Ticker

6/recent/ticker-posts

Ad Code

Responsive Advertisement

Simulizi: Beyond Love (Zaidi Ya Mapenzi) Sehemu ya Ishirini Na mbili (22)



Mariam aliweza kuwa macho hadi alipofika Kibaha tu, baada ya hapo alisinzia kabla ya kupitiwa na usingizi mzito. Hakujua Chalinze walipita muda gani, hata gari lilipoingia kwenye mizani eneo la Mikese hakujua, alishtuliwa na abiria aliyekuwa ameketi naye siti moja gari lilipokuwa likiingia katika katika Kituo cha Mabasi cha Msamvu.

“Tumefika sister amka!” Kijana huyo akamwambia akimtingisha.

“Mmmmh!” Mariam akaitikia akionekana kuwa na usingizi.

“Tumefika, inaonekana umechoka sana!”

“Ah! Ni kawaida, siku zote huwa napenda kulala nikiwa safarini!”

“Unashukia hapa?”

“Hapana, nitakwenda kushukia mjini!”

“Sawa basi, mimi nashuka hapa!” Baada ya abiria waliokuwa wakishukia pale Msamvu kuisha, gari likaondoka na kuingia katikati ya Mji ya Morogoro likawashusha abiria wote, eneo la Masika.

Mariam akanyoosha moja kwa moja akifuata barabara iliyokuwa ikielekea katika Kituo cha Daladala kilichokuwa kituo cha zamani cha mabasi yanayokwenda mikoani. Kwa bahati nzuri akapata gari la kwenda kwao, tena lililokuwa likikaribia kuondoka. Akaketi siti ya dirishani akiwa mkimya sana.

Muda mfupi baadaye safari ya kwenda Matombo ikaanza. Matombo siyo mbali sana kutokea Morogoro mjini, lakini kwasababu ya ubovu wa barabara na milima, ilimchukua saa mbili na nusu Mariam kufika kijijini kwao. Aliposhuka kituoni akakodisha baiskeli ambayo ilimpeleka nyumbani kwa bibi yake, katikati ya mashamba na mapori makubwa, mwendo ambao uliwachukua saa nzima na nusu njiani.

Hatimaye Mariam alifika akiwa amechoka sana, bibi yake alipomuona alimkimbilia na kumkumbatia kwa furaha. Hata hivyo alishangazwa sana na hali ya afya yake ilivyokuwa imezorota! Baada ya salamu, bibi alianza kuuliza habari za mjini.

“Wazee hawajambo?”

“Wazima kabisa bibi, wanakusalimia sana!”

“Nimefurahi sana kusikia hivyo....enheee, vipi wewe na mwenzako?”

Mariam hakuweza kujibu kitu, ni kama alikuwa amechomwa na chuma chenye moto katikati ya kidonda kibichi! Machozi yakaanza kumiminika machoni mwake. Akaanza kulia kwa sauti ya chini.

“Vipi, mbona unalia tena?”

Mariam hakujibu zaidi ya kuendelea kulia, tena safari hii alilia kwa sauti kubwa zaidi ya awali.

“Sema basi mjukuu wangu, kuna nini? Au amepata matatizo? Niambie mimi ni bibi yako, nitakusaidia!” Kauli hiyo ya bibi yake ilizidi kumchoma Mariam ambaye sasa alizidisha kilio chake.

Kazi aliyokuwa nayo bibi yake, ilikuwa moja tu, kumbembeleza!

*******

Kwa muda mfupi sana, roho ya Mayasa ilibadilika! Roho yake ilikuwa mbaya kuliko hata ya muuza sumu! Mayasa alikuwa na roho mbaya kuliko kawaida, hata yeye mwenyewe alijishangaa na alishindwa kuelewa roho hiyo ya paka alipoipata.

Macho yake mawili yalikuwa yamemuelekea Rukia ambaye kwa mwonekano wake wa nje, haikuwa rahisi kuamini kwamba anaweza kumshawishi mtu aondoe uhai wa mtu mwingine kirahisi kiasi kile. Tamaa ya mali ilimvaa, heshima na umaarufu ulikuwa umemtawala moyoni mwake. Alikuwa tayari kwa lolote.

