Ticker

6/recent/ticker-posts

Ad Code

Responsive Advertisement

Simulizi: beyond Love (Zaidi ya Mapenzi) Sehemu Ya Ishirini Na Moja (21)



 “Mariam!”

“Mariam siyo mwenzagu, siwezi kuishi na mwanamke kama yeye, mwenzangu ni Mayasa! Huyu mnayemuona hapa ndiye mke wangu ambaye ninampenda kuliko kitu chochote katika maisha yangu, sihitaji kusikia habari nyingine tofauti na Mayasa wangu. Nawaomba mtoke kwangu!” Tom alisema maneno hayo huku akibamiza geti na kufunga kwa komeo.

Mama Mariam na mumewe wakabaki wanaangaliana, machozi machoni mwao ndiyo faraja pekee ambayo ingewasaidia kwa wakati huo. Wakaangaliana kwa uchungu, wakasogeleana kisha wakakumbatiana na kuanza kulia. Walishindwa kuelewa ni mkosi wa aina gani uliompata binti yao.

“Binti yetu wa pekee Mariam, kwanini anapatwa na balaa kubwa kiasi hiki, kwanini lakini?!” Baba yake na Mariam alisema huku machozi yakilowanisha shingo ya mkewe aliyekuwa amelala kifuani mwake.

“Lakini naamini siyo Tom, yupo aliye nyuma ya akili zake, ni shetani pekee ndiye anayemsumbua!”

“Mungu adhihirishe utukufu wake!”

“Amen!” Wakatoka kwa pamoja wakiwa wameshikana mikono, wakalifuata gari lao, wakaingia na kuondoka taratibu. Msaada pekee uliobakia ulikuwa ni Mungu pekee.



Haikuwa rahisi kugundua kwamba kwa muda wote wa robo saa Dk. Joseph Kisanga aliuokuwa akiutumia kuzungumza na Mariam, alikuwa akizungumza mwenyewe! Dk. Kisanga alikuwa akizungumza kwa sauti ya taratibu, ukimya wa hali ya juu ukiwa umetawala na akihakikisha kwamba Mariama anarejea katika hali yake ya kawaida, lakini kumbe akili ya Mariam haikuwa pale!

Mapenzi yake kwa Tom ndiyo yaliyokuwa akilini mwake na siyo ushauri wa Dk. Kisanga ambao kwake ulikuwa sawa na porojo zisizo na maana yoyote. Kilikuwa chumba kimya, chenye mwanga hafifu, lakini kilichokuwa na hewa ya kutosha iliyozalishwa kwa mashine maalumu ya kisasa.

Mariam akiwa ameketi kwa mtindo wa kutazamana na Dk. Kisanga ambaye ni Mtaalamu wa Magonjwa ya Afya ya Akili na Mshauri wa Mambo ya Saikolojia na Maisha katika ofisi yake hii ambayo siku zote huwa ni tulivu sana akiwashauri watu wengi hasa waliokata tamaa. Ni Dk. Kisanga ndiye aliyemsaidia mzee Mallya, mfanyabiashara wa maarufu jijini Dar es Salaam, aliyetaka kujiua baada ya bohari lake la kuhifadhia mizigo muhimu kuungua na kumsababishia hasara ya mamilioni ya pesa!

Dk. Kisanga pia ndiye aliyemshauri msanii maarufu Bisongi ambaye aliathiriwa na dawa za kulevya lakini baada ya kuzungumza naye akimpa ushauri, akakubali kuacha na kubadilika kabisa! Naam. Dk. Kisanga ni mshauri maarufu ambaye amejizolea umaarufu mkubwa sana katika kutoa ushauri na kubadilisha maisha ya watu!

Hali ilikuwa tofauti sana kwa upande wa Mariam. Ilimchukua muda mrefu sana Dk. Kisanga kugundua kwamba muda wote huo alikuwa akizungumza peke yake.

“Mariam bila shaka tupo pamoja!” Dk. Kisanga akasema akimtizama Mariam usoni.

Mariam alikuwa kimya.

“Mariam...Mariam...we, Mariam...!” Dk. Kisanga akamwita kwa mara nyingine.

“Abee Dokta!”

“Mbona kama haupo hapa?”

“Tupo pamoja!”

“Unakumbuka nilizungumza nini mara ya mwisho?”

“Ndiyo!”

“Nilisemaje?”

“Ah! Dokta...nakuelewa vizuri sana!”

“Hapana lazima unisikilize vizuri Mariam, maisha yako yana thamani kubwa sana, hutakiwi kuyapa mapenzi kipaumbele zaidi kuliko maisha yako. Ni kweli mapenzi yana umuhimu mkubwa sana katika maisha yako lakini maisha yako yana thamani zaidi kuliko hayo mapenzi ambayo kwasasa yamekuwa tatizo kubwa kwako....” Dk. Kisanga aliendelea kumshauri Mariam kwa muda mrefu sana, akijitahidi kuzungumza naye kwa upole huku akihakikisha hali ya afya yake inarudi kuwa nzuri.

