mbele. Nilitaka nitoka kwa kutumia mlango huo bila Zena na mwenzake kujua. Pikipiki yangu nilikuwa nimeshaisamehe.
Kwa muda ule pikipiki haikuwa na umuhimu kwangu, kilichokuwa muhimu illikuwa ni kujisalimisha roho yangu. Nilijiambia kama nitafanikiwa kutoka mle ndani na kukimbia nitakuwa nimeweza kujisalimisha kuuawa.
Nikawa natembea haraka haraka ili niwahi kutoka kabla sijagunduliwa. Kwa sababu ukumbi ulikuwa kiza nikakumba kitu kama meza iliyokuwa imewekwa ukumbini. Niliikumba kwa nguvu hadi ikatoa mlio wa kuburuzika.
Hapo hapo nikasikia sauti ya Zena ikiuliza.
“Amour unanitafuta?”
Sikujibu kitu, nikaikwepa ile meza na kundelea kwenda mbele sasa kwa haraka zaidi.
“Amour unaondoka?” Sauti ya Zena ikasikika tena.
Sikujibu. Nikaendelea kwenda. Sasa nilikuwa nahema kwa hofu. Mdomo nilikuwa nimeuacha wazi huku mikono yangu ikiwa mbele ili niweze kuugusa mlango nitakapoufikia.
“Amour usiondoke, nisubiri”
Sauti ya Zena ilizidi kunichanganya. Ndani ya moyo wangu nikawa naomba Mungu anisalimishe.
“Yarabi nisitiri…Yarabi nisitiri…”
Mara moja nikaufikia mlango. Nikawa naupapasa haraka haraka mpaka nikaushika ufunguo uliokuwa umeachwa kwenye kitasa, nikaufungua kisha nikauvuta mlango. Mlango haukufunguka.
INAENDELEA

0 Comments