Ticker

6/recent/ticker-posts

Ad Code

Responsive Advertisement

Simulizi: Beyond Love (Zaidi Ya mapenzi) Sehemu ya Ishirini Na Nne (24)



Hakutaka kusikia kuhusu wazazi wake, aliamua kuishi maisha yake peke yake, huku mtu muhimu aliyekuwa mbele yake akiwa ni Tom pekee.

Siku moja Ramsey alimtoa Mariam na kwenda naye ufukweni, hiyo ni baada ya kumweleza alikuwa na mazungumzo ya muhimu sana ambayo yalihitaji sehemu iliyotulia ili aweze kumweleza vizuri jambo ambalo Mariam hakulipinga.

Wakiwa katika hoteli moja, ufukweni mwa Bahari ya Hindi, Mariam ndiye aliyeanzisha mazungumzo baada ya kuona Ramsey hazungumzi chochote.

“Enheee Ramsey, ulisema una mazungumzo muhimu na mimi, muda unazidi kwenda, naona ni bora ukaniambia.”

“Ni kweli, tena ni muhimu sana.”

“Nakusikiliza, bila shaka huu ndiyo muda muafaka.”

“Mariam nataka kukuambia jambo moja muhimu sana, muhimu kwako na kwangu, muhimu kwa maisha yako,” Ramsey alisema kwa sauti ya utulivu sana.

“Nakusikiliza Ramsey.”

“Nafikiri unakumbuka kuwa mimi ndiye niliyekuokota Morogoro na kukupeleka hospitalini kwa ajili ya matibabu!”

“Ndiyo nafahamu.”

“Pia mimi ndiye niliyekuleta Dar ba kukupeleka hadi hospitalini!”

“Ni kweli.”

“Kwamba mpaka sasa hivi mimi ndiye ninayegharamia mahitaji yote ya Tom na wewe.”

“Ndiyo!”

“Nimekufanyia mambo mengi sana ili kukufanya mwenye furaha!”

“Hilo halipingiki.”

“Unajua ni kwanini nimekufanyia yote haya?”

“Hilo litakuwa moyoni mwako.”

“Kipo kitu kilichonisukuma mimi kufanya yote hayo Mariam, kipo! Tangu nilipokuona siku ya kwanza, niliona kitu kwako Mariam, nakumbuka uliwahi kuniuliza sababu ya kukufanyia wema wote huu lakini nilikujibu jibu la uongo kwa sababu muda wa kukuambia haya ninayokuambia ulikuwa haujafika.

“Nisikilize kwa makini Mariam, wewe ni msichana mrembo sana, ambaye unahitaji matunzo, unatakiwa ukae mahali utulie ukila na kunywa kila unachokitaka. Hupaswi kuwa na huzuni wala mateso kama uliyonayo hivi sasa, hutakiwi kuwa na msiba mzito moyoni mwako kama ulionao sasa hivi. Urembo wako haufanani na matatizo uliyonayo. Mariam unatakiwa kubembelezwa!” Ramsey alipofika hapo alitulia kwa muda kisha akapeleka glasi yake ya maji ya matunda kinywani kabla ya kuanza tena kuzungumza.

“Mariam mimi nakupenda, tena nakupenda kwa mapenzi ya dhati kutoka moyoni mwangu, nipe nafasi nikuonyeshe raha za ulimwengu. Achana na yule mlemavu kule Muhimbili, kwanza inawezekana baada ya kupata fahamu akakufukuza, kwanini uumize moyo wako? Nipe nafasi nikuonyeshe ninavyokupenda Mariam,” Ramsey alizungumza kwa sauti ya upole sana, akiamini Mariam angemsikiliza.

“Umemaliza?” Mariam akamwuliza akivuta midomo.”

“Tayari...”

“Sikiliza....tena sikiliza kwa makini sana, hivyo vijimsaada vyako visiwe sababu ya kunitongoza. Mwili wangu una thamani sana, tena ni maalum kwa ajili ya mtu mmoja tu, Tom! Huyo ambaye kwako wewe umeona ni mlemavu lakini kwangu ni mwanaume, tena mume wa ndoa. Kama umechoka kunisaidia, acha! Sikulazimishi, lakini mwili wangu, sahau!” Mariam akasema kwa kujiamini sana.

