“Lazima ufe, we bweha!” Mmoja wa wanaume wale walioonekana kuwa na hasira sana akauliza.
“Nimefanya nini lakini?”
“Utajua mwenyewe, jiulize ni nani ambaye una ugomvi naye!”
“Ugomvi?”
“Ndiyo, ugomvi...ni nani ambaye huna maelewano naye?”
“Mbona naishi na watu vizuri sana!”
“Hata hivyo, hiyo siyo kazi yetu, tunachojua sisi ni kukuua tu na hiyo ndiyo kazi yetu ambayo tumelipwa kuifanya, hayo mambo mengine hatuna haja nayo!”
“Msiniue tafadhali!”
“Tutakuua tu lazima, hakuna kitu cha kubadilisha ukweli huu, lazima ufe.” Mtu mwingine ambaye alionekana kama ndiye mkuu wa wengine alisema kwa hasira.
Tom alishindwa kuelewa mahali pale palikuwa ni wapi na alifikaje? Alijaribu kuwaza kama kuna mtu alikosana naye, lakini hakumuona. Ghafla akashangaa amepoteza fahamu, alipozinduka baadaye, alikuwa katika katikati ya pori nene, mbele yake kukiwa na shimo kubwa, akiwa amezungukwa na wale vijana wenye silaha mikononi mwao.
Tom alikuwa amefungwa kamba mikono yote na miguu na hakuw ana uwezo wa kufanya jambo lolote. Tom alitetemeka sana.
“Naombeni mnisamehe tafadhali!”
“Hatuwezi kukusamehe, lakini tutafanya jambo moja kwa ajili yako!” Kiongozi wa lile kundi akasema.
“Ni nini?’
“Tutakuonyesha picha ya mtu ambaye ametuagiza tukuue!”
“Sawa, naombeni nimuone!” Tom akasema akiwa na hamu kubwa sana ya kujua ni nani ambaye aliamua kufanya njama za kumuua.
“...ambaye anataka ufe ni huyu hapa...halafu acha kufuatilia maisha ya watu...kufa salama...” Yule mtu akamwambia akimwonyesha ile picha.
Macho ya Tom hayakuwa tayari kuamini mtu wake wa karibu, mpenzi wake wa kweli ambaye aliamua kuachana na mkewe kwa sababu yake ndiye aliyekuwa akitaka auawe. Ilikuwa picha ya Mayasa. Tom akachanganyikiwa.
“Mayasa, nooooooooo.....” Tom akapiga kelele.
Katika hali ya kushangaza sana, wale wakaanguka mmoja mmoja baada ya kupigwa risisi kama mvua miilini mwao. Tom hakuweza kugundua ni nani aliyewapiga risasi. Ghafla akashangaa kumuona mtu mbele yake akiwa amevaa kininja, akijifunika hadi usoni.
Mtu huyo akaanza kuvua zile nguo za Kininja, kisha akavua ile kofia iliytofunika hadi uso wake, hapo ndipo Tom alipogundua alikuwa ni Mariam. Tom akashtuka sana.
“Mariam?!”
“Ndiyo ni mimi ninayekupenda, ambaye penzi langu halina mashaka kwako, nakupenda Tom ndiyo maana nimekuja kukuokoa...” Mariam akasema akitokwa na machozi kama mvua.
“Siamini macho yangu...Mariam....”
“Ni mimi!”
“Marimuuuuuuuuu....” Tom akapiga kelele kwa sauti ya juu sana. Muda huo huo akazinduka usingizini, alikuwa amelala kitandani na Mayasa, hapo ndipo alipogundua kwamba alikuwa ndotoni.
Ilikuwa ndoto ya ajabu sana, hakuweza kujua maana ya ile ndoto. Alipogeuza macho yake kumwangalia Mayasa, alimkuta akiwa anakoroma usingizini, akawasha taa na kunyanyuka polepole kitandani, kisha akaizima taa na kutoka hadi sebuleni kwenda kumfuata Mariam.
