Ticker

6/recent/ticker-posts

Ad Code

Responsive Advertisement

Simulizi: Mwanamke jini sehemu ya kumi na tano (15)



Tulipofika pwani yule jini alinitafutia mahali chini ya mti akaniambia.

“Kaa hapa hadi saa tisa usiku. Utaona msafara mrefu wa majini unapita kutoka upande wa kusini kwenda kaskazini. Subiri mpaka utakapowaona mjini waliobeba kichanja (aina ya jukwaa). Ukiwaona majini hao wafuate uwasimamishe.

“Pale juu ya kichanja utamuona Sultani wa majini amebebwa, utamgundua kutokana na kilemba chake kikubwa cha rangi nyeupe, utampa hii barua iliyoandikwa na mzee Jabalkeysi” Jini huyo akaniambia nna kunipa ile bahasha aliyokuwa ameishika.

“Nikishampa itakuwaje?” nikamuuliza.

“Ataisoma halafu kuna kitu atakwambia. Hivyo ndivyo nilivyoagizwa na mzee Jabalkeysi”

Yule jini aliponiambia hivyo akaondoka na kuniacha pale pale. Hapo mahalli palikuwa na mazingira ya kutisha sana, halafu niliambiwa nikae peke yangu hadi saa tisa uiku nisubiri msafara wa majini. Hao majini hawatanidhuru? Nikajiuliza.

Pamoja na hofu niliyokuwa nayo ilibidi nikae hapo kwani sikuwa na la kufanya. Hata kama ningetaka nikimbie nirudi kwetu ningerudi kwa njia gain?.

Nikakaa hapo huku nikitetemeka kwa baridi. Mawazo na hofu vilikuwa vimesonga kwenye moyo wangu. Nilikuwa nikijiuliza maswali chungu nzima yasiyokuwa na majibu. Nikatamani Zena atokee pale anirudishe kwetu lakini hakukutokea Zena wala yeyote.

Kila wakati nilikuwa nikitazama saa yangu kujua majira yalivyokuwa yanakwenda. Kwa mtu mwenye wasiwasi na hofu kama nilivyokuwa mimi, nilihisi muda ulikuwa hauendi kabisa na baridi ilikuwa ikizidi kuniingia kwenye mifupa.

Baada ya masaa machache lakini niliyoyaona marefu ikafika saa tisa usiku. Jinsi nilivyokuwa nimejificha pale chini ya mti haikuwa rahisi kuonekana labda kwa jini aliyekuwa karibu.

Ghafla nikauona ule msafara nilioambiwa. Walikuwa majini waliovaa nguo nyeupe tupu wameandamana wakitokea upande wa kusini kuelekea upande wa kaskazini. Niliouna msafara huo tangu ulipoanza kutokea.

Nilipotupa macho nikakiona kichanja kilichokuwa kimebebwa katikati ya msafara huo. Kilikuwa kimepembwa kwa vitambaa vyeupe na kilikuwa na vidirisha.

Nikajiuliza kama ningekuwa na moyo na ujasiri wa kujitokea na kusimamisha msafara huo wa majini? Lakini nikajiambia hilo ndilo nililokuwa nikilisubiri pale, kwa hiyo ilikuwa lazima nilitekeleze.

Ule msafara ulifika karibu, nikainuka ghafla na kuukimbilia huku nikipiga kelele.

“Jamani subirini, nina ujumbe wa Sultani!”

Mara moja nikaouna msafara huo umesimama. Majini hao wakawa wananitazama mimi.

Yalikuwa ni maingira ya kutisha sana lakini yale matatizo niliyokuwa nayo yalinipa ujasiri. Nikaufikia ule msafara.

“Jamani nina ujumbe wa Sultani” nikawambia huku nikimtazama Yule jinni aliyekuwa kwenye kile kichanja kilichotengezwa kama gari lililobebwa likiwa na madirisha yenye mapazia.

Jini aliyekuwemo kwenye kichanja hicho alikuwa mfupi na mnene mwenye ndevu na sharubu nyeupe. Alikuwa amevaa kilemba cheupe na joho la rangi nyeupe. Alionekana kama sultani hasa.

Kulikuwa na jinni mmoja allinipa ishara nisogee pale kwenye kichanja. Nikasogea na kumuona vizuri yule sultani.

“Assa;aam alaykum” akaniambia kwa sauti tulivu iliyonipa matumaini.

“Wa alayka salaam” nikamjibu na kunyoosha mkono wangu kumpa ile barua.

Aliipokea akaikunjua na kuisoma.

Alipomaliza kuisoma aliniuliza.

“Wewe ndiye Amour?”

“Ndiye mimi”

Nilipomjibu hivyo aliwambia walae majini.

“Subirini kidogo hapa kuna mashitaka”

Majini wote wakanyamaa kimya kusikiliza.

“Ni nani ambaye anamfahamu Zainush binti Jabalkeyss?”

Majini kadhaa wakajitokeza wakidai kuwa wanamfahamu.