Ramsey akavimba kwa hasira, hakuzungumza neno lolote zaidi ya kusimama na kuanza kupiga hatua moja baada ya nyingine akimwacha Mariam mwenyewe ufukweni.

Mariam akafikiria kwa haraka, akaona giza nene lililokuwa mbele yake, kumuacha Ramsey aondoke kulimaanisha yeye kutokuwa na mahali pa kulala kuanzia siku hiyo, pia asingeweza kumuhudumia Tom wake, achilia chakula chake yeye mwenyewe.

Mariam akaanza kulia. Ramsey aliendelea kutembea bila kugeuka nyuma, akiwa amedhamiria kabisa kuondoka na kumwacha Mariam pale ufukweni. Mariam akasimama na kuanza kumkimbilia Ramsey huku akiita jina lake kwa sauti kubwa.

“Ramseeeeeeeyyyy.....” Mariam aliita kwa sauti kubwa sana.

Ramsey akageuka nyuma, akasimama akiwa tayari kumsikiliza Mariam, hakuhitaji kitu kingine chochote zaidi ya penzi lake, vinginevyo aliamua kucha kusaidia tena Mariam.



Ni kama alikuwa amewahi kukimbia mbio za marathon, lakini haikuwa hivyo. Mariam hakuwahi kufanya mazoezi ya riadha hata mara moja, lakini siku hiyo alikimbia kwa mwendo wa ajabu. Hata yeye alijishangaa.

Alimfikia Ramsey akiwa anahema kwa kasi ya ajabu, akasimama mbele yake huku akiwa ameyatoa macho yake kama alikuwa akikimbizwa na mnyama hatari. Ghafla macho yake yakaanza kupatwa na unyevunyevu, baadaye kidogo machozi yakaanza kumiminika machoni mwake.

“Nyamaza Mariam, nyamaza...kulia kwako hakutasaidia kitu kama...”

“Kama sitakuambia nakupenda pia...”

“Ndiyo Mariam, kwanini unataka kuutesa moyo wangu kiasi hiki? Ni nani ambaye angeweza kufanya yote haya kwa ajili yako? Ni mimi ninayekupenda pekee ndiye niwezaye kufanya mambo haya.

“Lakini sasa, unadhani unafanya vyema kufanyiwa yote haya kwa mapenzi halafu wewe ulipe mabaya? Angalia mara mbili Mariam,” Ramsey alikuwa akizungumza kwa sauti laini, taratibu na macho yake yakiwa yameganda usoni mwa Mariam aliyekuwa akilia wakati wote.

Mariam hakuzungumza kitu, alitulia kwa muda kabla ya kwenda kujilaza kifuani mwa Ramsey. Ramsey alisikia raha sana kusikia pumzi za Mariam zikitoka kwa shida akiwa amelala juu ya kifua chake.

“Najua unanipenda sana Ramsey, najua...nafahamu kwamba ulifanya yote yale kwa sababu ya mapenzi yako kwangu...lakini pia unatakiwa kufahamu kwamba sikuwa nafahamu haya mambo mpaka leo uliponiambia, sikujua kama ulikuwa na jambo hilo moyoni mwako.

“Nashukuru sana kwa kunipenda na kunipa nafasi ya kwanza moyoni mwako, lakini unatakiwa kufahamu kwamba moyo wangu una makovu, kama ni sumu nilipewa kali, yenye kuua na kukausha kabisa! Hali yangu siyo nzuri kihisia....

“Najisikia kumpenda mtu mmoja tu, Tom! Lakini wema unaonipa nashindwa kujua nitakulipa vipi? Najua ni kiasi gani unavyoumia juu ya penzi lako kwangu, lakini nitafanyaje?” Mariam aliongea kwa sauti iliyojaa kwikwi huku machozi yakimiminika mgongoni mwa Ramsey aliyekuwa kimya akimsikiliza kwa makini sana.

“Kipo kitu cha kufanya Mariam, kipo...”

“Nini?”

“Kunipenda!”

“Ingeweza kuwa rahisi kukupenda, lakini siyo kukupenda wewe tu, Ramsey hata mwanaume mwingine yeyote. Ni kweli wewe ni kijana mzuri sana unayevutia kwa kila kitu, lakini moyo wangu una sumu, hauwezi tena kumpenda mtu mwingine zaidi ya Tom.

“Tafadhali usiumizwe na kauli zangu, ni hisia za kweli zinazotoka moyoni mwangu, naomba uzipokee kama zilivyo, nakupenda kama kaka yangu lakini siyo kimapenzi.”