Moyo wake ulimuuma sana kumkuta Mariam hadi wakati ule hajazinduka, alichokifanya ilikuwa ni kumbeba hadi chumba cha wageni na kumlaza kitandani, akamfunika shuka na kumwekea chandarua. Moyo wake ulikuwa kama umepigwa ganzi, alishindwa kulewa ilikuwaje hadi akamchukia Mariam kiasi kile.
“Nashindwa kuelewa kwanini inakuwa hivi, ni kweli mimi siyo wa kwanza kuwa na mwanamke wa nje, lakini mbona mimi namfanyia mke wangu vituko kiasi hiki? Kuna nini lakini?” Tom akajikuta akijiuliza maswali mfululizo kichwani mwake bila kupata majibu yakinifu.
Akiwa anamwangalia Mariam aliyekuwa amelala pale kitandani kwa huruma, akashangaa mtu akimgusa mgongoni.
“Hivi we’ mwanaume una nini? Hutosheki? Umeona uje na huku?”
“Ah! Mayasa?!”
“Ndiyo mimi, unashangazwa na nini?”
“Samahani mpenzi wangu?”
“Imekuwaje tena?”
“Ah, hakuna kitu.”
“Unafanya nini hapa?”
“Nimeamua kumleta Mariam huku.”
“Kwanini?”
“Mbu zilikuwa zinamng’ata sebuleni.”
“Una uhakika hakuna zaidi ya hivyo?”
“Ndiyo, hakuna kitu.”
“Kwanini hukuniaga?”
“Sikuona sababu ya kukusumbua.”
“Haya twende chumbani.” Mayasa akamuamrisha Tom ambaye hakubisha.
Mayasa alikuwa mbabe kupitiliza, alikuwa na kitu kilichomfanya awe na jeuri aliyokuwa nayo, nguvu za giza alizokuwa akizitumia zilikuwa zinafanya kazi vyema bila ya Tom kugundua chochote. Walipofika chumbani, kazi ilikuwa moja tu, kupeana mapenzi motomoto hadi asubuhi.
Hawakulala tena, Tom hakuwa na kumbukumbu za Mariam tena, kichwani mwake kulikuwa na mtu mmoja tu, Mayasa. Alimuona mwanamke mzuri kuliko kawaida.
“Nakupenda sana Mayasa!” Tom akamwambia.
“Una uhakika?’
“Ndiyo, nakupenda sana, huoni mambo niliyokufanyia?”
“Mambo gani?”
“Nimekujengea nyumba nzuri, nimekupa gari na kila kitu utakacho nakupa, hiyo haitoshi kukufanya uamini kwamba nakupenda?”
“Haitoshi!!!”
“Unataka nifanye nini tena, sema chochote nitafanya!”
“Kweli?”
“Ndiyo, nakupenda sana na sitaki kukufanya uumie kwa ajili yangu!”
“Nataka umfukuze Mariam hapa nyumbani, tuishi kwa furaha!”
“Na kule kwako?”
“Nitaweka mpangaji, nataka kuishi na wewe hapa!”
Tom hakuwa na jibu.
*******
Jicho lake la kuume ndilo lilikuwa na kwanza kufumbuka, kisha likafuata la upande wa kushoto. Taratibu kumbukumbu zikaanza kumrejea Mariam. Kilikuwa chumba ambacho siyo alichokuwa akilala siku zote. Akapiga jicho kila upande na kujaribu kuvuta kumbukumbu zaidi, akatambua kwamba ni kweli siyo chumba anacholala siku zote.
Akakumbuka vyema kwamba kilikuwa chumba cha wageni, tena alichokiandaa jioni yake kwa ajili ya mgeni ambaye Tom alimwambia angekuja naye. Kufikia hapo, akakumbuka kila kitu. Alikuwa amelala katika chumba cha wageni. Hakuweza kukumbuka aliingia vipi na muda gani. Akaamka kichovu na kupiga hatua za taratibu kuelekea chumbani kwake.
