Macho ya Mariam yaliganda katika saa ya ukutani iliyokuwa ikionyesha kuwa ilikuwa imeshatimia saa 7:55 usiku! Zilibaki dakika tano tu, kabla ya kufika saa 8:00, muda ambao kwa hakika, wanandoa wengi huwa katika harakati za kutafuta watoto!
Mariam alikuwa sebuleni akiwa anamsubiria mume wake bila mafanikio. Machozi yake sasa yalikuwa ya kawaida. Vituko na mateso kutoka kwa mumewe vilizidi, hakuona kama alikuwa na thamani kwa mumewe tena. Siku zote alikuwa wa kumangwa na kutukanwa kuwa yeye mgumba, neno lililomuuma sana.
“Kwahiyo kwasababu sijashika mimba ndiyo anichukie kiasi hiki? Tom hanitendei haki, ananinyanyasa!” Mariam alisema kwa sauti kubwa na kuamua kwenda chumbani kulala, hapakuwa na matumaini ya Tom kurejea.
Asubuhi ya saa 4:30, gari la Tom lilikuwa likipiga honi nje, mlinzi akafungua na Tom akaingiza gari na kuegesha mahala pazuri. Akashuka na kuingia ndani. Alipokutana na Mariam sebuleni, hakuonyesha kama kuna kosa alilokosea, akamsalia katika hali ya kawaida kabisa.
“Umeamkaje Mariam?!” Tom akamsalimia huku akielekea chumbani.
“Salama!” Mariam alipojibu, Tom akaongeza mwendo kwenda chumbani.
Mariam hakuweza kuvumilia zaidi, akamfuata nyuma nyuma hadi chumbani. Hakuwa na ukali kwa mume wake, akamwacha akavua nguo na kwenda bafuni, aliporudi ndipo alipomwomba kuzungumza naye.
“Lakini mume wangu, kwanini umebadilika tabia kiasi hiki? Kila siku unalala nje, kwanini lakini?” Mariam akamwuliza Tom.
“Mazungumzo yenyewe ndiyo haya?”
“Ndiyo, kwani unaona ni madogo mume wangu?”
“Makubwa, tena makubwa sana!”
“Sasa una mpango gani?”
“Wa kuendelea kulala nje kila siku!”
“Naomba usifanye hivyo Tom wangu, unajua ninakupenda sana!”
“Hata mimi nakupenda sana, lakini kipo kinachokifanya nilale nje, sasa kama unataka nianze kulala nyumbani, basi niruhusu niwe nakuja na kinachokifanya nilale huko nje!”
“Hilo ni jambo dogo sana kwa mtu anayempenda mpenzi wake kama mimi. Hakuna tabu, nimekuruhusu!”
“Kweli?”
“Niamini mpenzi wangu!” Wakakumbatiana kwa furaha.
Siku nzima Tom alishinda nyumbani akiwa na mkewe, tena akijitahidi kumpa haki ya ndoa kwa kikamilifu, lakini jioni akamuaga Mariam kuwa anatoka kidogo.
“Unakwenda wapi tena?”
“Kuchukua hicho kinachonifanya nisilale nyumbani karibu kila siku!”
“Sawa!” Mariam alijibu akitabasamu.
******
Mariam alichukulia maneno ya Tom kama utani, hakujua kama mwenzake alikuwa akimaanisha alichokuwa akikizungumza. Tom alipoondoka, moja kwa moja alikwenda nyumbani kwa Mayasa ambaye alimkuta akitizama luninga sebuleni.
“Njoo chumbani nina habari njema mpenzi wangu!”
“Habari njema? Kuhusu nini tena?”
“Jiandae tuondoke!”
“Tunakwenda wapi?”
“Nimesema jiandae twende!” Ndani ya dakika kumi tu, Mayasa alikuwa ameshamaliza kuvaa na walikuwa njiani wakielekea nyumani kwa Tom, ingawa Mayasa alikuwa hajui.
“Tunakwenda wapi lakini?”