“Ni kweli upo tayari?” Rukia akamwuliza akimkazia macho.

“Nipo tayari kwa moyo wangu wote!”

“Sawa, sasa ipo njia, lakini lazima uwe makini sana!”

“Nimeshasema nipo tayari kwa lolote!”

“Hatutaki utusaliti Mayasa!”

“Ni kitu ambacho hakiwezi kutokea.”

“Tom anatakiwa kufa, ndani ya mwezi huu, hatutakiwi kuwa na haraka, unachotakiwa kufanya kwa sasa ni kuongeza mapenzi yako kwa nguvu, mchanganye kimapenzi sana, toka naye mara nyingi, jamii ione mapenzi yenu na ikiwezekana wadaku waandike, baada ya hapo kazi itafanyika kiulaini kabisa!”

“Sawa kabisa...” kila mmoja alimuunga mkono.

“Lakini nina wasiwasi na jambo moja!” Mayasa akasema akitetemeka, hakuweza kuificha hofu yake.

Rukia akamkata jicho la chuki lililojaa mashaka, kwa ilivyoonekana, kama Mayasa angeongea jambo lolote kupingana na uamuzi wake wa awali, basi hatari ambayo ingekuwa mbele yake asingeisahau hadi atakapoingia kaburini!



Kuulizwa habari za Tom, ilikuwa ni sawa na kumchoma kwa msumari wenye moto, katikati ya kidonda kibichi kilichokuwa moyoni mwake. Alitegemea kuulizwa na bibi yake juu ya Tom, lakini siyo mapema kiasi kile. Hata kama asingeulizwa, lazima angesema, kwani ndiyo sababu hasa iliyomfanya awe kule kijijini.

Moyo wa Mariam ulimuuma sana, alishindwa kuelewa ni mapenzi ya aina gani aliyokuwa kwa Tom, aliumizwa zaidi na jinsi alivyokuwa akimpenda kwa moyo wake mtu ambaye hakuonyesha kushtuka kabisa na penzi lake. Bibi yake alikuwa amemtonesha!

“Nyamaza mjukuu wangu, lakini lazima unieleze ukweli wa kilichotokea!” Baada ya Mariam kutulia, bibi yake akamwambia.

“Bibi kuna matatizo!”

“Ni nini?”

“Tom bibi, Tom ameniacha!”

“Amekuacha?””

“Ndiyo bibi!”

“Sababu?”

“Hakuna!”

“Haiwezekani, lazima kuna kitu umemuudhi mwenzako, lakini wazee wameshindwa kumaliza huko nyumbani?”

“Walikwenda kwake lakini walifukuzwa na Tom na mwanamke wake!”

“Mwanamke wake? Unataka kusema kwamba Tom ana mwanamke mwingine?”

“Tena anaishi naye pale nyumbani, mimi nilikuwa nalala chumba cha wageni, baada ya kuchoshwa na mambo yao, ndiyo nikaondoka kwenda nyumbani, huko napo ndiyo....” Mariam akamsimulia bibi yake kila kitu, hadi alipofikia hatua ya kulazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

“Pole sana mjukuu wangu, wewe baki hapa nyumbani, pumzika kwanza, utulize akili yako, mambo mengine yatafuata baadaye, naamini hali yako itarudi kuwa nzuri. Hapa utakula kambale na mboga za majani na afya yako itarudi kama zamani, sawa mama?!” Bibi yake akamwambia kwa sauti iliyojaa mapenzi mazito.

“Ahsante bibi, nimefurahi sana, umenifurahisha sana kwakweli, naanza kujiona mpya sasa.”

“Kama ndivyo kweli, basi Mungu wa Mbinguni ashukuriwe!”

“Amen!”