Alipofika mlangoni, akasikia kelele za mahaba zikitokea chumbani. Walikuwa ni Tom na Mayasa wakipeana maraha chumbani. Mariam akachanganyikiwa, lilikuwa tukio la udhalilishaji sana. Mariam akachungulia kupitia tundu la ufunguo lililokuwa mlangoni, alichokiona humo ndani hakifai kuandikika hapa! Akaanza kulia.
“Tom mume wangu, ni nini unafanya na huyo mwanamke wako? Kwanini unakuwa hivi lakini? Yaani umeshindwa kufanya uchafu wako huko nje, unakuja kunifanyia hapa nyumbani, tena chumbani kwetu, katika kitanda ninacholala na wewe...Tom...Tom...Tom...kwanini unafanya hivi lakini?!” Mariam akapiga kelele akilia kwa uchungu.
Muda mfupi baadaye mlango ulifunguliwa, Mayasa akatoka akiwa amevaa upande wa kanga, tena kanga yake mwenyewe, uso wake ulikuwa umejaa makunyanzi, akamsogelea na kumzaba kibao kikali sana shavuni mwake.
“Koma kuharibu starehe za watu, ungekuwa na maana angenileta hapa? Huna jipya, mwanamke hujui mapenzi zaidi ya kufua na kupika, unafikiri kwa mtindo huo ataacha kutafuta mtoto wa mjini anayeweza kumpa raha kama mimi? Na utalijua jiji na mitaa yake...” Mayasa akasema akibenua midomo yake.
Uso wa Mariam ulilowana kwa machozi, alishindwa kuelewa kwanini mateso yale yalikuwa kwake tu na siyo kwa mwingine.
“Halafu Mariam uwe na adabu, naomba usijaribu kumsumbua mpenzi wangu, nenda kalale chumbako kwako kule!” Tom naye akatoka na kumwambia Mariam.
Mariam alihisi alikuwa ndotoni, lakini ukweli ni kwamba haikuwa ndoto, kila kilichokuwa kikitokea katika maisha yake kilikuwa yakini kwa maana ya yakini haswa.
Masikio ya Mariam yalikuwa hayataki kuamini yalichosikia wakati macho yake yakikataa katakata kukubaliana na kilichoonekana kupitia tundu la funguo, mambo yaliyofanyika chumbani yalikuwa mazito sana. Alishindwa kuelewa ni kosa gani kubwa alilomfanyia Mungu kiasi cha kumpa adhabu kubwa kiasi kile.
Ilikuwa lazima afikirie kitu cha kufanya, mawazo pekee yasingeweza kutosha kukabiliana na tatizo lililokuwa mbele yake. Alijua kitu kimoja moyoni mwake, kwamba alikuwa anampenda sana Tom, na mambo yote yaliyokuwa yakitokea ni juhudi za shetani kutaka kumharibia mume wake.
“Mungu ni wewe peke yako ndiye mwenye uwezo wa kunisaidia tatizo hili, naomba msaada wako baba, sina uwezo peke yangu, nisaidie mwanao...” Mariam aliomba moyoni mwake machozi machoni mwake yakitiririka.
Mara akapata wazo jipya, aliona ni bora aendelee kumuomba Tom abadili mawazo yeke. Aachane na huyo mwanamke kwani yeye ndiye mkewe wa ndoa aliyekuwa kwa ajili yake.
“Tom mume wangu, kwanini unanitesa kiasi hiki? Ni kosa gani nililokufanyia lakini mume wangu mpenzi? Kumbuka ahadi yako siku ya ndoa Tom, kumbuka!” Mariam alisema akitokwa na machozi.
“Huna kosa Mariam...” Tom akajibu akiwa chumbani.
“Sasa kwanini unanitenda hivi?”
“Huna mvuto mtoto wa kike, ndiyo maana ameona awe na mimi mwenye mvuto.” Mayasa akajibu.
“Sijakuuliza wewe!”
“Kumbe umemuuliza nani?”