“Leo tunaenda kulala kwangu, nataka Mariam ajue nina akili na nilifunga naye ndoa kwa bahati mbaya, wewe ndiye unayefaa kuwa mke wangu wa ndoa na siyo yeye!”
“Sijakusikia vizuri, umesema tunaenda wapi?”
“Nyumbani kwangu!”
“Nakupenda sana Tom, kweli sasa umeamua kudhihirisha penzi lako kwangu, naomba ukanyage mafuta sawasawa tumuwahi huyo mwehu wako!” Mayasa alimwambia Tom kwa sauti iliyojaa mahaba mazito, kweli Tom akafuata maagizo aliyopewa na Mayasa, akakanyaga mafuta kisawa-sawa.
Alikuwa anamuwahi Mariam, hakika alidhamiria kumuumiza.
Mayasa alikuwa akishangilia ushindi moyoni mwake, alijiona mwenye akili kuliko kawaida. Alimshukuru sana mganga wake kimoyomoyo, akiamini ndumba zilikuwa zinafanya kazi ipasavyo.
“Huu ni mwanzo mzuri sasa, naamini kila kitu kitakwenda sawa, utajiri wa Papaa Bill utakuwa wetu na siyo wake.
“Halafu inaonekana hicho kimwanamke chake hakijui mapenzi, sasa ngoja nimuonyeshe mji, mimi ndiyo mtoto wa mjini bwana!” Aliwaza Mayasa akimtizama machoni Tom.
“Tom...” Mayasa akaita.
“Nakusikiliza mpenzi wangu!”
“Nimeamini kwamba unanipenda sana, wewe ni mwanaume wangu wa maisha na sasa najihakikishia kuwa na wewe siku zote za maisha yangu.”
“Ni kweli kabisa, usiwe na wasiwasi Mayasa wangu, yaani mpaka najuta kumfahamu Mariam, sijui kwanini nilikutana na yule mjinga-mjinga, yaani nina mkosi wa ajabu sana, simpendi yule mwanamke hata chembe!”
“Pole sana, lakini mimi nipo kwa ajili ya kukupa furaha katika maisha yako, usiwe na wasiwasi mpenzi wangu, kila utachokitaka kwangu utakipata, sawa sweetie wangu?!” Sauti ya mahaba ilimtoka Mayasa, tena kwa kutokea puani.
Tom alikiri kwamba mwanamke yule alifanikiwa kwa kiasi kikubwa sana kuufanya moyo wake mateka. Hakuwa na la kufanya zaidi ya kukubali kuwa katika himaya ya mapenzi ya Mayasa.
“Naweza kukuliza!” Mayasa akamwuliza Tom.
“Maswali mangapi?”
“Moja tu!”
“Uliza.”
“Nataka kujua tutalala wapi?”
“Una swali la nyongeza?”
“Hapana.”
“Umesema unataka kujua mahali tutakapolala?”
“Ndiyo!”
“Hilo tu?”
“Kwani dogo?”
“Ok! Vizuri sana, acha nikujibu kwa vitendo!”
Alichokifanya Tom ni kuchukua simu yake kisha kubonyeza namba za Mariam, ikaita na baada ya muda ikapokelewa. Tom akaweka sauti ya juu ‘loud speaker’ kisha akaanza kuzungumza naye.
“Vipi Tom mume wangu?”
“Salama mama, habari za hapo nyumbani?”
“Nzuri, sijui wewe?”
“Mie ni mzima wa afya njema!”
“...ah Tom wangu, kama kuna siku umenifurahisha ni leo, yaani umenipa raha sana!”
“Kweli eh?!”
“Saaana, halafu naomba uwahi, usiku wa leo utakuwa kwa ajili yetu, nitakuonyesha mambo zaidi ya mchana!”
“Sawa mpenzi, hakuna shida, umepika nini?”
“Chakula chako ukipendacho!”
“Nini?”
“Bunia!”
“Kama siyo ndizi samaki, basi itakuwa ugali samaki!”