Mariam alionekana kumsikiliza Dk. Kisanga kwa makini sana, lakini kilichokuwa kikifanyika kilikuwa ni sawa na mchezo wa kuigiza, kwani alionekana kumsikiliza kwa umakini mkubwa lakini ndani ya moyo wake kulikuwa na kitu tofauti kabisa, moyoni mwa Mariam kulikuwa na maandishi makubwa yaliyosomeka; TOM! Ni yeye tu ndiye aliyekuwa wimbo moyoni mwake.

“Nimekuelewa Dk. Kisanga, nashukuru sana kwa kubadilisha maisha yangu, naamini sasa nimekuwa mpya na nitahakikisha natulia na kuishi maisha yangu bila matatizo wala kumuwaza Tom!” Mariam alisema kwa utulivu sana.

“Nimefurahi sana kusikia hivyo, amini kila kitu hupangwa na Mungu, hivyo ni wajibu kuhakikisha yeye anakuwa nguzo yako namba moja katika maisha yako. Nimefurahi sana Mariam, naona sasa unaweza kurudi nyumbani, hakikisha unafika hapa hospitalini kuonana na mimi kila mwezi hadi hali yako itakapokaa sawa.”

“Hakuna tabu Dokta, nashukuru sana!”

“Ahsante!”

Siku hiyo hiyo Mariam aliruhusiwa kurudi nyumbani akiwa ameonekana kuwa na nafuu kubwa. Wazazi wake walifika hospitalini na kumchukua kwenda naye nyumbani. Walikuwa na matumaini makubwa sana ya mwanao kuwa mpya, walimwamini sana Dk. Kisanga kutokana na uwezo wake mkubwa wa kushauri.

“Vipi mama, unajisikiaje sasa?!” Mama yake na Mariam alimwuliza akiwa anatizama usoni.

“Nina nafuu sasa mama!”

“Kweli?”

“Ndiyo mama.”

“Kwahiyo unataka kutuambia kwamba, sasa hivi hali yako imetengemaa.” Baba yake akadakia.

Mariam hakuwa na jibu!

Alitulia kimya bila kuzungumza chochote, ni jambo lililowashtua sana, hawakutarajia kama mwanawo angekaa kimya kwa muda mrefu kiasi kile, hasa kutokana na ukweli kwamba alikuwa akionyesha ushirikiano wa kutosha kuanzia mwanzoni.

“Vipi mbona umenyamaza?”

“Kuna tatizo baba!”

“Tatizo? Tatizo gani tena, si umesema unaendelea vizuri mwanangu?”

“Baba bado mawazo juu ya Tom yananisumbua na kuna jambo ambalo ni bora kama ningelifanya ili kuepukana na haya matatizo.”

“Ni nini?”

“Nahitaji kuwa mbali na Dar es Salaam, mbali na Tom, mbali na Mayasa, mbali na Vyombo vya Habari. Sihitaji kusikia wala kujua chochote kinachohusiana na Tom, nimechoshwa na mambo yake, nataka kutulia sasa.” Mariam akasema huku akilia kwa uchungu.

“Mwanangu huwezi kuwakimbia watu na hata kama unaweza, utawakimbia hadi lini?” Mama yake akadakia.

“Naweza mama, inawezekana kabisa kuwakimbia, sina jinsi zaidi ya kuondoka hapa Dar es Salaam!”

“Uende wapi sasa, uende wapi mwanangu?” Baba yake akadakia.

“Nitakwenda kwa bibi!”

“Yupi?”

“Wa Morogoro, acha niende nikapumzike Matombo!”

“Lini?”

“Kesho!”

“Mbona haraka sana?”

“Kesho ni siku nzuri sana kwangu, acha nianze kujiandaa!”

******

Mapenzi ya Tom na Mayasa yalizidi kupamba moto, Tom akawa hashikiki wala hakamatiki, kila kitu ilikuwa ni Mayasa. Tayari alishamkabidhi kila kitu katika maisha yake. Siri zote za kibiashara alikuwa ameshampa, namba zote za siri za kadi zake za benki Mayasa alikuwa anazijua.

Tom alikuwa amechanganyikiwa! Penzi la Mayasa lilimchanganya sana kiasi kwamba, alikuwa kama chizi mwenye akili timamu! Hata yeye mwenyewe alishindwa kuelewa ni mapenzi ya aina gani yaliyokuwa na nguvu kiasi kile. Hata hivyo alipuuza na kuamini kwamba alikuwa akimpenda sana Mayasa na hapakuwa na kitu kingine zaidi ya hicho.