“Mume wangu!”
“Unachekesha sana wewe, hivi Tom ni mumeo kweli wewe?”
“Kwani mume wa nani?”
“Yupo na nani chumbani? Hivi angekuwa anakuthamini angekulaza chumba cha wageni? Ameona huna jipya ndiyo maana amekususa, mwanamke usiye na haya, unayesubiri kutupiwa mabegi nje?! Kwani huoni kuwa hutakiwi humu ndani? Si uondoke...” Mayasa alisema maneno hayo macho makavu akiwa hana woga hata kidogo, alimchukia Mariam kuliko kitu chochote.
Mariam alikuwa ni kama anaharibu mambo yake, wazo la kwamba yeye ndiye aliyemwingilia mwenzake nyumbani kwake halikupata nafasi kabisa akilini mwake. Aliona kama Mariam ndiye aliyekuwa akimwingilia yeye.
Mariam alilia kwa uchungu mwingi sana, aliamini machozi yake pengene yangemuuma Tom na kubadilisha uamuzi wake, lakini ilikuwa tofauti kabisa, Tom alikuwa kimya chumbani akila raha na Mayasa, hakuonyesha kujali hata kidogo thamani ya chozi la Mariam.
Maisha yaliendelea kwa mtindo wa Mariam kulala chumba cha wageni na Tom kulala na Mayasa huku Mariam akishurutishwa kufanya kazi zote za nyumbani. Ni kama alikuwa mfanyakazi wa ndani! Kazi kubwa ya Mariam ilikuwa ni kusali, akimuomba Mungu wake amsaidie. Maisha yalikuwa ya shida sana.
Afya ya Mariam ikaanza kuzorota, kila siku kwake ilikuwa ni kilio. Tom hakuonyesha kujali, Mayasa alikuwa ndiye kila kitu nyumbani kwake, alipanga na kutoa amri ya kila jambo ndani ya nyumba. Usiku mmoja Mariam hakulala kabisa, alitumia kuwaza maisha yake, kwa muda wa miezi mitatu aliyovumilia, hakuna hata siku moja ambayo Tom alionyesha dalili za kubadilika tabia wala msimamo wake.
Tom alizidi kuwa mkali kwake na hakutaka kushirikiana naye kwa chochote, Mariam hakuona kama kuna sababu ya kuendelea kuteseka kwa mwanaume ambaye alikuwa hana mapenzi na yeye tena. Akapanga nguo zake usiku huo kwa safari ya kuondoka asubuhi yake. Alishachoshwa na vituko vya Tom.
*****
Saa kumi na mbili asubuhi, Mariam alikuwa ameshajiandaa kuondoka. Akiwa na begi lake la nguo, alikwenda hadi mlangoni mwa chumba cha Tom na Mayasa na kugonga. Alitumia muda wingi sana kugonga bila kufunguliwa.
“Nani?” Tom akauliza kwa ukali.
“Ni mimi!” Mariam akajibu kwa sauti ya unyonge sana.
“Sawa wewe, lakini nani?”
“Mariam!”
“Unataka nini asubuhi yote hii? Kwanini unatuharibia starehe zetu?”
“Samahani, sina nia mbaya!”
“Shida yako ni nini?”
“Nimekuja kukuaga Tom, naenda kwetu, nakuacha uendelee kuishi na mwanamke wako ambaye umeona anafaa kuliko mimi!”
“Siyo kwamba nimeona anafaa kuliko wewe, bali ndiyo uweli wenyewe ulivyo. Sasa unaondoka sasa hivi au baadaye?”
“Nimekuja kukuaga sasa hivi naondoka!”
“Hakuna neno wasalimie wote, waambie Tom au Papaa Bill sasa anakula bata na mtoto mzuri Mayasa!”
Mariam hakujibu tena, akaanza kulia akivuta mabegi yake kwenda nyumbani kwao. Kwa Mariam ilikuwa siku mbaya sana ambayo kwa hakika isingeweza kufutika katika maisha yake, lakini kwa Mayasa na Tom, ilikuwa siku nzuri sana kwao, kwani walikuwa wanaachiwa uhuru wa kufanya kila kitu wanachotaka kwa nafasi!