Maisha yaliendelea kijijini kama kawaida, Mariam akiwa anamsaidia bibi yake kazi za kilimo. Aliyafurahia mno maisha ya pale kijijini, kwani kama alivyotarajia awali, hapakuwa na mawasiliano ya aina yoyote, kitu ambacho ndiyo haswa alikuwa akikitegemea.

Afya yake ikaanza kurejea taratibu hadi ilipotengemaa kabisa, wazazi wake kila walipokwenda kumtembelea walikuta mabadiliko! Furaha ikarudi katika maisha yake. Ingawa ilikuwa kazi ngumu sana, lakini alijishangaa aliwezaje kumsahau Tom, mwanaume ambaye kwake alikuwa sawa na Wimbo wa Taifa!

Alifurahishwa sana na mabadiliko yake, kwa bahati nzuri bibi yake alishajua kwamba kutaja jina la Tom ni sawa na kuchochea matatizo aliyokuwa nayo, hivyo hakuthubutu kutaja jina la Tom katika mazungumzo yao. Siku zote alikuwa akimfundisha maisha ya kijijini na jinsi wazee wa zamani walivyoweza kuishi maisha marefu kijijini kutokana na aina ya vyakula wanavyokula.

“Kwahiyo bibi, unataka kuniambia kwamba hata mimi sasa nitaishi maisha marefu kwasababu nipo huku?”

“Bila shaka mjukuu wangu!”

“Lakini bibi ukiachana na vyakula, ni nini kingine kilichowafanya wazee wa zamani waishi miaka mingi zaidi kuliko hivi sasa?”

“Mazingira pia yanachangia, unajua Mariam, huku kijijini kila kitu ni cha asili. Hakuna kuvuta moshi wa dizeli wala petroli, hakuna mionzi ya minara ya simu, moshi wa viwandani wala dawa zenye kemikali, hizi ni sababu kubwa sana zilizowafanya wazee wa zamani waishi umri mrefu!”

“Sasa naanza kuelewa!”

Mariam alikubali maisha mapya, akajifunza vitu vipya kila siku. Hakika aliyafurahia maisha ya kijijini. Aliona ni bora kuishi maisha yale kijijini, kuliko kuishi Dar es Salaam lakini akiumizwa na kukosa amani ya kuendelea na maisha. Maisha ya kijijini yalikuwa chaguo lake la kweli na hakuwahi kuyajutia.

********

Kitendo cha Mayasa kusema kuna jambo lililompa wasiwasi, kilitoa tafsiri tofauti kwa Rukia. Msichana huyu ni katili na siku zote hakupenda kabisa msaliti katika mipango yake. Alimwangalia Mayasa kwa jicho la hasira akisubiria azungumze jambo lolote ambalo ni kinyume na makubaliano yao ili amuadhibu.

Mayasa akawaangalia wote kwa zamu, kisha akatingisha kichwa kama anayesikitishwa na jambo ambalo angelitamka.

“Una nini?”

“Nimeshasema kwamba kuna jambo linanitatiza kidogo!”

“Sema ni nini?”

“Hivi Rukia, askari hawawezi kujua kweli?”

“Labda uwaambie wewe, tena naomba nikuambie jambo moja, sina muda wa kupoteza zaidi juu ya jambo hili...ni hivi, leo jioni tutakutana katika kikao cha siri na vijana tutakaowapa kazi hii!”

“Ni wapi?”

“Mbezi!”

*******

Kilikuwa chumba kidogo, lakini nadhifu na kinachovutia, kikiwa na uwezo wa kuhudumia watu ishirini kwa wakati mmoja. Ndani ya chumba hicho kilichokuwa na kiyoyozi, kulikuwa na watu sita waliokutana katika kikao cha siri usiku huo.

Watu hao walikuwa ni Rukia, Mayasa na vijana wanne ambao walikuwa maalumu kwa kukodiwa kwa ajili ya kufanya mauaji. Wote walikuwa kimya, vinywani mwao, ukitoka moshi mzito wa sigara ambao wakati mwingine walikuwa wakiutolea puani na masikioni! Baada ya ukimya wa muda kupita, Rukia aligonga meza kwa nguvu!