Kwa upande wa Mayasa ilikuwa tofauti sana, hata siku moja hakuwahi kuhisi kumpenda Tom, hilo hata yeye mwenyewe alilikiri moyoni mwake. Kama alikuwa akimpenda, basi ni kwasababu ya pesa alizokuwa nazo. Aifurahia kuishi maisha mazuri, huku akisiamia miradi mbalimbali ya Tom iliyokuwa jijini Dar es Salaam na mikoani. Mayasa alikuwa ni kila kitu.

Mara nyingi alikuwa akikutana na marafiki zake na kuzungumza nao juu ya mambo mbalimbali ya kimaisha, siku zote walishindwa kuelewa ni kwanini Tom alimpenda kiasi kile. Siku zote aliishia kuwaambia kwamba mapenzi yake ya kweli ndiyo nguzo kubwa inayomfanya aendelee kufaidi maisha mazuri kwa Tom.

“Shosti sema ukweli bwana, lazima kuna kitu kipo nyuma ya pazia!” Rukia, mmoja wa marafiki zake alimwuliza Mayasa.

“Zaidi ya penzi langu, nini kingine?”

“Sema shoga yetu na sisi tuwatulize wapenzi wetu, haiwezekani Papaa Bill mpaka anafikia hatua ya kumuacha mkewe kama hakuna kitu kingine nyuma ya pazia!”

“Aaaah! Bwana...kikubwa ni utaalamu kitandani...haya inatosha sana shoga zangu, nendeni mkajifunze mambo ya kitandani....tehe...tehe...tehe....” Mayasa alisema akicheka.

“Lakini ni vizuri ukatuambia ukweli bwana!”

“Sina ukweli mwingine zaidi ya huo...” Mayasa akazidi kusisitiza. Hakuwa tayari kutoa siri zake za ndani kiasi kile.

“Sawa shoga yetu lakini nina ushauri mzuri sana kwa ajili yako. Huwezi kuwa mjinga kiasi hicho, Papaa Bill ana pesa nyingi sana na tayari anakuamini kwa kiasi kikubwa, lakini kama hutakuwa makini, unaweza kuachana naye ukawa huna kitu!”

“Kwahiyo?”

“Lazima ufanye kitu fulani, uwe tajiri!”

“Kitu gani hicho shosti yangu?”

“KAMA UNATAKA UTAJIRI WA TOM, HUNA BUDI KUWA NA ROHO NGUMU! UNACHOTAKIWA WEWE KUFANYA NI KUMPOTEZA!”

“Kumpoteza? Unamaanisha nini?”

“PAPAA BILL ANATAKIWA AFE!” Rukia akambia Mayasa ambaye alikuwa kimya sana akiwasikiliza.

Lilionekana wazo lililomchanganya sana akili yake, alitumia kimya kwa muda mrefu sana bila kuzungumza kitu, lakini baadaye akafungua kinywa chake na kuzungumza; “Wazo lako ni zuri sana, lakini sasa nitamuuaje? Na watu wakijua?” Mayasa akasema akitetemeka kwa hofu.

“Acha ujinga Mayasa, wewe ni mtoto wa mjini, kama ni kweli unataka utajiri wa Papaa Bill lazima umwondoe duniani, kama upo tayari sema nikupe njia nzuri ambazo zitakuwa katika mazingira ya usiri mkubwa, yeye afe akuache na utajiri wako!”

“Nipo tayari, nakusikiliza!”



Pamoja na ushauri wa kitaalamu alioupata kutoka kwa Dk. Joseph Kisanga, bado Mariam hakuwa katika hali yake ya kawaida. Hata yeye mwenyewe alijishangaa, hapakuwa na kitu kingine akilini mwake zaidi ya Tom. Aliamini pasingetokea mwanaume atakayempenda kwa mapenzi yake yote kama ilivyokuwa kwa Tom!

Kwake Tom alikuwa ni kila kitu! Kilichomuumiza zaidi ni majibu ya wazazi wake, kwamba Tom aliwafukuza nyumbani kwake mbele ya mwanamke wake Mayasa, hilo lilimuumiza sana.

Hakika isingewezekana Mariam, akavumilia kumuona Tom akiendelea kutesa na Mayasa wake, mbele ya macho yake. Pengine angejifungia ndani, lakini bado angeweza kumuona kwenye magazeti na hata kwenye luninga akiwa katika shughuli mbalimbali za kijamii.

Tom asingekwepeka kirahisi! Kitu pekee kilichokuwa mbele yake ilikuwa ni lazima Mariam aondoke Dar es Salaam, aende mbali, kijijini, nje ya mji kusipokuwa na Teknolojia ya Mawasiliano kabisa. Hiyo ndiyo njia pekee ambayo Mariam alikuwa nayo.