“Kama hunipendi Mariam?”

“Nakupenda sana, tena sana lakini siyo kimapenzi, labda kama utanisaidia katika hilo!”

“Kukusaidia nini?”

“Kukupenda!”

“Unamaanisha nini?”

“Nisaidie niweze kupenda tena, moyo wangu sijui una matatizo gani?”

“Una uhakika na kauli yako?”

“Ndiyo!”

“Kweli?”

“Ndiyo...mbona unaniuliza mara mbilimbili, kwani huniamini?”

“Nakuamini sana...”

“Sema nakupenda sana Ramsey!”

“Nakupenda sana Ramsey!”

“Hebu niangalie!” Ramsey akamwambia Mariam ambaye alijitoa kifuani mwake na kusimama mbele yake huku akiwa ameyatuliza macho yake kwa Ramsey.

Ramsey akatabasamu, Mariam naye akatabasamu pia.

“Unahisi nini?”

“Kukupenda!”

“Kwahiyo mimi sasa ni mpenzi wako siyo?”

“Ndiyo, lakini nitaomba msaada mwingine kutoka kwako!”

“Unahitaji kiasi gani cha pesa?”

“Siyo pesa Ramsey, sizungumzii pesa!”

“Bali nini?”

“Tom!”

“Tom? Ameingia vipi tena kwenye mazungumzo yetu?”

“Naomba uniruhusu niendelee kumsaidia mpaka atakapopona!”

“Akifa je?”

“Hiyo itakuwa mipango ya Mungu!”

“Ok, hakuna tatizo katika hilo.”

Wakasogeleana tena, wakakumbatiana kwa nguvu, wakaanza kupeana mvua ya mabusu motomoto. Wakafungua ukurasa wa mapenzi. Hapo sasa wakarudi tena ufukweni ambapo walicheza michezo ya kimahaba mpaka usiku waliporudi zao hotelini.

*******

Moyo wa Mariam ulikuwa na maumivu makali sana, alikubali machoni tu kuwa na Ramsey lakini moyoni hakuwa na hata chembe ya mapenzi kwake. Moyoni mwake kulikuwa na mtu mmoja, Tom. Hakuwahi na wala hakufikiria kuwa na mtu mwingine zaidi ya Tom.

Alikubali ili aweze kuendelea kupata misaada yake kwani asingeweza kumhudumia Tom akiwa hana fedha. Kumkubalia ulikuwa mtihani wa kwanza, lakini mtihani wa pili ambao ungekuwa mgumu zaidi kwake ni kufanya mapenzi na Ramsey.

Alijiapiza kukabiliana na hilo mpaka mwisho wa pumzi zake. Ni kweli hakuwa na mapenzi naye, lakini asingeshindwa kujifanya kuonyesha mapenzi yake kwa kila njia, lakini tatizo kubwa kwake likawa ni mapenzi, hakutaka kabisa kuruhusu mwili wake uguswe na mwanaume mwingine zaidi ya Tom wake.

Jioni walikuwa wanakula pamoja hotelini, Mariam akimlisha na kumbusu kila wakati, alionyesha kila dalili za wao kuwa wapenzi, ingawa Mariam alikuwa makini sana na kamera za waandishi wa habari hasa za waandishi wa magazeti ya udaku.

“Angalia bwana, haya maeneo siyo kabisa. Kuna mwandishi mmoja anaitwa Issa Mnally akituona tu, lazima atatupiga picha na utashangaa tumetoka kwenye gazeti la Risasi!”

“Issa Mnally?”

“Ndiyo...huyu ni mdaku balaa, hakuna asiyemjua hapa Bongo. Habari nyingi za Tom amekuwa akiziripoti yeye na kama siyo yeye basi ni Senchawa, hawa wadaku hawafai kabisa!”

“Usijali mpenzi wangu, tupo kwenye chimbo hapa hawawezi kutuona.”

“Lakini ni vyema tukichukua tahadhari.”

“Hakuna shida.”

Wakaendelea kula na kunywa kwa furaha hadi usiku kabisa, walipoamua kuondoka na kwenda vyumbani mwao kulala. Mariam aliingia chumbani kwake na Ramsey naye akaenda chumbani mwake. Muda mfupi baada ya Mariam kuingia chumbani kwake, simu ya mezani ikaita. Haraka akapokea akijua ni lazima angekuwa ni Ramsey.