“Tumekutana hapa kwa kazi moja muhimu iliyopo mbele yetu, kama nilivyotangulia kusema awali, Papaa Bill anatakiwa aondoke duniani, tena ndani ya mwezi huu! Malipo yenu ni mazuri sana na leo mtapata malipo ya utangulizi!” Alisema Rukia, akiwatazama wote kwa zamu.

“Hakuna tabu sister Rukia, nafikiri unatuamini katika michongo hii, sisi hatuna noma, tupeni cash, tufanye kazi!”

“Hakuna shida, suala la pesa siyo tatizo kwangu, chukueni hizi kwanza na ninaomba baada ya wiki mbili Papaa Bill awe na jina lingine! Marehemu nadhani ni jina litakalomfaa zaidi!” Mayasa alisema akitoa shilingi milioni tano kama fedha za utangulizi na kuwapatia wale vijana.

“Hakuna tabu, tunakuhakikishia kazi nzuri baada ya huo muda uliosema.” Mmoja wao ambaye ndiye aliyepokea zile fedha alisema.

“Kilichobaki ni utekelezaji tu!” Mayasa akasema.

“Kuhusu hilo, usijali kabisa, hawa vijana nawaaminia!” Rukia akasema.

“Sawa, tutaona!” Kikao kikaahirishwa.

******

Alichokifanya Mayasa ni kuwa karibu zaidi na mume wake kuliko kipindi kingine chochote walipokuwa wakiishi na Tom. Alijifanya kumpenda zaidi, kuwa karibu naye zaidi kuliko kawaida. Tom akafurahi sana, akazidi kumpa siri zake za biashara akiamini alikuwa mke mwema wa maisha yake.

Hakujua kilichokuwa nyuma ya pazia, laiti kama angejua alikuwa katika hatari ya kufa wakati wowote, angeachana naye haraka sana, lakini jambo hilo hakulijua kwani lilikuwa siri kubwa sana. Maisha yaliendelea kama kawaida, Mayasa akiendelea kuwasiliana kwa karibu na vijana waliopewa kazi ya kumuua Tom na kuelekezekana kila kitu kwa hatua.

“Nadhani sasa kila kitu kipo tayari, mnaweza kukamilisha hiyo kazi!”

“Poa sister, ungependa iwe lini?”

“Kesho usiku, miye nitakuwa nyumbani, halafu nyie mtamtegea jirani na nyumbani mpaka atakapoingia, lakini muda wake mara nyingi ni saa mbili na madakika hivi, lakini haifiki saa tatu!”

“Umesomoka!”

Siku iliyofuata, kuanzia saa moja na nusu jioni, nyumba ya Tom ilikuwa imezungukwa na vijana sita wenye silaha, wakisubiria muda atakaorudi! Kama kawaida yake, saa mbili na robo alikuwa getini akipiga honi mfululizo ili afunguliwe lakini cha ajabu hakuna aliyetokea kumfungulia!

“Shiiit! Huyu mwanamke vipi, kwanini hanifungulii, ngoja nishuke nikagonge mwenyewe!” Tom akasema akifungua mlango wa mbele ili atoke, lakini kabla hajafanya hivyo akashangaa akihisi kitu cha baridi kikigusa shingoni mwake.

“Tulia hivyo hivyo, nyoosha mikono yako juu na ufuate maagizo yote tutakayokuambia!” Alisikia sauti ya mtu ikimuamrisha nyuma yake.

“Kuna nini tena jamani?”

“Hatubishani, lakini kama utaleta ubishi wa aina yoyote nakulipua sasa hivi!”

Sekunde chache baadaye, Tom alikuwa amezungukwa na watu sita waliokuwa wanaonekana dhahiri kuwa ni watu wa mazoezi. Alishajua kwamba kifo chake kilikuwa kimekaribia! Isingekuwa rahisi akubali kufa kijinga kiasi kile, alitakiwa kufanya jambo fulani ili aokoe roho yake.