*****
“Vipi tena mwanangu? Mbona hivyo?!”
“Mama acha tu!”
“Nini?”
“Matatizo!”
“Matatizo gani? Mbona sikuelewi?”
Mariam hakuweza kujibu kitu tena zaidi ya kulia. Mama yake akamfuata huku naye machozi yakimtoka, lakini kabla hajamfikia, Maram alianguka chini na kupoteza fahamu.
“Mungu wangu, mwanangu ana nini jamani? Nini kimempata tena jamani?” Mama yake na Mariam alipiga kelele, muda huo huo baba yake Mariam akatoka ndani.
“Vipi kuna nini?”
“Mariam amekuja analia...kaanguka chini kabla hata sijajua kinachomsumbua!”
“Amesema ana tatizo gani?”
“Hajasema chochote, tumpeleke hospitalini kwanza, hayo mambo mengine tutajua baadaye!”
“Sawa!”
Hawakuwa na muda wa kupoteza, wakamwingiza Mariam kwenye gari na kumpeleka katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Nusu saa baadaye tayari walishafika hospitalini na Mariam apelekwa katika chumba cha mapumziko kwanza kwa ajili ya kupewa huduma ya awali.
“Nini kimempata?” Daktari aliwauliza wazazi wa Mariam.
“Ameanguka ghafla!”
“Kabla ya hapo alikuwa anaumwa?”
“Kwakweli hatuna uhakika maana alitokea kwa mume wake asubuhi hii akiwa katika hali hii, inawezekana amegombana naye!”
“Mmejaribu kumtafuta kwenye simu?”
“Ndiyo, hapatikani.”
“Ok! Subirini kidogo nje, acha sisi tufanye kazi yetu!” Daktari yule akasema akiwatizama wenzake ambao walitingisha vichwa kumuunga mkono alichokizungumza.
Wazazi wa Mariam wakatoka nje na kuwaacha madaktari wakijaribu kuokoa maisha ya Mariam.
“Sijui atakuwa amepatwa na nini mwanetu jamani!” Mama Mariam akamwambia mume wake.
“Inawezekana kuna kitu wamekorofishana na mume wake, maana naona hata afya yake siyo nzuri kabisa.”
“Mungu amsaidie apate nafuu kwanza, tutazungumza naye baadaye!”
Waliendelea kuzungumza juu ya afya ya mtoto wao hadi saa moja baadaye, mmoja wa madaktari waliyekuwa wakimhudumia Mariam alipotoka nje.
“Anaendeleaje sasa?” Mama Mariam alikuwa wa kwanza kumuuliza daktari.
“Msijali, inabidi mkubaliane na matokeo, maana hatuwezi kubadili kitu kilichopo!” Daktari akasema kwa utulivu sana.
“Dokta sema tu, nini kimetokea?”
“Punguzeni wasiwasi kwanza, tulieni...”
mwenyewe...
Mwili wa mama yake na Mariam ghafla ulikuwa kama umemwagiwa maji ya baridi, alishahisi lazima mwanaye atakuwa amekubwa na matatizo makubwa sana, kitu pekee ambacho kilizunguka ubongoni mwake ilikuwa ni kiifo! Kwa vyovyote vile uso wa daktari yule ulisomeka kwamba taarifa zilizokuwa zikiwajia baadaye zilikuwa za msiba.
Machozi kama maji yalianza kutiririka ghafla machoni mwa mwanamke huyo ambaye uso wake ulishajaa makunyanzi. Machozi yake yalisbabisha hata baba yake na Mariam naye apatwe na wasiwasi mkubwa sana. Hisia za mwanaye alikuwa marehemu ziliutawala moyo wake kwa kasi ambayo hata yeye hakujua ilipotokea!