“Vipi mpenzi wangu, si tumeachana muda huu tu,” Mariam alisema maneno hayo mara baada ya kupokea simu.

“Siyo shwari darling!”

“Kwanini?”

“Kuna baridi sana, siwezi kulala mwenyewe, nahitaji sana joto lako!”

“Lakini mbona bado mapema sana?”

“Mapema kupata joto lako? Mbona sikuelewi Mariam, naomba uje chumbani kwangu!”

“Sawa,” Mariam akajibu na kuamka haraka kisha akavaa na kwenda chumbani kwa Ramsey.

Hakutaka kumuudhi tena, lakini kikubwa ambacho kilikuwa akilini mwake ni kutomuachia kabisa mwili wake. Hilo alijihakikishia kabisa kwamba lilikuwa ndani ya uwezo wake. Akatoka nje, kisha akafunga mlango wake na kwenda chumbani kwa Ramsey.

“Karibu mpenzi wangu!”

“Ahsante sana!” Mariam akaingia na kwenda moja kwa moja kitandani.

Wakalala wakiwa wamekumbatiana. Katikati ya usiku, Mariam akiwa amelala fofofo, alisikia mikono laini ya Ramsey ikipita mwilini mwake. Mwanzoni alihisi alikuwa usingizini, lakini muda ulivyozidi kwenda ndivyo alivyogundua kwamba kila kilichokuwa kinatokea kilikuwa yakini!

Akashtuka zaidi alipogundua, Ramsey alikuwa ameshamvua nguo zake zote na alikuwa mtupu kabisa.

“Ramsey unataka kufanya nini?” Mariam akasema kwa ukali sana.

“Mbona hivyo mpenzi wangu? Kwani wewe ni nani wangu enheee? Sisi si ni wapenzi, sasa kuna ubaya gani kufanya mapenzi?”

“Ubaya upo!”

“Kivipi?”

“Hatujajuana vizuri Ramsey, lazima tupime kwanza kabla ya kuanza haya mambo!”

“Ninazo kondom!”

“Sipo tayari....kwanza huwa situmii kondom!”

“Mbona unakuwa hivyo?”

“Nooooo...haiwezekani Ramsey, naomba uelewe!” Mariam akajitoa kitandani kisha akavaa nguo zake haraka na kutoka nje, akarudi chumbani mwake.

*******

Hadi inafika saa moja kamili asubuhi, Mariam alikuwa hajafumba macho yake kulala. Alitumia usiku mzima kuwaza maisha yake. Hakuwa tayari kumsaliti Tom wake, lakini pia hakuwa tayari kupoteza misaada ya Ramsey.

“Nitafanya nini mimi jamani? Mbona dunia inanigeuka kiasi hiki?” Mariam akawaza akilia.

Usiku mzima alikuwa hapokei simu ya Ramsey, baadaye akaamua kuweka mkonge wa simu pembeni ili kukwepa usumbufu. Alipoanza kupiga simu yake ya mkononi akaamua kuizima kabisa. Akili yake ikawa ni juu ya mpenzi wake wa moyo wa Tom.

Akiwa anaendelea kuwaza, ghafla akasikia mlango ukigongwa, akaenda kufungua. Akakutana na Ramsey akiwa amebeba begi lake. Akamwangalia Mariam akionekana kuwa na chuki za wazi. Akaingiza mkono mfukoni kisha akatoa burungutu la pesa na kumrushia kitandani, baada ya hapo akaingiza tena mkono katika mfuko wa shati kisha akatoa karatasi iliyokuwa na maandishi na kumpatia.

“Maisha mema!” Ramsey akasema kisha akafunga mlango kwa nguvu na kuondoka.

Haraka Mariam akafungua lile karatasi kisha akaanza kusoma kwa makini. Ilikuwa imeandika hivi; Nilikupenda kwa mapenzi ya dhati, nikakupa kila kitu lakini hukuthamini penzi langu. Nilikuwa tayari kukupa kila aina ya msaada uliotaka, lakini ukanilipa machungu.

Kuondoka chumbani kwangu usiku, kumenipa taswira kwamba hunipendi, unanionea kinyaa na ni mwaume ambaye sina uwezo wa kuwa na wewe. Ahsante sana kwa hilo, naomba na mimi niishie hapa.