“Jamani kama ni pesa au kitu chochote cha thamani mnataka, niambieni niwape lakini mniachie roho yangu, nawaombeni sana!”

“Hatuna shida na pesa zako!”

“Sasa kumbe mnataka nini jamani?!” Tom akasema akitetemeka kwa woga.

“Tunahitaji roho yako!”

“Roho yangu?”/


“Ndiyo, unatakiwa kufa Tom!” Tom akachanganyikiwa zaidi.

“Sikilizeni ndugu zangu, mnajua...” hakupewa nafasi ya kumalizia sentesi yake.

“Hivi kwanini tunamkawiza?”

“Mlipue!” Mwingine akadakia.

Hakuna aliyezungumza tena baada ya hapo, muda mfupi baadaye ulisikika mlio wa risasi. Wale vijana wakatoweka na kumuacha Tom akiwa ameanguka chini hoi, damu zikimvuja mwilini. Tom alikuwa hajitambui!



lio wa risasi ulisikika mara tatu, lakini baada ya hapo muungurumo wa gari ukasikika. Hiyo ilimaanisha tayari wauaji walikuwa wameshatoweka eneo la tukio. Ndani ya dakika tatu tu, watu walikuwa wamejaa getini mwa nyumba ya Tom wakishuhudia Tom alikiwa hajigusi chini, huku damu zikimtoka kwa wigi!

“Mume wangu oh! Mume wangu jamani...” Mayasa naye alitoka nje na kuanza kulia, akamlalia Tom, huku akisikilizia mapigo yake ya moyo kuhakikisha kwamba alikuwa amekufa au lah!

“Nitabaki na nani miye...Tom wangu jamani...” Mayasa alizidi kupiga kelele.

Watu walimuonea huruma sana, walijua ni kaisi gani alikuwa anaumia kutokana na matatizo aliyopata mumewe. Hakuna aliyejua kwamba yote aliyokuwa akiyafanya ilikuwa ni maigizo tu! Siri hiyo aliijua yeye mwenyewe.

“Lakini wezi gani wa mapema hivi?’ Mtu mmoja aliyekuwa kwenye tukio lile aliuliza.

“Hata mimi nashangaa...” mwingine akadakia.

“Mnashangazwa na nini jamani, kama watu wanaiba kwenye benki mchana inashindikana vipi kwa muda huu?”

“Lakini mbona hawajachukua kitu?”

“Hata mimi nashangaa!”

Kila mmoja alikuwa anaongea lake, lakini wengi walishangazwa sana na majambazi hao, ambao hawakuiba kitu chcohote zaidi ya kumdhuru Tom na kuondoka zao. Ilionekana kuwepo kwa kitu kilichojificha, kitu ambacho hakuna ambaye alikuwa anakijua.

Muda mfupi baadaye watu walijadiliana na kuamua kumkimbiza Tom katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Akalazwa kwa ajili ya kupatiwa matibabu. Muda wote huo Mayasa alikuwa analia sana, alionyesha huzuni kubwa, lakini moyoni mwake alikuwa akitamani sana Tom afe, hilo ndilo lililokuwa akilini mwake.

Kilichoonekana usoni mwa Mayasa kilikuwa tofauti kabisa na kilichokuwa moyoni mwake. Mayasa alikuwa na roho mbaya kuliko hata ya muuza sumu! Aliweka mbele masilahi yake baada ya kifo cha Tom.

“Samahani Dokta naweza kumuona mume wangu?”

“Hapana, yupo kwenye uangalizi maalum kwa sasa, tafadhali nenda urudi kesho asubuhi!”

“Lakini atapona?”

“Tumuombe Mungu, tutajitahidi kufanya kila tutakaloweza, lakini nguvu za Mungu ndizo zinazohitajika zaidi katika hili.”

“Ahsante sana Dokta.”

*****

Kilikuwa chumba kidogo, kizuri, chenye hewa safi ya kiyoyozi, ndani ya chumba hicho kulikuwa na vijana wanne na wasichana watatu, hiyo ndiyo ilikuwa Kamati nzima ya mauaji ya Tom. Wote walikuwa kimya, wakimtizama Rukia ambaye alikuwa ndiye Kiongozi wa Kamati hiyo. Rukia akapiga meza kwa nguvu!