“Ni ugali samaki mpenzi wangu, mboga za majani na mtindi, najua leo utajilamba sana!”
“...hasa kama samaki wenyewe watakuwa sato!”
“Ni lini nimekupikia samaki wengine tofauti na sato?”
“Utakuwa mlo mzuri sana kwangu!”
“Basi uwahi Tom, angalau tuoge pamoja!”
“Hakuna tabu, lakini nitakuwa na mgeni, sasa ni vizuri kama utaandaa kile chumba cha wageni vizuri!”
“Hilo tu mume wangu, labda useme lingine!”
“Na chakula chake pia!”
“Hakuna shida!”
“Basi baadaye mpenzi wangu!”
“Sawa...mwaaaaaaa....”
“Mwaaaaaa...” baada ya mazungumzo hayo kwenye simu, Mariam alimuangushia busu mwanana Tom ambaye naye alijibu kisha akakata simu.
Baada ya hapo akamgeukia Mayasa akamwangalia kwa jicho lililojaa mahaba, huku akitabasamu kwa furaha. Alikuwa akishangilia ushindi!
“Nadhani umesikia kila kitu!”
“Sina la kuongeza mpenzi wangu, sasa moyo wangu mweupeeeee!”
“Leo ni siku yake, atajuta kukutana na mimi, mwanamke ananing’ang’ania utafikiri aliambiwa mwanaume nipo peke yangu? Nimeshafanya kila aina ya vituko lakini hasikii, sijui ni mwanamke wa aina gani yule?”
“Kwanza mwanamke gani mgumba? Subiri nikuzalie watoto haraka-haraka, upate warithi wa mali zako!” Mayasa akadakia.
Ilikuwa kauli ambayo ilimsisimua sana Tom, kuambiwa kwamba angezaliwa mtoto, tena haraka-haraka kulimpa faraja sana moyoni mwake, akawa na matumaini ya kuwa baba baadaye.
“Umenifurahisha sana Mayasa, hakuna kitu ninachokitamani kama kuwa baba, unanifanya nijisikie vizuri sana, ahsante sana mpenzi wangu, ahsante!”
“Tena nipe muda mfupi tu, kutoka sasa!”
“Tutaona!”
“Sasa?”
“Nini tena?”
“Tunakwenda moja kwa moja nyumbani au tunapitia mahali kwanza?”
“Wewe unaonaje?”
“Nilikuwa naona ingekuwa vizuri zaidi kama tutapitia mahali tuzungumze zaidi kwanza, kabla ya kwenda nyumbani. Nafikiri muda mzuri ni kuanzia saa tano au sita za usiku!”
“Tufanye saa saba!”
“Sawa, twende wapi?”
“Corner Bar!”
“Sawa!” Safari yao ikabadilika, wakaenda moja kwa moja Corner Bar, iliyopo Sinza, Afrika Sana, jijini Dar es Salaam.
******
Furaha iliyokuwa moyoni mwa Mariam, haikuwa rahisi kuelezeka, alimuona kama Tom wake alikuwa mpya kabisa, sasa alikuwa na imani kwamba Mungu wake alikuwa ameshamsikia na yake yalikuwa majibu.
Hakuwa na chembe ya hisia tofauti na hizo, hakujua kama muda huo, Tom alikuwa na mwanamke Bar, tena alikuwa akipanga kwenda kulala naye nyumbani kwao. Hilo halikuweza kuchukua nafasi kabisa katika moyo wake.
Alichokifanya ni kuhakikisha anamridhisha mumewe ipasavyo siku hiyo, kitu cha kwanza kabisa kufanya ilikuwa ni kupika chakula kizuri sana ambacho mumewe alikuwa akikipenda sana, ugali sato! Kitu kingine alichokifanya ni kuhakikisha chumba chao kinakuwa kisafi kuliko zote, baada ya hapo akafanya usafi katika chumba cha wageni.
Alipomaliza maandalizi yote hayo, akakaa sebuleni akimsubiria kwa hamu kubwa sana mumewe ambaye mpaka wakati huo, saa 2:00 za usiku, wakati taarifa ya habari ya Kituo cha Televisheni cha ITV ikianza, alikuwa hajafika!