“Dokta kuna nini, mbona unatutisha?” Baba yake na Mariam akauliza akiwa na wasiwasi mwingi sana moyoni mwake.
“Sema tu, kama mwanangu amekufa, hakuna jambo jipya hapo na wala huna haja ya kujaribu kutuficha!”
“Hapana wazee wangu, hebu tulieni kwanza, hakuna jambo baya lililotokea, na kwa hakika tunahitaji sana msaada wenu katika tatizo hili!”
“Tatizo gani?”
“La binti yenu!”
“Sawa, kwani amekufa?”
“Hapana...Mariam ni mzima na kwa bahati nzuri ameshazinduka sasa, lakini kuna jambo limejitokeza ambalo ndilo lililosababisha nije kuwaona kwanza!”
“Ni nini dokta?” Mama Mariam alikuwa wa kwanza kuuliza kwa sauti iliyojaa wasiwasi mwingi sana.
Angalau sasa tabasamu la baba yake na Mariam sasa lilianza kuonekana, uso wenye makunyanzi ulianza kupotea taratibu na nuru kuanza kushamiri katika nyuso za wazee hawa ambao kwa hakika walikuwa na mapenzi mazito sana kwa mtoto wao.
“Enhee dokta, tatizo ni nini?”
“Binti yenu baada ya kuzinduka tu, ametaja jina la Tom, tena akipiga kelele akidai kwamba anamnyanyasa sana. Sasa sijui kama mnamfahamu huyo Tom!”
“Ndiyo tunamfahamu!”
“Ni nani?”
“Mumewe!”
“Ameachana naye?”
“Hapana, wanaishi pamoja ila leo asubuhi hii ndiyo amekuja nyumbani lakini kabla ya kuzungumza chochote tukashangaa amepoteza fahamu kwa inavyoonekana watakuwa wamekwaruzana kidogo!”
“Ok! Sasa hatua gani mmekwishachukua kama wazazi?”
“Kubwa ambalo kwetu sisi lilikuwa la maana zaidi ilikuwa ni kuhangaikia afya ya binti yetu kwanza, ingawa pia tumejaribu kumpigia mwenziye simu lakini hapatikani!” Baba yake na Mariam alisema.
“Ok! Poleni sana!”
“Tunashukuru, nini kinaendelea kwa muda huu?”
“Mariam itabidi abaki hapa hospitalini kwa siku tatu zaidi, tunahitaji kuwa naye karibu sana kwa kipindi hiki, anahitaji ushauri wa Kisaikolojia na baadaye tutawapa taratibu za kuzungumza naye kwa ukaribu zaidi ili kuweka haya mambo sawa!”
“Tunashukuru sana dokta, tunaweza kumuona?”
“Hakuna shida, lakini tunashauri msimuulize maswali magumu sana kwa kipindi hiki ambacho anaonekana kuwa na mawazo sana akilini mwake, msalimieni na mumpe pole tu, tafadhali msimuulize mambo magumu sana. Akili yake kwasasa inahitaji kupata wasaa wa kupumzika!”
“Hakuna tabu dokta!”
Dakika mbili baadaye wazazi wa Mariam walikuwa wameshaingia katika chumba kile ambapo walimkuta Mariam akiwa amelala juu ya kitanda, macho yake yakiwa yamejaa machozi.
“Mama....baba....” Mariam aliita akionekana kuwa na majonzi sana.
“Mwanangu, pole sana mama...utapona mama usijali!” Mama yake Mariam alisema akimwangalia mwanaye aliyekuwa ametulia kitandani.
Hakuwa na uwezo hata wa kukaa mwenyewe. Mariam alitia huruma sana, muda huo mama yake alipata nafasi ya kuweza kugundua kwamba Mariam alikwa amedhoofu sana, afya aliyokuwa nayo, haikuwa yake ya siku zote. Mariam alikuwa amepungua sana.
“Ahsante mama, lakinia alichonifanyia Tom kinauma sana mama yangu...nimevumilia lakini nimeshindwa!”