“Nina furaha sana, nina furaha kwasababu kazi ambayo tuliwatuma, mmeikamilisha ingawa siyo kwa kiasi kikubwa!” Rukia alianza kuzungumza.

“Samahani sister!” Mmoja wa vijana wale akasema.

“Nakusikiliza!”

“Kwanini unasema siyo kwa kiasi kikubwa?”

“Acha wasiwasi kijana, nimesema siyo kwa kiwango kikubwa kwakuwa hajafa lakini nafikiri Mayasa atakuwa na majibu mazuri juu ya hilo kwakuwa yeye ndiye aliyeenda naye hospitalini!”

“Ni kweli Rukia, hali yake siyo nzuri, hana dalili za kupona kabisa, hadi sasa hivi hajazinduka, naona lazima atakufa tu!”

“Ni kweli kabisa!”

“Na hilo ndiyo lengo letu.”

“Kikubwa zaidi kilichotukutanisha hapa ni kuwalipa pesa zenu zilizobakia, lakini kama tukihitaji msaada wenu baadaye tutawajulisha na tafadhali mtoe ushirikiano.”

“Hakuna tabu sister Rukia.”

“Sawa.. Mayasa...” Rukia akaita.

“Nakusikiliza.”

“Wapatie mzigo wao uliobakia.”

Mayasa hakuwa na kitu cha kuzungumza zaidi ya kuchukua fedha kwenye pochi yake na kuwakabidhi.

“Tunashukuru sana kwa msaada wenu, lakini lazima jambo hili liwe siri,” Mayasa akasema.

“Siyo tu, siri bali kama tutaisikia mahali popote, basi mjue kuwa kifo kitakuwa jirani zaidi na nyie!”

“Kuhusu hilo huna sababu ya kuwa na wasiwasi nalo, kwani ni kazi ya kwanza tunafanya na wewe?”

“Lakini watu wanabadilika!”

‘Watakuwepo ila siyo sisi!”

“Nimefurahi kusikia hivyo!” Baada ya hapo kikao kikaahirishwa.

Siku iliyofuata, asubuhi na mapema Mayasa alikuwa ameshafika hospitalini, alikuwa makini sana na Tom, akihakikisha anamhudumia kwa karibu, lakini nia yake ya moyoni ilikuwa ni Tom afe, alichukia sana kumuona Tom akiwa bado anaendelea kuwa hai, ingawa alikuwa anapumua kwa msaada wa mashine.

Aliendelea kuwa karibu na Tom siku zote, hakuna aliyejua kilichokuwa akilini mwa Mayasa, kilichokuwa kikifanyika ilikuwa ni mchezo wa kuigiza tu, siri ambayo aliitunza moyoni mwake.

Wiki moja baadaye hakuona sababu ya kuendelea kumficha mama yake Tom juu ya hali ya mwanaye. Akafanya mawasiliano haraka, ambapo siku iliyofuata mama Tom alikuwa ameshafika Dar es Salaam, akipokelewa na Mayasa. Siku zote mama yake Tom, hakuwa akimpenda Mayasa, lakini kwasababu alishamuomba sana mwanaye aachane naye na akakataa, hakuwa na sababu ya kuendelea kuingilia mapenzi yao.

“Enhee vipi hali yake?” Mama Tom aliuliza mara baada ya kufika nyumbani na kuketi sofani.

“Pumzika kwanza mama!”

“Hapana, lazima nijue hali ya mwanangu!”

“Hana hali mbaya sana mama, lakini kesho asubuhi tutaongozana pamoja kwenda kumtizama, ila nimewasiliana na daktari wake amesema hali yake sasa siyo mbaya sana!”

“Fahamu zake zimesharudi?”

“Bado, lakini ana nafuu kubwa!”