Saa moja ikaondoka, ya pili, tatu na hatimaye ilifika saa 6:00 za usiku, Tom akiwa bado hajafika, hapo ndipo alipoanza kupatwa na wasiwasi ambapo aliamua kumpigia simu. Hata hivyo simu yake haikupatikana!
Hakuingia chumbani, akabaki pale pale sebuleni akimsubiria mumewe kwa shauku kubwa! Saa saba kasarobo za usiku, honi ilisikika getini, Mariam hakuwa na mashaka kwamba aliyekuwa mlangoni alikuwa mumewe. Mlinzi akafungua geti, Tom akaingia ndani na kuegesha mahala pazuri.
Akafungua mlango na kushuka garini, kisha akazunguka upande wa pili na kumfungulia Mayasa, akashuka.
“Karibu nyumbani mpenzi!”
“Ahsante sana.”
“Twende.”
“Tangulia.” Wakaongozana moja kwa moja, hadi ndani.
Mariam akawapokea kwa furaha sana, hakujua kilichokuwa nyuma ya pazia. Tofauti na matarajio yake, Tom alipita moja kwa moja na Mayasa hadi katika chumba anacholala yeye na Mariam kila siku.
Mariam akashindwa kuelewa kilichokuwa kikiendelea, kuna wakati alikuwa akifikiria labda mumewe aliamua kumfanyia mzaha. Alidumu sebuleni kwa dakika mbili tu, sebule haikukalika tena, akaondoka na kuwafuata chumbani. Dakika mbili zilikuwa nyingi sana kwa Tom na Mayasa.
Aliwakuta wakiwa kama walivyozaliwa, huku wakicheza michezo ya kimahaba bila wasiwasi!
“Tom!!!”
“Mariam!?”
“Nini unafanya na huyu mwanamke huku chumbani kwetu?”
“Sitaki kuamini kama macho yako yamepoteza uwezo wa kuona kiasi hiki!” Tom akasema kwa sauti tulivu sana, ambayo ilionekana dhahiri kabisa alidhamiria.
“Toooom...”
“Yes Mariam!”
“Umeona haifai kufanya uchafu wako huko nje, na sasa umeniletea hapa nyumbani kabisa!” Sauti ya Mariam sasa, ilianza kukata-kata, huku machozi yakifanana kabisa na maji machoni mwake.
“Lakini ukiona hivi ujue hutakiwi, kwanini unang’ang’ania? Mwanamke gani wewe, hata shepu huna, hebu ona wenzako tulivyojazia...hivi wakati wazuri tunaumbwa, we’ ulikuwa wapi mwenzetu? Hebu toka utuachie nafasi tujinafasi!” Mayasa akasema, akimtizama Mariam kwa dharau sana.
Wakati huo Mayasa alikuwa akijitingisha-tingisha akiwa kama alivyozaliwa. Mapigo ya moyo wa Mariam yaliongezeka kasi kuliko kawaida, akahisi kizunguzungu na kuanguka chini kama gunia la mchele.
“Haaaaah, Mariam?!” Tom akapiga kelele.
“Wa nini, mwache afe!” Mayasa akasema.
“Lazima tumsaidie!”
“Sasa amua kuwa na mkeo au mimi!” Mayasa akasema akianza kuvaa nguo zake tayari kwa kuondoka.
“Usifaye hivyo Mayasa, lakini tunatakiwa kumsaidia!”
“Inaonekana bado unampenda huyo mkeo, sasa baki naye!” Sasa Mayasa alikuwa anatoka nje ya chumba kile.
Tom hakutaka kuruhusu jambo lile litokee, akamfuata na kumrudisha chumbani, pamoja na kwamba moyo wake ulikuwa ukimuuma sana, lakini kwa kumridhisha Mayasa, Tom akaamua kumburuza Mariam hadi sebuleni kisha akarudi chumbani kulala na Mayasa. Hadi wakati huo, Mariam alikuwa hajazinduka.