“Amekufanyia nini?” Baba yake Mariam akadakia.
“Tom ameamua kuwa na mwanamke mwingine sasa!”
“Umejuaje?”
“Anaishi naye pale nyumbani, mwanzoni alikuwa anafanya siri, lakini sasa ameweka kila kitu wazi, kaamua kuja naye nyumbani na ni muda mrefu sasa mimi nalala chumba cha wageni, Tom amebadilika, ananichukia sana sasa hivi!”
“Usijali mwanangu, kila kitu kinapangwa na Mungu, binadamu hatuwezi kupanga mambo mama, na hata kama tukipanga Mungu mwenyewe ndiye mwenye uwezo wa kubadilisha, kitu cha msingi kwako kwa sasa ni kutuliza akili yako na kumwachia Mungu kila kitu! Yeye ndiye atakayejua kitu cha kufanya, atakupigania na kukufanya huru tena, mkabidhi yeye kila kitu na maisha yako yatakuwa mapya mwanangu. Mungu ni kila kitu mama, asikudanganye mtu mwanangu!” Mama yake Mariam alihakikisha anamuweka sawa mwanaye ili aweze kukabiliana na tatizo alilokuwa nalo.
“Lakini mama, hamuwezi kuzungumza naye, nampenda sana Tom wangu mama, nampenda Tom, nitawezaje kuishi bila yeye?”
“Sawa, acha tujaribu kwanza, lakini nakusihi tuliza akili yako mama, afya yako imezorota sana mwanangu, kumbuka sisi wazazi wako tupo na tunakupenda sana, hatutaweza kukubali tukuache uteseke, sawa mama?” Mama Mariam alizungumza kwa sauti ya upole iliyojaa mapenzi mazito.
“Sawa mama, lakini lazima mjaribu kuzungumza na Tom kwanza!”
“Sawa, usijali!”
Baada ya hayo, wazazi wa Mariam wakatoka nje ya chumba kile na kuwaacha Madaktari wakiendelea kumtibu Mariam.
******
“Karibuni sana, sijui mnamuhitaji nani?” Ilikuwa sauti ya Mayasa ambayo ilitokea puani huku ikiwa na sifa zote za ushangingi.
“Mwenye nyumba!” Mama yake na Mariam akasema kwa sauti tulivu sana.
“Hivi nyie ni kina nani?”
“Siyo kazi yako binti, nahitaji kuonana na mwenye nyumba!” Mama Mariam akasisitiza.
“Unajua nawashangaa sana, haiwezekani nyie mkawa wageni wa hapa halafu mnashindwa kujua kuwa mimi ndiyo mama mwenye nyumba!” Mayasa akasema kwa nyodo za wazi kabisa.
Ilikuwa kauli kali ambayo ilimnyomnyong’onyesha sana mama Mariam na mumewe.
“Sikiliza binti, tunahitaji kuonana na Tom!” Baba Mariam akasema kwa sauti ya ukali.
“Oh! Tom, sasa mtaingia ndani au nimuite hapa nje?”
“Mwite huku nje, tutazungumza naye hapa hapa!”
“Nimwambie ni akina nani?”
“Wageni wake wa kibiashara!”
“Ok!” Mayasa akaondoka na muda mfupi baadaye, Tom akaja akiwa ameongozana na Mayasa.
“Mnataka nini kwangu?” Tom akauliza kwa ukali sana.
“Unasemaje?” Baba yake Mariam akauliza kwa sauti iliyojaa mshangao mkubwa.
“Kwani masikio yako umeweka pamba? Kwanza ondokeni kwangu, sina muda wa kupoteza kuzungumza na nyie, mnanipotezea muda wangu wa kustarehe na mpenzi wangu!”
“We’ Tom umechanganyikiwa? Hujui kuwa sisi ni wakwe zako? Tumekuletea taarifa muhimu, mwenzako amelazwa Muhimbili!”
“Mwenzangu ndiyo nani?”
ITAENDELEA
0 Comments