Mama Tom alimpenda sana mwanaye, hakuwa tayari kumuona anakufa akiwa mdogo kiasi kile, kwa maisha ya shida ambayo amekulia, aliamini alipaswa kuendelea kuwa hai ili ale matunda ya jasho lake.

Kila alipokumbuka siku aliyotoka kwenye mgodi unaotitia akiwa na madini kwenye mfuko wake wa salufeti, alitokwa machozi. Kwake Tom alitakiwa aendelee kuyafaidi maisha! Kufa mapema kiasi kile ilikuwa ni pigo kubwa sana kwake. Mayasa alipata kazi ya kumbembeleza mama Tom, ambaye hakunyamaza mpaka sauti ilipoanza kukauka ndipo akanyamza na kupitiwa na usingizi.

Yeye ndiye aliyemwamsha Mayasa asubuhi, akimkumbusha kuwahi hospitani kumwona Tom. Walipoingia wodini na mama Tom kumuona mwanaye akiwa amefungwa mashine za kupumua, alichanganyikiwa! Tom alikuwa na hali mbaya sana na hadi wakati huo alikuwa hajitambui!

Ghafla mama Tom akaanza kuhisi kizunguzungu kikali, mwili wake ukaanza kupoteza nguvu taratibu, kisha akaanguka chini kama mzigo! Muda huo huo akakimbizwa wodini na kuanza kushughulikiwa. Hata hivyo hali yake ilizidi kuwa mbaya, usiku wa siku ile ile, mama Tom alifariki dunia!

“Pole sana dada, mgonjwa ni nani wako?” Daktari aliyekuwa akimhudumia alimwuliza Mayasa akifikiria jinsi ya kumweleza juu ya kifo cha mama huyo.

“Mama mkwe wangu, kwani vipi?”

“Kwa bahati mbaya sana, ameshafariki dunia!”

“Unasema?”

“Usijali ni mambo ya kawaida ambayo unapaswa kukubaliana nayo, hata kama ukilia, machozi yako hayataweza kumrudisha mama duniani, zaidi utakuwa unajiumiza mwenyewe.”

“Lakini kwanini inakuwa kwangu, nina mkosi gani mimi jamani! Mume wangu amelazwa na mpaka sasa hivi hajarejewa na fahamu, mama naye amefariki, nitakuwa mgeni wa nani mimi?”

“Usijali dada yangu, kubaliana na hali halisi, hatuwezi kubadilisha kilichotokea, zaidi unapaswa kumshukuru Mungu maana ameagiza tushukuru kwa kila jambo.”

“Ahsante sana Dokta, nashukuru. Acha nikawapashe habari ndugu zetu na kuandaa taratibu za mazishi.” Mayasa akasema na kuondoka.

“Sawa.”

Mayasa aliondoka akiwa na mawazo mengi sana kichwani mwake, hakuona sababu ya kuendelea kuishi nyumbani kwa Tom, alishachuma mali za kutosha kwa kipindi kifupi sana ambacho Tom alikuwa amelazwa hospitalini. Aliweza kufanya hivyo kwasababu Tom alikuwa akiweka mambo yake wazi.

Alishachukua fedha katika akaunti zote na kuziacha nyeupe kabisa, madini yaliyokuwa yakihifadhiwa chumbani nayo aliyachukua na kuyauza. Hakurudi tena hospitalini kumuangalia Tom wala kuuchukua mwili wa mama mkwe wake kwa ajili ya mazishi.

Wiki moja baadaye, kila kitu kilikuwa tayari na kilichokuwa mbele yake ilikuwa ni kuondoka nchini, kwenda zake kujichimbia Uingereza. Hilo ndilo lililofanyika, Mayasa akapanda ndege na kwenda zake Uingereza, akiwa hajui kabisa kilichoendelea huku nyuma.