Nimekuachia hizo lakini tano, nikusaidie katika mwanzo mpya wa maisha yako, maana najua ni kiasi gani utakuwa katika hali ngumu. Maisha ya hapo hotelini hutayaweza, hivyo nakushauri rudi nyumbani, ukawaangukie wazazi wako, uwaombe radhi.

Hata hivyo, bado nakupenda, siku ukiona utaweza kuwa na mimi, basi nipigie simu kwa namba zangu nilizokuachia. Sina kingine zaidi ya kuendelea kukuambia nakupenda na sitaacha kukupenda. Huyo Tom ni msumari wako wa milele, lakini mwenye uamuzi wa kuutoa huo msumari ni wewe mwenyewe.

Akupendaye kwa dhati,

Ramsey.

Mariam alirudia kusoma yale maneno zaidi ya mara kumi na hakuna sehemu hata moja iliyobadilika! Yalikuwa maneno makali sana ambayo yaliuchoma moyo wake. Hakuwa na kitu kingine cha kufanya zaidi ya kulia. Mariam akaanza kulia.

“Lakini nimekumbuka, ipo njia ya kuepukana na haya matatizo yote, ipo...hapa natakiwa kufa tu, hakuna kingine. Nife, niende zangu kwa Mungu, yeye mwenyewe anajua kwanini nimeamua kwenda kwake mapema kabla yeye hajaniita. Nataka kufa, tena leo hii hii!” Mariam akasema maneno hayo kwa sauti ya chini huku akitokwa na machozi.



CHUMBA kilikuwa kichungu kwake, asingeweza kuendelea kuishi pale bila msaada wowote. Bado akilini mwake hakuweza kujua nini cha kufanya tofauti na uamuzi wa kufa ambao aliuona kuwa ni bora zaidi.

“Nitakuwa nimepotea kabisa, sitaonana na mtu yeyote tena, nitakuwa nimepumzika kwa Mungu, mateso na shida zote yatakuwa yameisha. Kwanini niendelee kuishi kwa shida kiasi hiki? Wazazi wangu hawanitaki, Ramsey amenikimbia, Tom naye ni mgonjwa, pamoja na kwamba nampenda lakini bado anaweza akapona na akaendelea kuwa na msimamo wake ule ule, sasa kwanini nijitese? Kwanini niendelee kuteseka?

“Ni bora kufa, ni bora niondoke, hiyo ndiyo inaweza kuwa salama yangu, sina kitu kingine cha kufanya zaidi ya hivyo, acha nikapumzike,” Mariam akawaza akilini mwake huku machozi mithili ya maji yakimiminika machoni mwake.

Alitulia kwa muda mrefu pale kitandani, akiendelea kulia, muda ukizidi kwenda. Alitumia muda mwingi akiwaza maisha yake, hapo ndipo alipokumbuka kwamba hakuwahi kufurahi kabisa katika maisha yake ya kimapenzi.

Mchana mzima alikuwa akilia, hakukumbuka kula siku hiyo, usiku akaamua kwenda kununua sumu ya panya ili ajitoe uhai. Alidhamiria kufa, baada ya kununua sumu yake ya panya, alirudi hotelini na kutulia kwa muda akijaribu kufikiria maisha yake baada ya kifo chake.

“Hakuna kitakachoharibika, sina thamani ya maisha hapa duniani, naamini kwa Mungu kuna afadhali, najua nitakuwa na dhambi ya kujiua lakini Mungu mwenyewe naamini atanisamehe kutokana na haya mateso niliyonayo. Sijapenda kufa, ila nalazimika kukimbia matatizo ya hapa duniani, siwezi kukabiliana nayo, yamenishinda,” Mariam alijisemea moyoni.

Mariam alibadilika sana, hakuona thamani yake tena duniani, aliamini kwa kufa pekee ndiyo angeweza kupumzika na kuepukana na matatizo anayoyapata. Alichokifanya ni kuchukua mkonge wa simu, kisha akabonyeza namba za hotelini.

“Hotelini!”

“Ndiyo habari yako?”

“Salama.”

“Naomba kukusikiliza!”

“Nahitaji soda ya badiri sana!”

“Soda gani?”

“Yoyote isiyo na gesi sana!”

“Soda gani sasa?”

“Yoyote.”

“Upo chumba namba ngapi?”

“206.”

“Ghorofa ya ngapi?”

“Tatu.”