“Ni nani ambaye anaweza kumleta hapa kwa haraka sana”

Wale majini wote wakanyoosha vidole juu, kila mmoja akionesha kuwa angeweza kumleta Zainush kwa haraka.

“Wewe unaweza kutumia muda gani kumleta hapa?” Sultani wa majini akamuuliza mmoja wa wale majini.

“Mimi naweza kumleta chini ya dakika moja tu”

“Utatuchelewesha” Sultani huyo wa majini alimwammbia akamtazama jinni mwingine.

“Je wewe unawea kumleta kwa muda gani?”

“Mimi naweza kumleta chini ya nusu dakika”

“Wewe pia utatuchelewesha. Hakuna anayeweza kumleta chini ya robo dakika?”

Akatokea jinni mmoja mzee lakini aliyeonekana kuwa na nguvu.

“Mimi nawea kumleta” akasema.

“Kwa muda gani?”

“Kwa kiasi cha kufumba na kufumbua tu, nitakuwa nimeshakuja naye”

“Wewe nenda kamlete. Tunakusubiri”

Hapo hapo Yule jinni alipotea mbele ya macho yangu. Hata kabla sijafumba macho yangu na kuyafumbua nikamuona Yule jinni akitua tena akiwa peke yake tena jicho lake la mkono wa kushoto likiwa linavuja damu.

“Yuko wapi Zainush?” Sulatani wa majini akamuuliza akiwa amekunja uso.

“Nimeshindwa kumkamata. Kwana nilihangaika sana kumtafuta. Nilimkuta katika visiwa vya Comoro akinywa mvinyo na wasichana wenzake wa kijini. Nilipotaka kumkamata wakatokea walinzi wao wakanishambulia na kunipasua jicho langu”

“Zainusha ndiye aliyekufanyia hivyo? Basi ataniona” Yule Sultani alliyeonesha kukasirika alisema kasha akawaita majini wawili kwa majina.

“Harishi na Kaikushi!”

Majini hao wakafika mbele yake. Walikuwa vibonge vya majini. Kila mmoja alikuwa ameshika jambia lililokuwa linameremeta.

“Mwende na huyu nyumbani kwake. Mtakapomuona Zainusha anamfuata mkateni kichwa chake mniletee au mkiweza mleteni kwangu akiwa mzima, nije nimfunze adabu. MMenisikia?”

“Tumekusikia bwana mkubwa” majini hao wakamjibu.

“Haya nendeni naye”

Msafara huo ukaendelea na safari. Mimi na wale majini tulifuatana hadi kwenye ule mti nilipokuwa nimeketi nikachukua mabegi yangu. Jini mmoja akanishika mkono na kuniambia nifumbe macho. Nikayafumba.

Baadaye nilisikia sauti yake ikiniambia.

“Sasa fumbua macho yako”



Nikafumbua macho yangu na kupigwa na mshangao.

Nilishangaa baada ya kujikuta sikuwa tena pale ufukweni mwa bahari, bali nilikuwa mbele ya mlango wa nyumba yangu iliyokuwa eneo la Msambweni mjini Tanga.

Mabegi yangu mawili yalikuwa chini mbele yangu. Wale majini wawili sikuwaona tena.

Nikatazama huku na huku kisha nikafungua mlango wa nyumba yangu na kuingia ndani. Kwa vile ilikuwa usiku niliwasha taa. Mwanga ukaingia kwenye sebule ya nyumba yangu.

Sebule ilikuwa imejaa vumbi kwa vile haikuwa imefanyiwa usafi kwa muda mrefu. Ubuibui ulikuwa umetanda kila kona.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Nikafungua mlango wa chumbani mwangu na kuingia. Humo namo mlikuwa mmejaa vumbi. Hata hivyo nilishukuru kuona nilikuwa nimerudi salama nyumbani kwangu bila ya Zena.

Nilifanya usafi mle ndani kisha nikaenda kuoga. Baada ya kuoga nilifungua kabati nikakuta baadhi ya nguo zangu zimo kama nilivyoziacha.

Nikabadili nguo kisha nikahifadhi zile dola na dhahabu niliotoka nazo Somalia.

Baada ya hapo nilitoka kwenda kuonana na ndugu na jamaa.

Kwanza nilikwenda kwa mama yangu nikiwa sijui kama yuko hai au ameshakufa. Nilipofika nilimkuta mama yangu akizungumza na kaka yangu.

Waliponiona walipatwa na mshangao.

“Amour!” kaka yangu alimaka peke yake kama vile hakuyaamini macho yake.

Nikakumbatianna na mama yangu kisha nikakumbatiana na kaka yangu.

“Unatoka wapi Amour?” mama yangu akaniuliza.

Nikawaelea mkasa uliokuwa umenikuta.

Mkasa huo uliwashangaza sana.

“Sisi tulidhani kuwa umeshakufa” Kaka yangu akaniambia na kuongea.