******

Maisha ya kijijini Matombo, yalianza kumzoea Mariam, kama ilivyokuwa nia yake, kujitenga mbali na mji ili asiweze kujua habari zinazomhusu Tom na Mayasa. Alifurahia sana kuishi kijijini na aliyapenda maisha ya kule. Hata afya yake ilianza kuridhisha. Siku moja alitumwa na bibi yake mjini. Alipokuwa akikatiza eneo la Nunge akaona meza ya magazeti, hakutaka kuisogelea, maana alijua pengine angekutana na habari za Tom, jambo ambalo hakutaka litokee.

Katika hali ya kushangaza sana, akajikuta kuna kitu kinamlazimisha kwenda kwenye meza ile ya magazeti. Baadaye akaamua kwenda, akijipa moyo kwamba hata kama ataona habari zake, hazitamuuma sana kwasababu tayari ameshaanza kumzoea!

Magazeti karibu yote ya siku hiyo, yaliandika habari juu ya kifo cha mama yake Tom, Mariam alihisi kuchanganyikiwa! Macho yake yakatua juu ya gazeti la Ijumaa. Gazeti hilo lilikuwa limeandika kwa maandishi yaliyosomeka; ...wakati hali ya Papaa Bill ikizidi kuwa mbaya, MAMA YAKE MZAZI AFARIKI DUNIA! Chini ya maneno hayo, kulikuwa na maneno mengine yaliyosomeka; Mwenyewe yupo hoi Muhimbili, bado hajapata fahamu, mkewe amkimbia...soma habari kamili uk. 2

Zilikuwa habari mbaya sana kwa Mariam, akajikuta akipoteza nguvu taratibu, giza totoro likaanza kupita mbele ya macho yake. Akaanguka chini na kupoteza fahamu.




Alishaumia vya kutosha, alishateseka kiasi cha kutosha, aliamua kuishi kijijini Matombo ili asizidi kuteseka, alitaka kuwa mbali na maumivu ya mapenzi. Ni kweli alikuwa akimpenda sana Tom, hata moyo wake ulimhakikishia jambo hilo, lakini ilikuwa lazima awe mbali na matatizo!

Kumpenda mtu si tatizo, lakini kwa Mariam ilikuwa tatizo! Alikuwa na kila sababu ya kujitenga na matatizo. Hakutaka kuzidi kujipa mateso ambayo anaweza kuwa nayo mbali.

Mariam hakuwa na penzi la kinafiki, alikuwa na penzi la dhati ambalo siku zote lilikuwa hai, lakini hakutaka kumwaga machozi tena, hakutaka kuumia zaidi, lakini kwasababu tayari alishatambua kwamba moyo wake ulimpenda sana, akaona njia pekee ilikuwa ni kumkimbia!

Pengine ulikuwa uamuzi wa busara, lakini safari yake ya mjini ya siku hiyo, ilisababisha matatizo makubwa, ikatonesha kidonda kilichoanza kukauka. Mambo yakawa yale yale! Hakuweza kuvumilia kusoma habari za Tom akiwa amelazwa hospitalini, tena akiwa hana msaada wowote, mbaya zaidi mama mkwe wake akiwa amefariki! Hilo lilimuuma sana na kujikuta akianguka chini na kupoteza fahamu!

Hakuna aliyekuwa na taarifa za Mariam.

“Vipi jamani?!” Mmoja wa watu waliokuwa wamesimama mbele ya meza ile ya magazeti alisema.

“Siyo suala la kuuliza, kilichobaki hapa ni kumsaidia tu!”

“Lete gari bro,” jamaa mmoja alijitolea kumchukulia na teksi.

“Mshike huko...tusaidiane jamani...” watu wakasaidiana kumwingiza Mariam kwenye gari na safari ya kwenda Hospitali ya Mkoa wa Morogoro ikaanza.

Kutoka Nunge hadi Hospitali ya Mkoa, hapakuwa mbali, dakika tano tu tayari gari lilikuwa limeshaingia ndani ya Jengo la Hospitali hiyo. Walipofika mapokezi, waliruhusiwa kwenda moja kwa moja Chumba cha Mapumziko, akapokelewa vizuri na kuanzishiwa tiba haraka.

INAENDELEA

Post a Comment

0 Comments