“Ok! Baada ya muda mfupi utaletewa.”

Mariam akachukua kalamu na karatasi akaanza kuandika ujumbe ambao ungewasaidia wahudumu kufahamu alikuwa ni nani na ndugu zake ni akina nani. Ulikuwa ujumbe unaosikitisha sana, muda wote aliokuwa akiandika alikuwa akilia machozi.

Ujumbe huo, ulisomeka hivi; ‘Nimeamua kufa ili kukwepa fedheha ninayoipata hapa duniani, naamini kifo pekee ndicho kitakachoweza kunitenganisha na kero na matatizo yote ninayoyapata hapa duniani. Nimeteseka vya kutosha, ninayempenda hanipendi, wazazi wangu wamenifukuza nyumbani, sina msaada wowote.

Sioni thamani wala faida yangu duniani, ni heri nife tu, ni wengi wananifahamu, mimi ni mke halali wa Tom ambaye wengi wamekuwa wakimfahamu kwa jina la Papaa Bill. Naamini kwa utambulisho huu utawarahisishia kuwapa taarifa wazazi wangu ambao watakuja kuuchukua mwili wangu na kuuzika.

Naamini kifo ni safari ya kwenda mbinguni, hivyo basi ni imani yangu kwamba siku moja tutakutana katika enzi yake Mungu wa mbinguni. Kwaherini ya kuonana.

Mariam.’

Alipomaliza kuandika ujumbe huo, alirudia kuusoma mara mbili mbili huku akilia. Akiwa anarudia kwa mara ya tatu, mlango wa chumba chake ukagongwa, alijua lazima alikuwa mhudumu. Haraka akafuta machozi yake kisha akaficha karatasi yake, akasogea mlangoni, akafungua mlango.

“Vipi sister?”

“Salama.”

“Mbona kama ulikuwa unalia? Kuna tatizo?” mhudumu akamwuliza.

“Hapana macho yananisumbua kaka yangu!” Mariam akadanganya.

“Pole sana!”

“Ahsante!” Wakati Mariam anajibu hivyo, alijikuta machozi yakimwagika usoni mwake kama maji yanayotiririka kutoka mferejini.

“Mh! Dada inaonekana una tatizo, lakini unajaribu kunificha, kwanini usiseme ukweli, naweza kukusaidia mawazo,” yule mhudumu akamsisitizia.

“Kaka nimeshakuambia macho yananisumbua lakini kwanini unazidi kuning’ang’aniza niwe na matatizo? Kwanza siyo kazi yako kujua matatizo yangu, tafadhali fungua soda uondoke!” Mariam aliongea kwa ukali sana, alionyesha kudhamiria alichokuwa akizungumza.

Yule mhudumu hakuwa na maneno mengi, akafungua soda kisha akaondoka zake. Mariam akaimimina soda kwenye glasi kisha akachanganya na ile sumu aliyoinunua, baada ya hapo akaanza kuikoroga kwa pamoja. Akasimama mwili ukimsisimka, kisha akaiangalia ile glasi, baada ya hapo akaielekeza mdomoni mwake.

“Eeeh baba naomba upokee roho yangu,” Mariam akasema maneno hayo glasi ikikaribia kufika kinywani.

Aliamua kufa!

******

Nyumba ilipoteza amani, furaha yao haikuwepo tena, walishamtafuta Mariam hadi wamechoka na hawakufanikiwa kumpata. Mama yake Mariam alikuwa akilia muda wote.

Kila walipoenda Muhimbili kumtafuta Mariam, waliambiwa kuwa huwa anakwenda mara moja moja, jibu ambalo lilizidi kuwachanganya. Walishaamua kumchukua mtoto wao ili wafanye mazungumzo na kumuweka sawa, lakini waliumia sana walipomtafuta bila mafanikio.

“Lakini nina wazo mume wangu,” mama yake Mariam akamwambia mumewe.

“Wazo gani mama Mariam?”

“Tunahangaika na tutahangaika sana, lakini ipo njia moja tu tunayopaswa kuitumia!”

“Ipi?”

“Tumesahau kumuomba Mungu, nakuhakikishia kama tukimshirikisha yeye kila kitu kitakuwa sawa, ni lazima tuwe karibu na Mungu baba Mariam.”

“Ni kweli, tumefanya kosa kubwa sana mke wangu, hatuna haja ya kupoteza muda, tunatakiwa kuanza kusali sasa hivi.”