Kitendo cha Tom kukubali kumuacha Mariam akiteseka sebuleni na kwenda chumbani kulala na Mayasa, kilimfurahisha sana Mayasa, alijiona mwanamke mshindi ambaye ana nguvu ya ushawishi. Hali ilikuwa tofauti sana na Tom, yeye moyoni mwake alikuwa mwenye uchugu mwingi sana, ingawa ni kweli alikiri kwamba Mayasa alikuwa moyoni mwake zaidi kuliko Mariam.
“Umenifurahisha sana mpenzi wangu, sasa naamini kweli unanipenda kwa mapenzi ya dhati, wewe ndiye mwanaume wa maisha yangu, siwezi kukuacha hata siku moja!” Mayasa akasema akimkumbatia Tom aliyekuwa anaonekana dhahiri hana furara aliyokuwa nayo awali.
Jambo hilo liligundulika haraka sana na Mayasa, alijua wazi kwamba Tom hakuwa na furaha aliyokuwa nayo awali, jambo ambalo kwa kiasi kikubwa hakulipenda, siku zote alitaka kuibuka mshindi, kupotea kwa furaha ya Tom, kwa kiasi kikubwa kulimaanisha ushindi wake ulikuwa katika hati hati za kutoweka.
Ni jambo ambalo Mayasa alipingana nalo siku zote, kwake kulikuwa hakuna kitu kinachoitwa kushindwa, ushindi ndiyo kitu pekee ambacho kilikuwa na maana kubwa katika maisha yake, akili yake iliwaza ushindi pekee, bila kujali njia ambayo ushindi huo ungepatikana!
Alimwangalia Tom kwa jicho la hasira, kisha mkono wake akaupeleka moja kwa moja hadi kwenye sidiria yake alipokuwa amefunga hirizi yake na kuiminya kwa nguvu!
“Una nini Tom?” Mayasa akauliza kwa ukali sana.
Tom hakujibu!
“Hivi, nazungumza mwenyewe?”
“...hapana...” Tom akajibu kama alikuwa ametokea katika usingizi mzito.
“Bali?”
“Mbona upo hivyo?”
“Vipi Mayasa?”
“Umeniitaje?!”
“Mayasa!”
“Yaani umefikia hatua unaniita Mayasa?”
“...samahani mpenzi wangu, nilipitiwa kiudogo, unasemaje mpenzi wangu?”
“Inaonekana bado unampenda huyo mkeo, kama ndivyo ni bora uniambie niondoke zangu, sikulazimishi kuwa na mimi!”
“Hapana, kwani kuna nini?”
“Mbona sioni uchangamfu wako? Hukuwa hivyo Tom, naona una mawazo ya mkeo!”
“...hapana...nani? mariam? Mimi...ah no! Labda siyo Thomas, siwezi kabisa kuwa na mwanamke mbovu kama yule, tena sijui nilikutana naye usiku au vipi? Tena usikumbushe kuhusu hilo lijanamke, hebu tuzime taa tulale...” Tom akajikuta akiropoka bila kujua maneno yale yalitokea wapi.
Kwa Mayasa ulikuwa ushindi ambao alikuwa akiutegemea siku zote. Kama ni barabara, basi hiyo ilikuwa imenyooka! Hapakuwa na kitu kingine zaidi kupanda kitandani na kulala usingizi wa kiutu uzima!
***
Kila alipojaribu kuvuta kumbukumbu juu ya watu waliokuwa mbele yake, hakuweza kuwajua kabisa. Hilo halikuwa na maana sana kwake kwa wakati huo, lakini kwanini waliamua kumtesa na kumnyanyasa ndiyo jambo ambalo lilimnyima kabisa raha.
Huyu ni Tom, akiwa katikakati ya wanaume sita waliokuwa wamejazia vyema vifuani mwao, wakimwangalia kwa hasira huku wakimhakikishia kifo!
INAENDELEA
0 Comments