“Ni bora niondoke, nihame kabisa, sina sababu ya kuendelea kuteseka, pengine ilikuwa lazima niteseke, niumie, nikose amani, lakini haya yote naamini Mungu wa mbinguni anaona na atanipigania kwa kila hali ili niweze kushindana na haya majaribu,” Mariam alimwambia mama yake kwa uchungu, muda mfupi kabla ya kuingia kwenye basi, eneo la Kituo Kikuu cha Mabasi ya Mikoani, Ubungo jijini Dar es Salaam.

“Usijali mwanangu, hakuna lenye mwanzo linalokosa mwisho, safiri salama mama, msalimie bibi yako. Hakikisha unatuliza akili yako mama, huna sababu ya kumfikiria mtu mbaya kama Tom tena katika maisha yako, fungua ukurasa mpya sasa mwanangu!”

“Nashukuru sana mama!”

“Usijali, lakini bado kuna kitu ambacho ni muhimu sana ukifahamu mwanangu!”

“Kitu gani mama?”

“Maombi! Unatakiwa uombe sana mwanangu, msaada pekee kwa sasa ambao upo mbele yako ni kuwa karibu na Mungu! Ukiweza kutimiza hilo itakuwa rahisi sana kushinda majaribu yaliyopo mbele yako.”

“Ahsante sana mama kwa ushauri wako, nafikiri unanijua vizuri sana kuhusu hilo mama yangu, nitakuwa karibu sana na Mungu wangu kwa kila kitu mama...nakuahidi na itakuwa hivyo kweli!”

“Nimefurahi sana, nakutakia safari njema!”

“Ahsante sana mama!”

“Halafu kitu kingine mwanangu, lazima ujue kwamba wewe bado ni mzuri sana, naamini kuna wanaume wengi ambao wanahitaji angalau kunywa soda na wewe, kwahiyo huna haja ya kuhuzunika sana!” Mama yake Mariam alisema akitabasamu.

Mariam naye akatabasamu, tabasamu la ushindi! Ulikuwa ushindi mkubwa sana kwa mama yake na Mariam, tangu alipoamka asubuhi, hakuwahi kumuona mwanaye akitabasamu, lakini tabasamu lake la muda ule, tena la ghafla lilikuwa faraja kubwa sana kwa mama Mariam, sasa alikuwa ana imani kwamba ufumbuzi umepatikana.

“Nafikiri umenielewa mwanangu!” Tabasamu la mama yake na Mariam, sasa liliongezeka.

“Mama, kwa utani na wewe!!!”

“Siyo utani mwanangu, wewe ni binti yangu na sina sababu ya kukutania, ninachokuambia ni kitu cha ukweli ambacho hata wewe utakidhibitisha, kama utaamua kutulia!”

“Ahsante mama, ahsante sana mama yangu kwa kuona uzuri wangu, lakini uzuri huu mama, ulikuwa kwa ajili ya Tom!”

“Tom?!” Mama Mariam akauliza akiwa ameukunja uso wake.

“Ndiyo mama, Tom!”

“Ndiyo hakutaki sasa mwanangu!”

“Najua siyo yeye!”

“Ni nani?”

“Shetani!”

“Hata kama ni shetani, ndiyo ampe nafasi kubwa kiasi kile? Wakati mwingine shetani huwa anakaribishwa na mtu mwenyewe, na ndivyo alivyofanya Tom, yeye ameamua kumkaribisha shetani, unafikiri kwanini asimchezee kama yeye mwenyewe amemruhusu?”

“Usiseme hivyo mama!”

“Kumbe niseme nini Mariam, niseme nini?”

“Tunatakiwa kumuombea, naamini kwa kufanya hivyo siku moja atabadilika, niamini mama!”

Mama Mariam hakujibu kitu zaidi ya kumtulizia macho mwanaye, macho ambayo hayakuweza kuficha hasira na chuki za wazi alizokuwa nazo dhidi ya Tom.

“Naomba kukuuliza kitu mama!”

“Uliza!”

“Unamwamini Mungu?”

“Ndiyo, hata yeye anajua hilo!”

“Vizuri, nina swali lingine!”

“Uliza!”

“Kuna mahali popote ambapo Mungu amewahi kushindwa?”

“Hapana, yeye ni mshindi siku zote!”

“Basi ataendelea kuwa mshindi hata katika hili linalonisumbua na kunitesa mama!”

“Aaaamen!”

“Kwahiyo bado naendelea kukuomba umuombee!”

“Nitamuombea!”

“Nimefurahi kusikia hivyo, nimefurahi pia kwa wewe kuwa upande wangu. Nakupenda sana mama...nakupenda sana!”

“Nakupenda pia mwanangu mpenzi, nakutakia safari njema!”

“Ahsante mama!” Baada ya hapo mama Mariam aliondoka kwani dakika moja tu, baadaye basi liliondoka kituoni na safari ya kwenda Morogoro ikaanza.

INAENDELEA

Post a Comment

0 Comments