“Tulishakufanyia hitima”

“Sikufa. Niko hai na leo nimerudishwa tena. Kwa kweli nashukuru”

Baada ya siku ile nilikaa kama wiki moja hivi nikiwatemebelea ndugu na jamaa niliopotezana nao. Siku hiyo nikiwa nyumbani kwangu saa sita usiku nikasikia mlango wa mbele unabishwa. Nikaenda kuufungua. Kwa mshituko mkubwa nilimuona Zainush binti Jabalkeys mbele ya mlango.

“Hujambo Amour” akanisalimia kwa bashasha.

Nikajikuta nikimjibu.

“Sijambo. Karibu ndani”

Zainusha akaingia ndani na kukaa sebuleni.

“Waai wangu waliniudhi sana. Wananifanya kama mimi mtoto mdogo wakati mimi ni mtu mzima na nina maamuzi yangu”

Wakati Zainusha akainieleza hivyo ghafla wakatokea wale majini wawili walioambiwa wakimuona ainusha ananifuata wamkate kichwa au wamkamate na kumpeleka kwa sultani wao.

Nilipowaona kajini hao nikajiambia Zainusha sasa amekwisha.

Majini hao walipotaka kumvamia Zena wakiwa na majambia yao mikononi ainusha alikurupuka akaruka upande mwingine wa sebule na kuwauliza majini hao kwa ukali.

“Mna nini nyinyi wapumbavu! Mnataka nini kwangu?”


“Unatuita sisi wapumbavu! Ngoja tutakuonyesha!” Mmoja wa majini hao alimwambia Zainush kwa hasira kabla ya kuliinua jambia lake.

“Tumeambiwa tukupeleke mzima au tukukate kishwa lakini sasa tutakupeleka ukiwa vipande vipande” jinni huyo aliendea kumuambia huku akimsogelea Zainush ili amkatekate.

Zainusha alipiga ukulele mkali akarudi hatua moja nyuma kabla ya kuuvuta unywele wake mmoja kutoka kichwani mwake kisha akaupulizia.

Baada ya kuupulizia unywele huo uligeuka jambia lililokuwa likimeremeta.

Akawambia majini hao kwa sauti ya kishujaa.

“Sasa njooni nyinyi niwararuerarue kama paka aliyeshambuliwa na mbwa!”

Majini hao kwanza walisita kisha ghafla walimfuata Zainush kwa pamoja wakiwa wamepunga majambia yao kwa unyenyekevu wa hali ya juu kama mtu alipigwa na baridi ya Lushoto kule Mkoani Tanga.

Zainusha aliruka upande mwingine huku akitamba na jambia lake. Alilichezesha mikononi kwa haraka haraka kabla ya kulikinga jambia la jinni mmojawapo aliyekuwa amemshushia dharuba.

Baada ya kulikinga jambia hilo Zainusha aliruka tena akamsukumia dharuba jinni huyo ambayo aliikwepa. Kwa muda wa dakika kumi Zainusha aliwakabili majini hao kama mwanaume!

Hawakuweza kumpiga hata dharuba moja japokuwa walikuwa wawili. Zainush alikuwa amefundishwa kupigana na alikuwa shujaa wa kike aliyeweza kupigana na wanaume.

Katika kulikinga jambia la jinni mmoja wapo lililoelekea kichwani mwake ndipo jambia la Zainush lilipokatika vipande viwili. Zainusha alikimbilia upande niliokuwa nimesimama nikiwa nimegwaya. Akaja nyuma yangu na kunishika shati.

“Amour wainue majini hao wataniua!” Zainusha aliniammbia kwa sauti ya huruma.

Kwa kweli nilimuhurumia lakini sikuwa na namna yoyote ya kumsaidia.

Majini hao wakamfuata Zainusha mgongoni kwangu.

“Msimuue! Msimuue!” nikawambia.

Zainusha alijaribu kuwakwepa lakini majini hao walimdaka.

Zainusha alikuwa akipiga kelele na mimi nilikuwa nikipiga kelele kuwambia majini hao wamuachie lakini hakuna aliyenisikia.

Walimbeba Zainush wakatoweka naye pale sebuleni. Sikuwaona tena.

Bila shaka walimpeleka kwa yule sulatani wao aliyewaagiza wamkamate na sijui alifanywa nini kwani tangu siku Zainush sikumuona tena.

Sikujua kama Zainush alifungwa au aliuawa. Lakini nilimkumbuka sana. Hivi sasa nimekuwa tajiri mkubwa na chanzo cha utajiri huo ni yeye.

Kuna wakati huwa najimabia nilifanya kosa kwenda kumshitaki kwa sulatani wao, bora ningemuacha tu kwa sababu nilishamzoea.CHANZO:  https://deusdeditmahunda.blogspot.com/

Nitakusimulia kisa kingine nitakapopata nafasi ili ujue maisha yangu yalikuwaje baada ya hapo na pia ujue kama Zainusha aliibuka tena au la.


MWISHO.



Post a Comment

0 Comments