“Haya simama tuombe mume wangu.” Wote wakasimama, kisha wakashikana mikono, mama Marim akaongoza sala.

Walianza na nyimbo za kuabudu, ambazo waliimba kwa robo saa kabla ya kuingia kwenye maombi yaliyowachukua saa nzima! Kila mmoja alikuwa akimuomba Mungu wake, amuepushie Mariam kwenye mateso na shida zote na hata kama alikuwa na mawazo mabaya ambayo yalikuwa yanateka akili yake, yashindwe!

“Katika jina la Yesu Kristo wa Nazareth tumeomba na kushukuru...”

“Aaamen...” baba Mariam akaitikia.

“Mungu ndiyo kila kitu mume wangu, nakuhakikishia tutaona majibu yake, Mungu wetu siyo mwongo, maana yeye mwenyewe tumuombe naye atatujibu, hawezi kutoa ahadi ya uongo, lazima atatujibu tu, lazima.”

“Ni kweli mke wangu, twende chumbani tukalale.”

Wakaongozana hadi chumbani kulala, angalau sasa mioyo yao ilikuwa na amani baada ya kufanya maombi.

*******

“Acha!” Mariam alisikia sauti hiyo ambayo hakuelewa ilitokea wapi.

Alihisi alikuwa ndotoni, hivyo akapuuza, akaamua kuipandisha glasi yake hadi kinywani, akiwa anataka kuanza kunywa, ghafla akahisi mkono wake ukitetemeka kwa kasi, ukazidisha kasi hadi glasi ikaanguka chini.

Mariam hakuelewa kilichotokea, chumba kizima kikawa kinanuka harufu ya sumu ya panya. Ilikuwa harufu mbaya sana, Mariam alichanganyikiwa, hakujua kwanini jambo lile lilitokea, alichoamua kwa muda huo, ilikuwa ni kurudi tena dukani na kununua sumu nyingine ili aweze kuendelea na zoezi lake.

Akiwa ndiyo anataka kufungua mlango ili atoke nje, akashangaa miguu yake inakuwa mizito, sauti nyingine tena ikasisika, tena kwa sauti ya juu na ya msisitizo zaidi; “Wewe ni msichana mzuri sana, unayevutia na ambaye una mpenzi mzuri sana, siyo kweli kwamba baada ya kufa utakuwa umekimbia matatizo, achana na mawazo hayo.

“Unachotakiwa kufanya sasa ni kwenda kwa wazazi wako, uwaangukie na kuwaomba radhi, bado una nafasi ya kuendelea kuishi. Mariam badili uamuzi wako...” Mariam alizidi kuchanganyikiwa, hakuweza kuelewa ilikuwa sauti ya nani na wapi ilipotokea.

Katika hali ambayo hata yeye mwenyewe hakuitegemea, alijikuta akiahirisha kujiua, moyo wake ukawa umekunjamana na kuhisi uhitaji wa radhi za wazazi wake.

“Lazima nirudi nyumbani, lazima tena usiku huu huu wa leo,” Mariam akawaza na kuchukua begi lake dogo lililokuwa na nguo zake chache kisha akafunga chumba na kushuka hadi chini ambapo aliingia kwenye taxi.

“Wapi sister?”

“Jeti, Lumo!”

“Poa.” Dereva akawasha gari na safari ya kwenda nyumbani kwa wazazi wake ikaanza.

Kwa kuwa hakukuwa na foleni, dakika ishirini zilitosha kabisa kutoka Magomeni Mapipa katika hoteli aliyokuwa akiishi hadi Jeti, Lumo. Tayari ilikuwa imeshafika saa saba kasoro za usiku. Kwa bahati nzuri, nyumba yao ilikuwa barabarani, hivyo alimlipa dereva akashuka na kuanza kugonga geti.

Muda mfupi baadaye baba yake akafika getini.

“Nani usiku wote huu?”

“Ni mimi baba!”

“Mariam!”

“Ndiyo!”

“Karibu mwanangu, ngoja nikufungulie!” Mlango ukafunguliwa na Mariam akaingia.

Mapokezi aliyokutana nayo hakuyategemea kabisa, baba yake akampokea begi na kuingia naye hadi ndani ambapo alimwita mama Mariam ambaye hakuamini kilichokuwa mbele yake.

INAENDELEA

Post a Comment

0 Comments